Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii, maana yake nilishaanza kukata tamaa, maana yake muda unazidi kwenda. Naomba kwa kuanza kabisa niunge mkono hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ya Bajeti yake na vilevile naunga kwa dhati kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa umahiri wake, kwa uongozi wake na umakini wake wa kusimamia shughuli za Serikali na unaiona katika hotuba aliyoleta mbele ya Bunge hili. Vilevile nitakuwa mnyimi wa fadhila kwa sababu najua kazi wanayofanya Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Angella Kairuki kwa kuweza kumsaidia na kuonyesha mambo mazuri yanayofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa kutumia nafasi hii vizuri, nitajielekeza kwenye uwekezaji na nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kuona mambo kwa upesi kuitoa Wizara hii, Sekta hii kwenye Viwanda na Biashara na kuileta chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa sababu uwekezaji ni suala mtambuka, uwekezaji uko kwenye viwanda, uwekezaji uko kwenye kilimo, uwekezaji uko kwenye elimu na uwekezaji uko kwenye sehemu nyingi. Kwa hiyo, mahali panapofaa ni kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kuona hili, kwa sababu kwa kweli, katika uwekezaji ndiyo tutaongeza mapata ya Taifa hili, bila uwekezaji hatutaweza kuongeza mapato ya Taifa hili. Vilevile, ajira hii inayoliliwa na vijana ambao wako vijijini na ambao wanatoka vyuo vikuu na vyuo vingine itatokana na uwekezaji ambao tutawekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi ya hapo, vilevile uwekezaji ndiyo unatumia teknolojia mbalimbali na kuongeza maendeleo ya nchi yetu. Kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, lakini vilevile kwa ajili ya yeye kusimamia uwekezaji huu kupitia ofisi mbalimbali, Tanzania imekuwa ya saba katika bara la Afrika kuvutia uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, mtaji umeongezeka, uwekezaji umeongezeka kutoka dola 640 mwaka 2005 hapo tulipo mwaka 2016 ilifikia mwaka dola 1,365, ingawa umeteremka kidogo mwaka 2017 kuwa dola milioni 1,180 kwa sababu huu ndiyo mwelekeo wa dunia, siyo wa Tanzania, lakini Tanzania ndiyo iko mahali pazuri na wanaotaka kuja kuwekeza Afrika watataka Tanzania kwanza, kwa ajili ya amani yetu. Vile vile uwekezaji kwenye miundombinu, uwekezaji kwenye maji, uwekezaji kwenye maeneo ambayo yanahitaji kufanya uwekezaji uwe rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo, ningependa kuona kwamba, mwelekeo wa uwekezaji kwa Tanzania pamoja na mazingira mazuri ambayo Serikali imeweka, Tanzania katika nafasi nzuri iendelee kuona kwamba inasahihisha maeneo ambayo yataifanya Tanzania iwe bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo, napenda kuona kwamba mwelekeo wa uwekezaji kwa Tanzania pamoja na mazingira mazuri ambayo Serikali imeweka iendelee kuona kwamba inasahisha maeneo ambayo yataifanya Tanzania iwe bora zaidi. Naomba tuimarishe One Stop Center, kwa sababu bila ya hivyo, kwa mwekezaji kutoka nje au kutoka ndani kwenda BRELA, TRA na sehemu nyingine itamchukua muda na wakati mwingine anakwamishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningeomba tufuate mfano ambao uko Rwanda wa Rwanda Development Company au Center ambapo mambo yote ya uwekezaji yako mahali pamoja na wale ambao wako pale wana uwezo wa kupitisha na wawekezaji wanaweza wakapitishwa sehemu zote hata kwa siku moja. Kwa hiyo, naomba sana sisi Watanzania tuone umuhimu huu badala ya kuwa na TIC peke yake halafu hawana uwezo wa kupitisha kitu cha BRELA ambayo iko viwanda, hawana uwezo wa kupitisha mambo ya TRA ambayo yuko Wizara ya Fedha, tungepaswa kuwa siyo TIC tungekuwa na shirika au taasisi ya uwekezaji ambayo ina watu ambao wanaweza kupitisha kodi kiasi gani na mengine yote yanayohusika kwenye mambo ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Serikali imeimarisha sera, sharia na taasisi. Serikali kwa kuimarisha mazingira ya uwekezaji, kuna Roadmap ambayo imewekwa ambayo kama tutaisimamia vizuri Mheshimiwa Waziri Mkuu uwekezaji utakuja kwa nguvu zaidi. Ni muhimu sana Wizara na taasisi za Serikali zinazohusika katika kutekeleza mpango huu ziwe na mikakati madhubuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kusema ni kwamba Ofisi ya Waziri kama mratibu wa uwekezaji ni muhimu pia kuratibu na kusimamia mpango ambao unapitia Blueprint ya viwanda kwa sababu wakati huu ni wa kuimarisha viwanda, tuiangalie na mahali ambapo kuna upungufu tuweze kuyaboresha. Ukiunganisha hii Blueprint na Roadmap nina hakika nchi hii itajielekeza vizuri kwenye uwekezaji, mapato ya Serikali na uwekezaji unaotoka nje tukiimarisha hatutakuwa tunarudi nyuma bali tunaenda mbele na tutapata mapato zaidi kwenda kwenye elimu, afya na sehemu zingine. Ndugu zangu kama nchi haitatilia mkazo kwenye uwekezaji hatutafanya mambo makubwa tutakuwa tunatumia au tunakula bila kuangalia kesho tutapata faida gani. Tusipowekeza hatuwezi kujiendeleza kwenye mahitaji yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Angellah mwanangu huyu ambaye alikuwa na mimi wakati nikiwa Waziri wa Katiba na Sheria na nimefurahi sana kwa sababu ni mchapakazi na atamsaidia Mheshimiwa Waziri kuona uwekezaji unaenda vizuri na uchumi wa nchi hii utapanda na uchumi ukipanda huduma za jamii na mambo mengine yatakuwa mazuri zaidi. (Makofi)

Nakushukuru sana, nilitaka nijielekeze kwenye uwekezaji kwa sababu najua umuhimu wa uwekezaji ambao sasa hivi unatiliwa mkazo kwa kuwekwa chini ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Naunga mkono hotuba na bajeti hii na hii hotuba itafanya hotuba zingine ziende vizuri. Ahsante sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mwenyekiti wetu. (Makofi)