Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nami fursa ya kuchangia katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza kabisa naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Ofisi yake kwa utendaji mahiri wa kusimamia Serikali. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa namna anavyoiongoza nchi yetu na anavyopambana na rushwa lakini vilevile kufuatilia kwenye miradi ya maendeleo kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu nitazungumzia mambo machache kama matatu, manne hivi. La kwanza kabisa ni suala la kilimo, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ameelezea sana suala la kilimo na vilevile ameelezea suala la Mpango wa Kuendeleza Sekta ya Kilimo - ASDP II ambao pia umekuwa na vipaumbele vingi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba vipaumbele vyote hivyo vitaweza kuwaondolea wananchi umaskini, kuongeza tija, lakini vile vile kuongeza ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika moja ya mpango mkakati ambalo nataka niongelee mimi ni suala la mafuta ya kula. Katika mpango wa ASDP II umewekwa mpango mkakati wa kuongeza zao la mchikichi hapa nchini ili kukabiliana na tatizo la mafuta ya kula na sisi wote ni mashahidi hata bajeti iliyopita nchi yetu inatumia zaidi ya bilioni mia nne kumi na sita kuagiza mafuta ya kula nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja, zao hili la mchikichi kama ulivyoona katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu linafanyiwa kazi katika mpango ambao umewekwa katika mpango wa miaka mine. Hata hivyo, tunayo mazao mengine ambayo yenyewe yanaweza yakatoa matokeo ya haraka. Moja ya zao ambayo yanaweza matokeo ya haraka ni zao letu la alizeti ambalo linalimwa kwenye mikoa mingi hususani mkoa wetu wa Singida. Kwa bahati mbaya sana sioni mkakati wowote wa kuweza kuhakikisha kwamba zao hili la alizeti, linawekewa mkakati wa kuhakikisha kwamba tunakamua na kupata mafuta ya kutosheleza. Pengine hatuhitaji hata kuwa na bajeti ya ziada tunachohitaji ni kupunguza bajeti ya kununua mafuta kutoka nje ya nchi na kuhakikisha kwamba tunakamua alizeti tuliyonayo nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza wakulima wetu wanateseka sana kwa soko la alizeti yakiwemo na mazao mengine, sisi kwa Singida tuna zao la vitunguu kwa mfano, hali ni mbaya sana. Pamoja na mkakati mkubwa wa Serikali wa kujenga viwanda na kwa Mkoa wetu wa Singida kwa taarifa zilizopo tumevuka hata lengo la kuwa na viwanda mia moja, ni zaidi ya viwanda mia mbili, lakini bado tunalo tatizo la soko la vitunguu na soko kubwa sana la alizeti. Mpaka sasa wananchi wanahangaika kuuza alizeti yao, wanahangaika kukamua kidogo kidogo na kuweka kwenye madumu, kusimama barabarani na kupoteza muda mwingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niiombe sana Serikali, ili tuweze kupata matokeo ya haraka katika kuendelea kupoteza fedha nyingi za kigeni kuagiza mafuta, ni vyema Mheshimiwa Waziri Mkuu atakapokuja, tuone mkakati, mahususi kwa ajili ya hili zao la alizeti ili kusudi tuweze kuwasaidia wananchi hawa, kwa sababu hili ni zao ambalo ndani ya mwaka mmoja alihitaji kusubiri kama ulivyo mchikichi. Kwa hiyo, wakati tutakapokuwa tunaendelea kusubiri zao la mchikichi ni vema tukajikita kwenye zao la alizeti na mazao mengine ambayo yanaweza kutoa mafuta na matokeo ya haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika sekta ya maji, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, sekta ya maji hasa vijijini imekuwa kutoka asilimia 58.7 na kufikia asilimia 64.8. Kasi hii naiona bado ni ndogo na wananchi wengi bado hawajapata maji. Kwa mkoa wetu wa Singida sisi tumefikia asilimia 49 peke yake kwa upande wa vijijini. Hali hii ni mbaya sana, sasa niiombe Serikali tumebakiwa na mwaka mmoja wa utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo inatutaka tufikie asilimia 85 kwa vijijini na asilimia 95 kwa mijini, tuiombe sana Wizara ya Maji ambayo sasa hivi imechukua jukumu badala ya Halmashauri, watoe vibali kwa ajili ya miradi ya maji iliyopangwa kwa mwaka wa fedha 2018/2019, ili miradi hiyo itangazwe. Hatutaweza kufikia malengo kama Bunge limetenga fedha, halafu Wizara bado haijaweza kutoa vibali na miradi mingi ya mwaka huu wa fedha unaoendelea haijaweza kutolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la uwezeshaji, nilikuwa najaribu kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, wamefanya kazi, lakini kwa kweli bado kuna changamoto nyingi. Ukiangalia kwenye takwimu ambazo zipo katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ukienda kwenye ukurasa kwa mfano wa 28 kupitia TADB zimetolewa shilingi bilioni 107 ambazo zimewanufaisha wananchi kama milioni moja hivi. Ukijaribu kuangalia maana yake ni kwamba ni sawasawa na mwananchi moja kwa wastani amepata shilingi laki moja na mia saba. Ukienda ukurasa wa 34 kupitia SIDO zimetolewa shilingi bilioni 1.74 ambazo zimenufaisha vikundi au wananchi elfu moja na kumi na tatu kwa wastani wa shilingi milioni moja na laki saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukienda kwenye ukurasa wa 66 kwenye upande wa mafunzo hasa kwa vijana ambao ndiyo tatizo kubwa la nchi yetu, tunasema vijana hapa ni asilimia sitini, lakini vijana ambao tumewapa mafunzo nchi nzima ni vijana elfu thelathini na mbili mia tano na sitini na tatu, hapa tunahitaji kuongeza juhudi. Naomba sana Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye inashughulika na masuala ya vijana, tunaendelea kwa kweli kukuza tatizo hili kama tukienda kwa kasi ya kushughulika na vijana elfu thelathini na mbili peke yake ambayo haifikii hata asilimia 0.1. Kwa hiyo, niombe sana, suala hili lirekebishwe na kuhakikisha vijana hawa wanasaidiwa mitaji, wananchi wetu wanaweza wakakopeshwa kwa wingi, siyo kwa kiwango hiki cha nchi nzima, viwango hivi vingeweza kufaa kuzungumza kama viwango vya mkoa na si viwango vya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la mwisho nisemehe kwa upande wa umeme. Naipongeza sana Serikali kwa juhudi kubwa, Serikali ya Awamu ya Tano ambayo imeanza sana kupeleka umeme vijijini, lakini niombe sana juhudi hizi ziongezwe, kwa sababu kwa mujibu wa takwimu bado tuko asilimia 47 pekee kwa nchi nzima. Niseme tu kwa Jimbo langu la Singida Kaskazini mimi ni vijiji 19 peke yake kati ya vijiji 53 ambavyo viko kwenye mradi. Ukichukua kwenye vijiji vyote 84 maana yake sisi ni asilimia 22.6, kwa hiyo, kama wastani wa nchi ni asilimia 47 sisi bado tupo chiniā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Monko.

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.