Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ni kuhusu Sekta ya Kilimo; kwa kuwa mwaka huu Kanda ya Kaskazini hasa Mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro inakabiliwa na ukame kufuatia mvua za masika kutonyesha, nashauri Serikali iandae bajeti ya kutosha na kuweka utaratibu wa kuwaletea wananchi chakula cha bei nafuu toka mikoa yenye chakula cha kutosha mwaka huu.

Pili ni kuhusu Sekta ya Mifugo na Uvuvi; nashauri Serikali iwekeze katika uanzishwaji wa viwanda vya kuchakata mazao ya mifugo na uanzishwaji wa masoko ya ndani ya uhakika. Pia nashauri Serikali ipange bei elekezi kwenye bidhaa za mifugo na ipange bei ya kishindani kwa kulinganisha na bei ya bidhaa husika katika masoko ya nchi jirani kama vile Kenya. Vile vile nashauri bei ya nyama ya mbuzi, kondoo na ng’ombe kwa kilo ipangwe na Serikali na mifugo minadani iuzwe kwa kupimwa kwenye mizani na bei ya mifugo kwa mnyama hai (live weight) ipangwe na Serikali kama ilivyo kwa mazao ya kilimo (mazao ya biashara).

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ni Sekta ya Utalii; nashauri Serikali ipanue wigo wa biashara ya utalii kwa kuunganisha utangazaji wa vivutio vya utalii nchini ili pamoja na wanyamapori ambao ndio kivutio kikuu, pia tutangaze utalii katika misitu yetu ya asilia (Nature reserves) sambamba na utalii wa utamaduni (cultural tourism). Pia nashauri channel yetu ya utalii itangaze kwa lugha mbalimbali za mataifa yanayopenda utalii. Sambamba na hilo tuombe airtime space kwenye channel za Serikali za mataifa yanayopenda utalii na vivutio tulivyonavyo. Baadhi ya Channels hizo ni pamoja na PBS ya Marekani (Public Broadcasting Service), BBC, DW na National Geographic Society.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika, utitiri wa kodi uunganishwe ili kuwa na kituo kimoja (one stop center) na kodi moja jumuishi ili kuondolea wawekezaji na wateja usumbufu na urasimu usio wa lazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, Sekta ya Ardhi; nashauri Serikalli iongeze bajeti na rasilimali fedha, vifaa na wataalam wa kutosha hadi ngazi ya Halmashauri za Wilaya nchini ili kuongeza kasi ya kupanga, kupima na kumilikisha kila kipande cha ardhi ya nchi yetu kulingana na Sera na Mpango wa Taifa wa Ardhi 2013 – 2033.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano ni Sekta ya Barabara; katika kufungua barabara zenye kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi, naomba Serikali itoe kipaumbele mwaka huu wa fedha kumalizia kipande cha barabara chenye urefu wa kilomita 41 zilizobaki kwenye barabara ya Sanya Juu hadi Kimwanga kuzunguka Mlima Kilimanjaro. Pia barabara ya Siha/Sanya juu – Longido (kilomita 56) ipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, kuhusu Kazi, Ajira na Vijana; nashauri Serikali mgawo wa 10% ya mapato ya ndani ya Halmashauri zetu za Wilaya ambapo akinamama na vijana hupewa mikopo isiyo na riba kwa uwiano wa 4% kwa kila kundi na watu wenye ulemavu 2%. Nashauri watu wenye ulemavu wasikopeshwe hiyo 2% wanazogaiwa bali wapewe kama msaada (seed fund) wa kuwawezesha kuanzisha miradi ya kujikimu kimaisha. Kwa kuwa watu wenye ulemavu huwategemea ndugu na jamaa na watu wenye mapenzi mema kuwazungushia mitaji yao, mara nyingi kasi ya miradi huwa ndogo na pia uwezo wa kurejesha mikopo yao kwa wakati kuwa hafifu. Hivyo basi nashauri iwe sehemu ya social welfare na uwajibikaji (CSR) wa Serikali yetu kuwapa watu wenye ulemavu hiyo 2% kama msaada na siyo mikopo ya kurudishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira za moja kwa moja katika Utumishi wa Umma; nashauri Serikali iongeze bajeti ya kutoa ajira za moja kwa moja ili kuondoa upungufu mkubwa wa watumishi wa kada mbalimbali unaozikabili Halmashauri za Wilaya zetu na sekta mbalimbali za Serikali. Kwa kutoa ajira za moja kwa moja Serikali itaondoa changamoto kubwa iliyopo ya kuwa na utitiri wa watumishi wanaokaimu nafasi mbalimbali na kwa muda mrefu. Jambo hili linaathiri utendaji (performance) katika Halmashauri ya Wilaya yangu ya Longido ambapo zaidi ya 50% ya Watendaji wa Vijiji (VEDS) ni watumishi wanaokaimu nafasi hizo na kwa miaka mingi.

Pia kwenye idara za halmashauri tuna upungufu mkubwa na lundo la watumishi wanaokaimu nafasi kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, naomba kutamka kuwa naunga mkono hoja! Ahsante.