Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami jioni ya leo niweze kuchangia hotuba iliyo mbele yetu. Awali ya yote niseme namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai wa kuweza kusimama jioni hii na kutoa mchango wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kuchelea nataka nitoe vilevile pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wateule wote kwa kazi nzuri inayofanywa na vilevile niwaombee dua kwa Mwenyezi Mungu awape umri mrefu ili waweze kuitumikia nchi yetu twende kule ambako Tanzania inataka kwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze na kwa nini watu kila wakisimama hapa wanamsifia sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kweli kama kuna mtu anachelea kumsifia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anafanya dhambi. Yapo mambo ambayo Mheshimiwa huyu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yanafanywa katika nchi hii hayakutegemewa kwa miaka mingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata mimi nilivyokuwa upande wa pili alivyokuwa anaanzisha hii miradi mikubwa nilikuwa na wasiwasi hizi fedha zitapatikana wapi lakini kitu cha ajabu kilichotokea sasa hivi, tuna miradi mikubwa mingi inayofanywa na inafanywa kwa pesa zetu. Kama miradi hii ingeweza kutekelezwa kwenye awamu zilizopita leo Tanzania tusingekuwa hapa tulipo. Sasa kwa nini huyu mtu ambaye ana maono ya namna hii tusimpe sifa, tusimtie moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna miradi, kwa mfano kuna kuna huo mradi wa Stiegler’s Gorge, kuna ununuzi wa ndege, kuna ujenzi wa reli (SGR), kuna ujenzi wa viwanja vya ndege, tunajenga hospitali wilayani, tunajenga vituo vya afya kwenye kata zetu. Nani ambaye anaweza akasimama kwenye Bunge hili ambaye kwenye wilaya yake hakuna kituo cha afya kinachojengwa? Kwa spidi hii ya ujenzi wa vituo vya afya kama huko miaka ya nyuma tungekuwa tunajenga namna hii, kwa spidi hii leo hii kuna kata ambayo ingebaki haina kituo cha afya?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunapokwenda namna hii, tunajenga flyover, Dar es Salaam sasa hivi kunakwenda kujengwa flyovers zaidi ya tatu. Jamani, kwa nini tuache kusifia? Ni lazima tutasifia, ni lazima tutam-support na lazima tutamwombea dua Mwenyezi Mungu ampe umri mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhana ya Mheshimiwa Rais kutokutoka nje ya nchi hii sasa tunakwenda kuona faida yake. Kwa nini Mheshimiwa Rais alikuwa amesema kwamba hataki kusafiri nchi za nje; yuko tayari kulinda rasilimali za nchi hii ili ziweze kuwanufaisha watu wote na ulinzi wa rasilimali za nchi hii tumeuona kwa sababu katika hali ya kawaida watu walikuwa wanasema kwamba Mheshimiwa Rais hasafiri, tutapataje misaada? Yuko ndani na tunafanya mambo yetu, big up sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nichangie kwenye uwekezaji; kwenye uwekezaji nchi yetu inafanya vizuri, ni kwa sababu kubwa mbili. Kwanza ni kwa ajili ya amani yetu tuliyonayo na usalama, wawekezaji wanahakikishiwa usalama, kwa sababu wanakuwa salama na amani, mali zao zitakuwa salama. Hata hivyo, tunapwaya upande mmoja kwenye uwekezaji, Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji naomba anisikilize hapo; bado tuna tatizo la njoo kesho, njoo keshokutwa, hapa ndipo tunapokwama. Leo hii mwekezaji, nitoe mfano mmoja, jana nimemsikia Mheshimiwa Rais akiwa Mtwara, kuna mwekezaji mmoja pale amewekeza kiwanda, transfoma za umeme kanunua mwenyewe, amekwenda Idara ya Maji wanamwambia atoe milioni 100 wamletee maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa