Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Waziri Mkuu akiwa Kiongozi Mkuu wa shughuli za Serikali Bungeni, hotuba yake imetoa mwelekeo mzuri kabisa wa vikao vyetu vyote vya bajeti za Wizara mbalimbali zitakazofuata. Serikali ya Awamu ya Tano imejenga msingi madhubuti wa kujenga Tanzania ya viwanda ikisadifu na kauli mbiu ya Chama cha Mapinduzi ya CCM mpya na Tanzania mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Magufuli akisaidiwa na Makamu wake wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa imedhamiria kwa dhati kujenga uchumi wa kisasa kwa kuja na mpango wa kuwa na miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta mbalimbali ikiwemo ujenzi wa reli ya kisasa ya kiwango cha kimataifa (Standard Gauge – SGR), mradi mkubwa wa maji wa kufua umeme kutoka Mto Rufiji (Stigler’s Gorge) utakaosaidia kufua umeme wa MW 2,100, hii ikiwa ni katika kuhakikisha Tanzania ya viwanda inafikiwa kwani viwanda bila umeme haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya nishati kutokana na vyanzo mbalimbali kunasaidia sana utekelezaji wa miradi mbalimbali ya usambazaji wa huduma ya umeme kupitia Wakala wa Umeme Vijijini maarufu kama REA. Kwa hakika huduma hii imeleta mabadiliko makubwa katika shughuli za maendeleo vijijini na hivyo kupunguza uhamaji wa watu kutoka vijijini kuhamia vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, naipongeza Serikali kwa kuja na mpango kabambe wa kuimarisha huduma katika sekta ya afya kwa kujenga vituo vingi vya afya katika sehemu mbalimbali ikiwwemo Wilayani Mbogwe ambapo vituo vya afya vya Iboya na Masumbwe ambavyo kwa pamoja vimepatiwa jumla ya shilingi milioni 800 na kwa hakika vituo hivi vimeboreshwa kwa kiwango kikubwa. Kwa hili, tunaipongeza sana Serikali, pia Serikali imetupangia shilingi milioni 500 tunashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya elimu, suala la elimu bila malipo limeleta changamoto kubwa sana na wananchi wengi wamejitokeza kupeleka watoto wao kuandikishwa darasa la kwanza. Katika hali hii Watanzania wengi wamepata fursa ya kupata elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa reli kwa kiwango cha Standard Gauge kunategemewa kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya mawasiliano na uchukuzi, jambo ambalo litaokoa kwa kiwango kikubwa uharibifu wa barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imepiga hatua kubwa sana katika kupambana na biashara ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa viwanja vya ndege na ununuzi wa ndege mpya utachangia kwa kiwango kikubwa ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya utalii kwa kuleta wageni toka ng’ambo na kuleta chachu ya upatikanaji wa pesa za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni sekta nyeti sana nchini kwani kinaajiri watu wengi sana karibu asilimia 75. Hivyo napenda kuishauri Serikali kuwekeza zaidi katika suala la utafiti wa ardhi, mbegu, magonjwa pamoja na visumbufu vya aina mbalimbali. Upatikanaji wa pembejeo zikiwemo mbolea na mbegu bora kutasaidia kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao ya chakula na ya biashara ili yaweze kuwa ni chachu ya kuifanya Tanzania ya viwanda iweze kutimia maana viwanda vyetu vitatumia malighafi kutokana na mazao ya kilimo. Naiomba Serikali izidi kuwekeza ama kukaribisha wawekezaji katika viwanda vya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.