Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Awali ya yote niseme naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napende kusema kwamba, naipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri inayofanya. Katika Jimbo la Njombe tumepata maendeleo ambayo toka dunia kuumbwa haijawahi kutokea. Nitoe mfano mmoja tu, tumepelekewa maendeleo na Serikali ya Chama cha Mapinduzi katika Kata ya Utalingolo katika Kijiji kijulikanacho kwa jina la Ihalula, mpaka leo nilipokuwa nafuatilia, maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni mbili, haijawahi kutokea. Naipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumejengewa zahanati mahali pale ya shilingi milioni 500, tumepelekewa vifaa vya hospitali vya zaidi ya shilingi milioni 300, lakini tumepelekewa umeme kwa thamani ya shilingi bilioni moja. Naipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri inayofanya katika nchi yetu, lakini ni pamoja na maendeleo mengine makubwa yanayofanyika ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizi, yako mambo ambayo tungependa sana Serikali yetu ifanye. Ni- declare interest kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC. Tunakushukuru sana umetuwezesha tumefanya ziara nyingi sana katika Kamati yetu. Jambo kubwa nililoliona ni tatizo kubwa la maji katika nchi, lakini ni pamoja na Jimbo la Njombe Mjini, lina tatizo kubwa la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi mingi ya maji katika nchi yetu ukiiangalia imekosewa design. Kikubwa kinachofanyika ni kwamba, ndani ya Halmashauri husika hakuna wataalam wa maji. Halmashauri wanatafuta Mkandarasi au Msanifu wa mradi, anakuja msanifu wa mradi anasanifu mradi, baada ya kusanifu mradi anaikabidhi Halmashauri. Halmashauri inaupokea ule mradi haijui chochote. Ina Mhandisi pale naye hajui chochote. Vinaandikwa vitu ambavyo ikifika wakati wa kutekeleza mradi, mradi hautekelezeki. Hilo ndiyo tatizo kubwa katika Halmashauri zilizo nyingi ikiwemo Halmashauri yangu ya Mji wa Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Mji wa Njombe uko mradi unaitwa Igongwi, ni mradi wa vijiji sita kwa ajili ya maji, lakini mradi ule umesanifiwa na umeanza kutekelezwa na una lots kama tano au sita, lakini lot ya kwanza ni ya uzalishaji maji kwenye chanzo. Kwenye chanzo, kutokana na umbali na milima ilivyo, Msanifu ameweka mabomba ambayo hayawezi kufika kule. Sasa unajiuliza huyu Msanifu alifikaje kule aka-design mabomba mazito kiasi hicho ili yaweze kwenda kule?

Mheshimiwa Spika, nimeenda Halmashauri ya Ilemela, Mwanza, Msanifu amesanifu mradi wa maji wa kijiji uchimbwe mtaro kwenye mlima wa mawe. Matokeo yake imekuwa haiwezekani, Mkandarasi ameshindwa kufanya vile, imebidi ifanyike variation. Kwa hiyo, unajiuliza, hivi tuna Wahandisi wa Maji kweli katika Halmashauri zetu? Tuna wataalam wa maji kwenye nchi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeenda Halmashauri ya Ngara, Msanifu amesanifu tenki la maji lijengwe kwa matofali. Mkandarasi amejenga kwa mawe, tenki linavuja na kuna Mhandisi wa Halmashauri. Tumeenda Halmashauri ya Mheshimiwa Mwijage, mradi wa maji umekamilika hakuna mita inayoonesha kiasi gani cha maji kilichopo kwenye tenki. Unamwuliza Mhandisi wa Halmashauri anasema labda Mkandarasi ali-overlook. Sasa unajiuliza, yeye kama Mhandisi wa Halmashauri alikuwa wapi?

Mheshimiwa Spika, naomba sana Wizara ya Maji ifanye utaratibu mpya wa kupata Wahandisi sahihi wa Maji ili kusudi Wasanifu wanaposanifu miradi ya maji, ile miradi ikifika kwenye Halmashauri, wakiiwasilisha kwenye Halmashauri Mhandisi wa Maji mwenyewe auone ule mradi ni nini kimeandikwa na nini kinatakiwa kufanyika? Vinginevyo tutalalamika matatizo ya maji, fedha itapotea, Wakandarasi watashindwa kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kwenye miradi ya maji, pamoja na upungufu ambao upo, Wizara na yenyewe inachelewa mno kufanya marekebisho. Wakandarasi wanaweza wakaleta taarifa kwamba hapa hili jambo halitekelezeki, lakini unaona kabisa Wizara inachukua muda mrefu sana kufanya marekebisho. Naomba sana Wizara ijitahidi kufanya marekebisho mapema ili miradi ya maji iweze kwenda.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia ni suala la biashara. Katika Halmashauri ya Mji, Njombe sisi sio wafanyabiashara per-se, lakini sisi ni wakulima, lakini mazao yetu ndiyo hayo tunayoyafanya kuwa biashara. Nizungumzie suala la mazao ya misitu hasa mbao, miti, nguzo na majengo.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumza kwamba mazingira ya kufanya biashara Tanzania ni magumu, sisi wakulima wa miti Njombe tunayaona hayo. Tunayaona kwa namna ipi?