msingi huu hata kama tuna sifa nzuri kwamba bwana Tanzania ukiwekeza mali zako zitakuwa salama, ni nchi yenye utulivu, lakini bado akija ndani hapa anakutana na vikwazo vya njoo kesho, njoo keshokutwa, hili Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana naomba aliangalie kwa makini sana, bado kuna watu kwenye ofisi yake wana tabia ya njoo kesho, njoo keshokutwa. Inawezekana haohao ndio wapinzani wa Mheshimiwa Rais, kwa sababu haiwezekani mpaka leo hii kuna mteule wa Rais hajui mwelekeo wa nchi inapokwenda, hajui Mheshimiwa Rais anataka nini. Wapo watu wanashindwa kufanya maamuzi, wanashindwa kujua kwamba wamewekwa pale kwa sababu gani; Mheshimiwa Waziri naomba alichukue hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nielekee kwenye kilimo; kwenye kilimo kuna matatizo makubwa mawili, kwanza upatikanaji wa pembejeo kwa wakati na masoko. Suala la pembejeo kwangu mimi linachukua nafasi ya pili ukilinganisha na suala la masoko. Tunalo tatizo kubwa sana la wakulima wetu wanahangaika na masoko na ndiyo maana sasa hivi wakulima wanabadilisha mazao kila mwaka. Mwaka juzi korosho Kusini zimefanya vizuri, watu wameacha kulima mpunga, wameacha kulima mazao mengine wamekwenda Kusini kulima korosho, mwaka huu korosho zimeyumba bado wakulima wetu wanahangaika. Kwa hiyo, naomba kwenye upande wa kilimo tujikite sana kwenye kutafuta masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kwenye upande wa maliasili; upande huu naiomba sana Serikali ije na marekebisho ya Sheria ya Kifuta Machozi. Sisi tunaopakana na hifadhi tunapata shida sana mazao yetu kuliwa na wanyama, lakini hakuna sheria ambayo mkulima yule anapata fidia, kuna Sheria ile ya Kifuta Machozi. Naomba Serikali ije na marekebisho ya sheria, angalau sasa tuanze kufikiria kuwafidia wale ambao mazao yao yataliwa na wanyama wakali.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la umeme, REA; upande wa REA hapa hatujafanya vizuri. Ipo mikoa ambayo imefanya vizuri, ile tu ambayo imepata wakandarasi wanaojielewa, lakini kuna mikoa mingine ambayo imepata wakandarasi wa hovyo, mikoa ile bado REA haijafanya vizuri. Sielewi ni kwa sababu gani, Serikali ilikuwa na vigezo gani mkandarasi mmoja anapewa mikoa zaidi ya mitatu, matokeo yake anafanya mkoa mmoja mingine anasahau. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie upya suala la REA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano katika Wilaya yangu ya Liwale, katika REA awamu ya tatu, Sehemu ya Kwanza ambayo ilikuwa na vijiji 14 mpaka leo kumewashwa vijiji viwili tu na mkandarasi yule amepotea. Tena kibaya zaidi mkandarasi yule anatuchonganisha sisi na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu tangu alipopewa Mkoa wa Lindi, alikwenda Ruangwa akamaliza alipomaliza vijiji vya Ruangwa amekimbia. Sasa sijui kama aliambiwa kwamba Mkoa wa Lindi una wilaya moja, hatujui. Kwa hiyo naomba sana, suala la REA hawa wakandarasi waangaliwe upya, wale wakandarasi ambao wanaonekana kabisa wanaikwamisha Serikali kufikisha malengo yake waondolewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwamba, asilimia kubwa sisi tunazungukwa na hifadhi, lakini vilevile kuna Sheria ya Misitu. Naiomba sana Serikali, hebu twende turekebishe Sheria ya Misitu, asilimia tano kwa uvunaji wa mazao ya misitu inayopata halmashauri ni fedha ndogo sana ambazo hazilingani na jangwa au na uharibifu mkubwa wa misitu unaofanywa kwenye halmashauri zile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya kupanda miti, kwamba baada ya uvunaji wa miti panakuwa na fedha zimetengwa, asilimia mbili, kitu