Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nichukue nafasi hii kwanza kabisa kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kushughulikia kwa sehemu kubwa sana suala la ushirika kwenye maeneo yetu kwa sababu wakati huo ushirika ulikuwa umekufa kabisa. Mwaka jana wakati anasisitiza mimi binafsi nilikuwa na wasiwasi kama unaweza ukafanya jambo lolote lakini kwa kweli alijitahidi sana na watu walielewa ushirika umefanya jambo zuri kwa mwaka huu ulioisha na naamini mwaka huu tunaouanza utafanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri katika Ofisi ya Waziri ya Mkuu, Mheshimiwa Jenista kwa kutusaidia kwenye Wilaya yangu na kwenye Jimbo langu alitupa pesa tukaanzisha Kiwanda cha Kuchambua Mpunga pamoja na ku-grade. Tumefanikiwa na tumeweza, vijana wanaendelea, wamepata ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru kwa sababu aliweka mbegu kwenye Kiwanda cha Chaki na chenyewe sasa kimeota, kimekuwa kiwanda kikubwa, tumepata mabilioni kutoka Serikalini, mjenzi tayari amekwishaanza kujenga. Kwa hiyo, nawashukuru sana Ofisi ya Waziri Mkuu kwa uwezesho mkubwa ili vijana wetu waweze kupata ajira, kujiongezea kipato na kuendesha maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumze mambo mawili tu. Jambo la kwanza nataka kuzungumza juu ya ajira hizo hizo za vijana. Uchumi wetu kwa sehemu kubwa unaendeshwa na sekta isiyo rasmi. Sekta isiyo rasmi ina utawala uchumi wetu kwa asilimia kama 60 hivi. Katika sekta hii isiyo rasmi sehemu kubwa wanaofanya kazi huko ni vijana maana nguvu kazi ya vijana kwenye Taifa hili ni kama asilimia 56 na asilimia 70 wako kwenye sekta isiyo rasmi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii inapoendelea kuwa kubwa namna hii siyo afya sana kwa uchumi wetu kwa sababu wataalam wa mambo ya uchumi wanasema sekta isiyo rasmi kama ni kubwa tuhesabu kwamba nchi hiyo itaendelea kuwa katika hali ya umaskini kwa sababu sekta isiyo rasmi haina mchango mkubwa unaoweza kueleweka kwa Serikali na hata kwa uchumi wa nchi hiyo. Kwa hiyo, sekta hii isiyo rasmi lazima tuendelee kufanya juhudi kuipunguza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ili kurasimisha biashara za baadhi ya watu lakini pia kujenga ujuzi kwa vijana ili waweze kujiajiri watoke kwenye sekta hii isiyo rasmi wawe rasmi zaidi. Pia nashukuru pia kwa mpango wa Serikali ambao sasa umekwishaanza wa kugawa vitambulisho vya Sh.20,000 ili wafanyabiashara na wajasiriamali wadogo wadogo waweze kusajiliwa lakini hii ni hatua ya kwanza tu ili waweze kwenda hatua ya pili ambayo sasa itawafanya wajulikane na waweze kutoa mchango mkubwa kwenye uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sekta hii isiyo rasmi, sasa wanaingia vijana ambao wamemaliza vyuo vikuu na vyuo mbalimbali kwa sababu ya kukosa nafasi za ajira maeneo mengine. Sekta hii inapoingiliwa na watu waliosoma namna hii, lazima sasa kama Taifa tuanze kuangalia ni kwa namna gani tunafanya kwa kasi kuipunguza sekta hii ili iwe rasmi watu hawa ambao Taifa limewasomesha waweze kuchangia sawasawa kwenye uchumi wa nchi yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, vinginevyo tukiendelea kuiacha ikaendelea kuwa kubwa kwa wimbi kubwa la wasomi wanaoingia kwenye sekta hii, kwanza wakiingia huko kwa sababu mambo yake mengi hayajaeleweka vizuri watachanganyikiwa na kwa hiyo itakuwa ni chanzo cha vurugu au cha kukosesha amani nchi yetu kwa sababu wao wana-higher expectation. Tunaposoma chuoni tunaamini kwamba ukitoka hapo basi utakuwa umeukata sasa wakikutana na sekta isiyo rasmi ambayo haijaeleweka vizuri inaweza ikawapunguzia amani zaidi na hivyo kuwaongezea msongo wa mawazo na hatimaye kupelekea kutupeleka kwenye mahali ambapo hatutaki kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka kushauri pia vijana wetu wengi wanaomaliza vyuo vikuu hata kama ajira zipo wanashindwa kuajiriwa kwa sababu ya kukosa uzoefu. Suala hili limekuwa tatizo kubwa kweli. Nashauri Serikali kwa nini isije na mpango wa kujengea uwezo vijana wetu wanaomaliza vyuo wote wapate uzoefu wa mambo waliyoyasomea huko chuoni kupitia programu ambayo itakuwa ni ya kujenga uzoefu ya kiserikali. Siyo hii ambayo mtu anakuwa chuoni anaenda practical sijui miezi miwili, mitatu, no, akimaliza chuo kikuu aende Internship Programme ya muda wa mwaka mmoja au miwili ajenge uzoefu, aweze kuajiriwa nafasi za ajira zinapotokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakutana na watu mbalimbali, mashirika mbalimbali ya kimataifa na taasisi zingine zisizo za kiserikali zinasema tunashindwa kuwaajiri vijana wanaotoka chuoni kwa sababu kwanza