Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Vicky Paschal Kamata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. VICKY P. KAMATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mungu kwa kututia nguvu na kutuvusha salama katika kipindi kigumu ambacho kilikuwa ni cha kuuguza na hatimaye kumpumzisha mahali pa milele mama yetu mpendwa Paulina. Nimshukuru pia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa upendo, huruma na utu wema aliotuonesha katika kipindi cha kuuguza na hata mpaka mama alipofariki na hata baada ya kumpumzisha katika nyumba ya milele ameendelea kutupa faraja mimi na kaka yangu kwa kutupa maneno ya imani ambayo yametupa nguvu hata tunaweza kuendelea kustahimili kuishi bila mama yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Rais Mstaafu, Mheshimiwa Dkt. Jakaya pamoja na mama yetu mpenzi, Mheshimiwa mama Salma. Nawashukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mawaziri wote, Wabunge, Spika, kaka yangu Rashid Shangazi pamoja na Joseph wa Faraja Fund. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana viongozi wote wa dini, madaktari wote wa Muhimbili na Bugando, wananchi wote wa Geita, wananzengo wenzangu wa Mbweni pamoja na Mpigi kwa faraja kubwa ambayo wametupa na Watanzania wote kwa pamoja ambao wameweza kutufariji na sasa tunaendele vizuri, tunamshukuru Mungu. Raha ya milele umpe ee Bwana na mwanga wa milele umwangazie. Apumzike kwa amani.

WABUNGE FULANI: Amina.

MHE. VICKY P. KAMATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu baada ya kuwa nimekipitia kitabu hiki vizuri na kwa kweli niipongeze sana Serikali kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kutaka kututoa hapa tulipo na kutupeleka mbele zaidi kimaendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nitauanzia kwenye ukurasa wa 53. Ukurasa wa 53 unazungumzia mambo ya elimu bila malipo. Nitasoma kidogo: “Serikali inatekeleza kwa mafanikio makubwa mpango wa Elimumsingi bila malipo. Mpango huo una lengo la kuhakikisha kila mtoto wa Tanzania mwenye umri wa kwenda shule anapata haki ya kupata elimumsingi bila kikwazo cha ada na michango mingine.