kama hicho kwa ajili ya kupanda miti, mimi kwenye Halmashauri yangu ya Liwale sijawahi kuona kijiji hata kimoja kimepanda miti zaidi ya kukuta kwenye shule tu, ile miti ambayo inapandwa kwenye bustani za shule. Kwa hiyo, naomba kifungu hiki sasa kiondolewe kipelekwe kwenye halmashauri, ile asilimia inayokwenda hamashauri ifike angalau asilimia 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala hili la wazee, leo ni mara ya tatu naliongelea suala hili. Wazee wanatamkwa sana, ukienda kwenye hospitali zetu utakuta kuna labels zimeandikwa pisha wazee, watangulize wazee, lakini bado Serikali haijatuletea sheria ya kuwatambua hawa wazee, hawa wazee tunaokwenda kuwakusudia ni wazee wa aina gani. Ni bora sasa Serikali ikaharakisha mchakato wa kuleta sheria ambayo sasa hawa wazee tunaokwenda kuwatungia sheria wanatambulika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze kwenye suala la elimu maana mimi nadondosha sehemu mojamoja tu. Suala la elimu; suala hili bado hatujafanya vizuri. Tumefanya vizuri kwa kufanikiwa kupeleka watoto wengi shuleni, hili jambo tumefanya vizuri, lakini kwenye ubora wa elimu bado tuna tatizo. Tunacho kitengo chenye kazi ya kukagua, wanaita Kitengo cha Ukaguzi wa Ubora wa Elimu, kile kitengo hakina vitendeakazi, hata magari hawana, mafuta hawana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeweza kufanya ziara, unakwenda kwenye shule unauliza shule hii imekaguliwa kwa mara ya mwisho lini, watakwambia ni miaka miwili, miaka mitatu shule haijakaguliwa. Jambo hili ni jambo ambalo linatakiwa litiliwe maanani, kwamba hiki Kitengo cha Ukaguzi wa Ubora wa Elimu sasa ni wakati kinatakiwa kijengewe uwezo kupewa magari na fedha za mafuta ili kuweza kukagua maeneo yetu haya na hapo ndipo elimu yetu itakapoweza kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio ukaguzi peke yake, bado tumuangalie Mwalimu. Jambo kubwa kwenye elimu, mtu wa kwanza kumwangalia ni Mwalimu; je, Serikali imeshafanya tathmini kwamba madeni ya Walimu yamefikia kiwango gani, mpaka leo hii ni walimu wangapi wanaidai Serikali na mpaka leo hii kiasi gani walimu hawa wanadai? Wengine wanadai likizo, wengine wanadai kupandishwa vyeo, wengine madaraja, bado kuna tatizo kubwa kwa upande wa walimu. Kama tukiamua kucheza na walimu maana yake tunakwenda kucheza na elimu. Mimi jambo hili kwa upande wa elimu naomba sana kwamba litiliwe mkazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, naiomba Serikali ifanye tathmini kuangalia majengo au mahitaji ya wilaya, kata na vijiji vyetu. Kwa sababu Mheshimiwa Rais amesema hana mpango wa kuongeza sehemu za tawala kwa maana kwamba hawezi kuongeza wilaya, mkoa, kata wala tarafa ni mpaka mahitaji kwenye maeneo hayo yamekamilika. Je, Serikali imeshafanya utafiti?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Halmashauri au Wilaya yangu ya Liwale haina jengo la mahakama, jengo la polisi, Hospitali ya Wilaya wala nyumba ya Mkuu wa Wilaya na ina miaka 43. Kwa hiyo, ni lazima Serikali ije na mpango na takwimu ijue kuna wilaya ngapi zimekosa majengo ambayo yanaitambulisha wilaya, mikoa au kata zetu. Haiwezekani unakwenda kwenye kata hukuti jengo linaloitambulisha kata, hakuna zahanati, kituo cha afya, kituo cha polisi au mahakama ya mwanzo, sasa unasemaje pale ni kata? Ni vitu gani vinavyokwenda kutambulisha maeneo haya? Kwa jambo hili naiomba Serikali iwe makini sana na ije na takwimu sahihi kuhakikisha kwamba haya yote tunakwenda kuyasimamia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na napenda kuunga mkono hoja kwa asilimia mia kwa mia. (Makofi)