uzoefu hana lakini pia ujuzi wa kazi ile ambayo wangeweza kumpa hana, sasa atapataje uzoefu na ujuzi huo? Serikali ikija na mpango wa kila mwanafunzi anapomaliza chuo aende kwa Afisa Utumishi wa Wilaya, Idara au wa chombo chochote cha Serikali akae hapo, gharama zinaweza kuwa za mzazi au mlezi ili ajengewe uwezo awe na uzoefu na ujuzi wa lutosha ili aweze kuajirika nafasi za ajira zinapopatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tukiendelea na utaratibu tulio nao sasa mtu amalize chuo kikuu, ana matarajio makubwa, anafikiri atapata kazi, akienda kwenye interview anaonekana hana uzoefu, anarudishwa aende nyumbani akafanye nini? Kwa hiyo, nashauri Serikali kwamba ni muhimu sasa ije na Internship Programme ambayo itawawezesha vijana hawa wapate uzoefu na ujuzi wa mambo waliyoyasomea na hasa kazini ili waweze kuajirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nataka nizungumze na pengine litakuwa jambo la mwisho, ni suala la viwanda. Ni hivi, wawekezaji wa nje tunawahitaji sana lakini pia wawekezaji wa ndani nao tunawahitaji sana. Nadhani hawa wa ndani tunawahitaji zaidi kwa sababu wao pia wanatuona sisi kama Watanzania wenzao. Najua wawekezaji wa nje ni wazuri lakini wanatuona sisi kama soko lakini pia kama chanzo cha malighafi ili kutengeneza semi-processed commodity waweze kwenda kumalizia kwenye viwanda vyao kule nyumbani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumze tu juu ya viwanda vya nguo. Ni kweli tuna kauli mbiu inayosema ‘pamba hadi nguo’ lakini ni kauli mbiu tu inaungwa mkono na Sera ipi ya Viwanda vya Nguo? Hatuna Sera ya Viwanda vya Nguo! Naelewa tuna Sera ya Viwanda lakini Sera mahsusi kwa ajili ya Viwanda vya Nguo haipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, amesema Mheshimiwa mama Kilango jana hapa, nchi hii ina uwezo mkubwa wa kuzalisha pamba nyingi na hivyo kwa pamba hii tungeweza kuajiri watu wengi zaidi kama tungeangalia kwa ndani kwanza badala ya kuangalia soko la nje. Habari ya pamba ingeweza kujenga uchumi wetu vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa mama Malecela jana ametuambia Bangladesh ambayo ilikuwa nchi maskini sana hailimi pamba lakini imeajiri watu wake asilimia 85 kupitia pamba ambayo inazalishwa sehemu nyingine. Sasa sisi ni zaidi maana tuna watu milioni sita ambao wameajiriwa kwa kulima pamba kwenye nchi hii ambapo pamba yao inaweza ikatengeneza ajira zingine milioni tatu na kitu au mpaka nne. Kwa hiyo, pamba inaweza ikaajiri watu milioni kumi katika nchi hii ikiwa tutafanya juhudi za makusudi kuwaunga mkono wale waliowekeza kwenye viwanda vya pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini tusiwe na mpango kama ule tulionao kwenye sukari? Mbona viwanda vya sukari vimeweza kutu-sustain. Viwanda vya sukari vinazalisha sukari kwa nchi hii, hatuzalishi sukari kwa kuuza nje lakini tunazalisha sukari kwa ajili yetu Watanzania na tumevilinda kwa namna mbalimbali kwa kuzuia sukari isiingie hapa. Viwanda vya pamba hatujavilinda kwa namna hiyo, tumeacha soko huria hata kwa vitu ambavyo vinaweza vikatengenezwa hapa kwa kutumia pamba yetu na viwanda hivyo vikatengeneza ajira kwa ajili ya watu wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana tutafute ni kwa namna gani tunaweza kuongeza uzalishaji wa pamba lakini kuongeza viwanda vinavyochambua na kutengeneza nguo zinazotokana na pamba kutoka kwenye pamba yetu badala ya kuangalia tu kuuza pamba iliyo ghafi kwenda nje. After all tunapoiuza kule nje kilo moja kwa wenzetu inazalisha mashati matatu sisi hapa mkulima wa kwangu kule Maswa anapata Sh.1,200 tu lakini yule tuliyemuuzia pamba kule nje ananiletea shati, shati moja hapa nitanunua kwa Sh.40,000 mara tatu ni Sh.120,000. Tumetengeneza ajira kwake, tumemuongezea kipato yeye, sisi ambao tumezalisha tumeachwa hatuna kitu. Kwa hiyo, nafikiri Serikali ianze sasa kuwa na mkakati na mazao haya ambayo hasa ni ya Kimkakati tuone ni kwa namna gani tunaweza kuyalinda yakaajiri watu wetu wengi baadaye yakatupa kipato cha kutosha kwenye nchi yetu na watu wetu wakapata ajira wakafurahia matunda ya uhuru wa nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niseme hayo mambo mawili tu kwa leo, nitazungumza mambo mengine nitakapopata nafasi nyingine hasa kuhusiana na viwanda vya nguo hapa nchini. Viwanda vya nguo vya hapa nchini kwa kweli hatujavitendea haki kwa sababu hatuvilindi, vinajipigania vyenyewe lakini ukijaribu kuangalia waliowekeza ni wazawa, ni Watanzania ambao wanaajiri Watanzania, wanatupatia kipato na tunapata namna ya kuendesha maisha yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)