Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kuona siku hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa iliyofanya nchi nzima ikiwemo Jimbo la Mbulu Mji. Niseme tu kwa ujumla kazi zilizofanywa na Serikali hii ya Awamu ya Tano zipo katika ngazi mbalimbali na kwa nyakati tofauti. Watanzania wa leo wana masikio na macho na wanaona matokeo ambayo yanagusa zaidi maeneo ambayo pengine kwao yalikuwa tatizo kwa namna mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya ambayo ni muhimu sana lakini Serikali kwa jitihada mbalimbali imechukua hatua za makusudi kuboresha huduma ya afya kutoka kwenye miundombinu na huduma mbalimbali ikiwemo dawa na vifaa tiba lakini pia katika kila sekta kwa kazi hizi zimefanyika. Kwa namna ya pekee sana, tunampongeza Mheshimiwa Rais na Serikali yake lakini pia Baraza la Mawaziri kwa kuwa kila sekta imejaribu kufanya kazi. Nayazungumza haya kwa sababu yamefanyika katika Jimbo langu la Mbulu Mji na nchi nzima kwa ujumla kadri tulivyoona kwenye Kamati mbalimbali kwa kukagua miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwa uchache na umuhimu sana kuzungumzia eneo la ajira. Hali ni mbaya sana, tunaomba Serikali ifanye utafiti na ichukue hatua za makusudi kuona ni kwa namna gani vijana wote waliomaliza elimu yao katika vyuo mbalimbali wanaweza kutoa mchango wao kwa Taifa letu. Kadri nafsi za ajira zinavyokuwa chache basi sekta hii ambayo tunaiita ni sekta binafsi ina nafasi kubwa ya kuchukua vijana wetu ambao wamehitimu. Tatizo tulilonalo ni kwamba vijana wengi wanakosa nafasi ya kufikiri kwamba sekta binafsi inaweza kuwa na mchango mkubwa katika kuwapatia Watanzania ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili ili kwa namna mbalimbali tutazame sheria za ajira na upungufu uliopo kwenye sekta binafsi katika suala la ajira kwa vijana. Vijana wengi wanaogopa kuajiriwa na sekta binafsi kutokana na mtazamo wao uliojijenga kwamba Serikali itawaajiri, kwa hiyo, sekta binafsi inaogopwa. Kwa hivyo, ni jukumu la Serikali kutazama upya suala la ajira pamoja na mazingira ya kustaafu kwani ndiyo yanaifanya jamii na vijana kuona kwamba wakiajiriwa katika sekta binafsi hawatakuwa sawa na wale walioajiriwa katika sekta za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nayasema haya? Kila mtu hapa tulipo anaogopa kustaafu, hata Wabunge tunaogopa kustaafu kwa sababu mazingira ya kustaafu baadaye siyo mazuri, kila mtu ana hofu hatma yangu itakuwaje baadaye nikishastaafu. Kwa hiyo, kuna haja ya kuangalia sheria na taratibu za ajira na mafao ya kustaafu katika sekta binafsi kwa sababu akiangalia kama baadaye akistaafu hali yake siyo nzuri, basi lazima kijana aanze kupata hofu na waweze kuogopa kuajiriwa katika sekta binafsi. Pengine haya yanatokana na mishahara midogo lakini pia mazingira ya kufanyia kazi yanakuwa siyo rafiki sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima Serikali itazame pia shule zetu za sekondari na msingi ni namna gani tunabadilisha na kuingiza mitaala ya sekta za biashara, ajira na mafao baada ya kustaafu ili vijana wetu wasisome kwa dhamira au kwa nia ya kwamba hapo baadaye wataajiriwa na Serikali. Katika shule zetu za msingi lazima tuwe na mitaala ya kilimo na biashara na kufanya mambo haya kuwa rafiki kwa kijana wa Kitanzania. Sasa hivi vijana wana chuki kwetu sisi Wabunge wanaona kwamba hatuzungumzii suala zima la upungufu wa ajira katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya umma na sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia uanzishwaji wa viwanda, tusipotafuta utaratibu na mazingira yanayoruhusu vijana waende kwenye ile hali ya kwenda kwenye viwanda, tutakujakuta tumeanzisha viwanda lakini vijana wetu hatukuwaandaa katika ile mitaala ya ajira kwenye sekta ya viwanda. Hii ni kwa sababu utakuta vijana wengi hawana mwamko wa kwenda vyuo vya ufundi, vyuo vya kati na vyuo vya ujuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapopata ajira kwenye viwanda au tunapoanzisha kiwanda tutajikuta kwamba vijana hawana uwezo na taaluma ya kuweza kujiingiza kwenye zile sekta za viwanda. Nadhani tutumie vizuri nafasi za Maafisa Vijana katika Halmashauri zetu na kuwe na forum za majadiliano katika ngazi ya wilaya na baadaye mkoa. Serikali ione utaratibu ambao utawezesha vijana kujadili masuala yao mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapungufu haya yanaweza kufanyiwa kazi na kuleta tija kwa sababu hata sasa sekta ya michezo hatujaitumia vizuri ikaonesha mchango wake katika ajira kwa Taifa letu. Nasema hivi kwa sababu kama ambavyo vijana wanafanya mazoezi ya mashindano ya shule za msingi na sekondari na mwisho mkoa, hakuna utaratibu wa kuwashika mkono kwa vile vipaji vyao vinapoibuliwa na kufika kwenye ngazi ya mkoa. Kwa sababu hiyo basi, tunayo sababu ya kuendeleza fursa zote zinazowagusa vijana ili waweze kujiendesha na kutambuliwa kupitia vile vipaji walivyozaliwa navyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunawaambia vijana waanzishe shughuli binafsi au wajiari, mazingira si rafiki sana kwa sababu kwanza hawana mitaji lakini hata akisema anaanzisha biashara uwezo wa kusimamia biashara hana kwa sababu yeye mwenyewe alitarajia aajiriwe Serikalini ama kwenye sekta fulani wakati anasoma, hakuwa amejiandaa kwa kujiajiri. Kujiajiri ni nafasi pana au namna ya kijana kujiajiri kunahitaji maandalizi toka mwanzo, amefanya mazoezi kama nchi nyingine huko duniani zinavyofanya kwamba anapokuwa na sura fulani basi anakuwa na nafasi ambayo ameifanyia mazoezi na mwisho wa siku akijiajiri ni nature aliyokuwa nayo toka mwanzo na hiyo inampeleka kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili pia naomba kuishauri Serikali, kuna taarifa isiyo rasmi inatembea ambayo inasema kauli ile ya Rais ya kubadilisha Kikokotoo siyo waraka wa Serikali. Kama kuna hiyo kauli na kuna watu wanaitumia hiyo loophole tunawaomba watambue kauli ya mwenye nchi ni sheria, ni waraka huwa inatakiwa izingatiwe. Wastaafu wengi wanalalamikia jambo hili kwa maana ya kwamba bado hawajabadilishiwa, kwenye Jimbo langu kuna baadhi wamenipigia simu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Zacharia.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)