Mheshimiwa Spika, sisi zao la miti ni zao la kawaida kama yalivyo mazao mengine kama korosho, wanaolima mpunga, mtama, mbaazi, na kadhalika. Inapokuja kwenye zao la miti kumewekwa sheria na taratibu nyingi sana. Taratibu ya kwanza ambayo inachelewesha maendeleo kwa wananchi hawa, ukitaka kuvuna miti yako, baada ya kuivuna, ili usafirishe mbao kuna kitu kinaitwa TP (Transit Pass). Sasa kama umeshavuna na unataka kusafirisha, ile Transit Pass inapatikana Makao Makuu ya Halmashauri. Kwa hiyo, mwananchi anapaswa kusafiri kilometa kadhaa.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tuchukulie mwananchi anayetoka mwishoni kabisa mwa Jimbo la Njombe Mjini, kwa mfano Kata ya Makoo ambayo iko kilometa 70, lazima aje Njombe Mjini, akate TP ambayo thamani yake haizidi shilingi 3,000/= au shilingi 4,000/=, arudi kijijini akatafute usafiri asafirishe. Hiyo safari peke yake inamgharimu zaidi ya shilingi 20,000/=. Hiyo ya kwanza.

Mheshimiwa Spika, ya pili, mazao haya ya misitu pamoja na kwamba jana Serikali ilizungumza hapa kwamba itaweka utaratibu rasmi, lakini mwananchi yule haruhusiwi kusafirisha ule mzigo kutoka kule kijijini kuleta sokoni baada ya saa 12.00 jioni. Sasa ukiangalia haya ni mazingira ambayo yanachelewesha maendeleo. Wananchi wanashindwa kusafirisha mazao yao ya kawaida kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Njombe, kama Mkoa, idadi yetu tuko 700,000 tu, lakini wenye nafasi ya kuchangia maendeleo, nguvu kazi, siyo zaidi ya 400,000. Sasa ukiangalia watu 400,000 tunachangia maendeleo, tunafanya nchi iweze kupata mbao, ipate nguzo, ipate miti, lakini vilevile tunachangia chakula, tunalima mahindi kwa wingi sana, tunalima viazi kwa wingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana, idara inayohusika na mambo ya misitu iangalie upya jambo hili. Inapokuwa inazuia wananchi wasiweze kufanya biashara eti kwa sababu saa 12.00 imefika, huku ni kuchelewesha maendeleo kwa makusudi. Niombe sana sisi wenye misitu ya kupandwa turuhusiwe kufanya biashara, zao letu la miti liwe kama zao la kawaida kama vile zilivyo mbaazi, pamba, mpunga, na kadhalika ili kusudi speed ya maendeleo iweze kupatikana kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, mnapotuwekea mazingira ya kuweka sijui vibali, utaratibu, kama hiyo TP hatukatai, iwepo, lakini ikatwe kijijini, kwa sababu kule kuna Mtendaji wa Kijiji ambaye ni Mtumishi wa Serikali. Idara ya Misitu ikasimu kwamba akitokea mwananchi ana miti yake anataka kusafirisha, mkatie TP kuliko asafiri kilometa 70 akakate TP arudi kijijini akaanze kusafirisha, inafika saa 12.00 hawezi kuondoka, asubiri siku ya pili yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana Serikali iangalie hilo na ilione kwamba ni jambo linalochelewesha maendeleo wakati mahali kwingine tunakwenda haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuzungumzia jioni ya leo katika kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ni suala la elimu. Elimu yetu inapata shida, inapita wakati mgumu. Tunafanya elimu ipite wakati mgumu kwa sababu ya kutokutaka kubadilika. Kuna vitu tunavisimamia haviko sahihi.

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha Shule za Kata. Shule za Kata leo zimekuwa bora sana na performance inaonekana kwenda kuwa juu sana. Nimekuwa nikishauri hapa na Wajumbe wengine walikuwa wakichangia hapa kwamba, katika Shule zetu hizo za Kata, tuanzishe michepuo ya ufundi. Jambo hili limekuwa gumu sana. Yaani limekuwa gumu. Kila mtu akisimama hapa anasema VETA, Serikali yenyewe ikisimama inasema VETA; lakini hizo VETA ukiangalia jinsi zilivyo, zitaweza kuchukua watoto wote hawa wanaohitimu Kidato cha Nne? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna ugumu wa kubadilisha shule angalau moja kila Halmashauri kuwa Shule ya Ufundi. Naomba sasa Serikali ilione hilo na iweze kusaidia hawa vijana. Vijana hawa wakipata Elimu ya Ufundi tutakuwa tumewasaidia, tutakuwa tumewapa ajira na tumewapa ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nina mashaka nalo sana, miaka ya nyuma wakati tuna Shule za Ufundi kama Ifunda Tech, Moshi Tech, Tanga Tech, Mtwara Tech, Ihungo na nyinginezo, kulikuwa na Chuo kinaitwa Dar es Salaam Technical College, lakini kilikuwa kinatoa Diploma ya Ualimu wa Ufundi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. (Kicheko)

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)