Katika kipindi cha miaka mitatu, Serikali imetumia shilingi bilioni 711.22 kutekeleza mpango huu. Katika mwaka 2018/2019, Serikali tayari imetoa shilingi bilioni 166.44 hadi Februari, 2019, kwa ajili ya kutekeleza mpango wa Elimumsingi bila malipo hapa nchini. Utekelezaji wa mpango huo, umeongeza idadi ya wanafunzi walioandikishwa katika shule za msingi na sekondari”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena kusema, naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kubuni jambo hili ambalo ni muhimu na lenye tija kubwa sana kwa nchi yetu kwa ajili ya kizazi chetu cha leo na kijacho. Naipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kuwa kila jambo jema kubwa la namna hii linapokuwa linaanzwa kwa mara ya kwanza huwa halikosi changamoto mbalimbli na kwa kuwa mimi kama Mbunge kazi yangu ni kuishauri Serikali, napenda nishauri machache kwenye elimu bila malipo. Kwanza kabisa, kwa kanuni iliyowekwa kwamba pesa inayopelekwa shuleni inaenda kulingana na idadi ya wanafunzi katika shule husika. Kwa mfano, Shule ya Msingi Bunge ina watoto 150, nitolee mfano tu, kwa kuwa TAMISEMI inatoa Sh.10,000 kwa kila mtoto na katika Sh.10,000 hiyo, Sh.4,000 inabaki TAMISEMI kwa ajili ya kununua vitabu, Sh.6,000 ndiyo inaenda kule shuleni, sasa Sh.6,000x150 kwa mwezi nadhani inakimbilia kwenye Sh.75,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukipiga mahesabu ya matumizi kwa ile shule husika bado kuna changamoto kidogo kwamba inakuwa haitoshelezi. Kila shule kwa ajili ya usalama wa vifaa vilivyoko pale ni lazima kuwa na mlinzi. Mlinzi kwa vyovyote hawezi kulipwa chini ya laki moja, itakuwa ni laki moja na point. Shule yoyote ni muhimu na ni lazima kama ikibidi iwe na umeme, kama haina umeme basi lakini iwe na maji maana ni muhimu sana. Kwa hiyo, bili za umeme, bili za maji zitatoka kwenye hiyo hiyo Sh.75,000 kitu ambacho unaona kabisa bado kinakuwa ni kigumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mkuu wa shule huyu Mwalimu Mkuu kila mwezi anatakiwa aende hata mara mbili au ikibidi hata mara tatu kuhudhuria vikao na Afisa Elimu labda ameitwa au ameitwa na Mkurugenzi kwenye Halmashauri, atategemea ile ile Sh.75,000 ndiyo imsaidie yeye kwenda mpaka kule na wakati mwingine ni mbali inabidi alale, hakuna posho ambayo anaipata ya kwenda kulala au usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo, kuna hii michezo ya UMITASHUMTA ambapo anatakiwa huyu Mwalimu Mkuu achekeche akili yake ahakikishe kwamba watoto wanashiriki michezo kuanzia kata, wilaya, mkoa na mpaka taifa. Kwa taarifa nilizonazo ni kwamba mwaka huu Mtwara ndiyo michezo inafanyika kitaifa. Katika hiyo Sh.75,000 yake, atafanya muujiza gani ili watoto hawa waweze kushiriki vizuri michezo kwenye kata, waende kwenye wilaya, washiriki kwenye mkoa, anunue jezi na mipira, kwa kweli kiuhalisia inakuwa bado ni changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado huyu huyu Mwalimu Mkuu anatakiwa adurufu internal exams, test, wakati mwingine hata ku-print repoti kwa ajili ya watoto hawa wapeleke kwa wazazi wao, zote zinahitaji pesa ambayo inatoka kwenye ile Sh.75,000. Maelekezo yaliyotoka TAMISEMI pia yanaeleza kwamba pesa hiyo hiyo kama kuna marekebisho madogo madogo Mwalimu Mkuu aitumie hiyo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali ijaribu kufanya upya calculation ili tupate ile initial cost ambayo itasaidia kujua pamoja na kwamba tunaenda na uwiano wa shule, pesa inatolewa kwa ajili ya watoto 100, kuna shule nyingine zina watoto 1,000 tunatoa hiyo lakini lazima tuangalie vitu ambavyo ni vya muhimu. Kwa mfano, issue ya mlinzi, Mkuu wa Shule asiwe na hiyo headache kwamba nitatoa wapi hela ya kumlipa mlinzi mwisho wa mwezi umefika. Ikija bili za maji, umeme, kuna mpishi wa uji, Mwalimu Mkuu anaumia kichwa, kidogo inasumbua na kwa kweli inakuwa ni burden kwenye hizi shule ambazo tumelenga kuzisaidia. Kama tunataka elimu bora na tumeanzisha mpango huu mzuri kabisa wa Elimu bila malipo, basi tupeleke na haya marekebisho madogo madogo viende kwa pamoja ili tuweze kulifikia lengo la kutoa elimu bora, siyo tu elimu bila malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, napenda kuishauri Serikali yangu kupitia upya kuangalia kupandishwa kwa madaraja ya walimu. Ni muda kidogo walimu hawajapandishwa madaraja na increments za mishahara na yenyewe inaweza ikapunguza kidogo morale ya kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa lengo letu ni jema, tunataka watoto wetu wapate elimu iliyo bora, basi tujaribu kuangalia makandokando haya ambayo yanaweza yakakwamisha kutupeleka kwenye ile elimu bora tunayoitaka, tuhakikishe tunarekebisha hizi changamoto ambazo nimezizungumzia. Nina imani kubwa na Serikali ya Awamu ya Tano kwamba ushauri huu nilioutoa utafanyiwa kazi kwa sababu naamini pesa ipo, tutajaribu kurekebisha hayo ili tuweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, mchango wangu ulikuwa ni mdogo, naomba muuzingatie. (Makofi)