Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja hii. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri anayofanya lakini niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri pamoja na watendaji wote wa Wizara hii, kwa kweli wanafanya kazi nzuri. Kwa hiyo, naiunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na suala la maji, maji ni uhai, maji ni maendeleo, maji ni uchumi wa nchi yetu. Wilaya ya Mpwapwa na Kongwa tuna matatizo makubwa ya maji. Kuna miradi ya maji inayoendelea mpaka sasa lakini bahati mbaya sana imesimama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi niliuliza swali hapa kwamba kwa nini Serikali haiwalipi wakandarasi? Kuna miradi inachukua miaka kumi haijakamilika, kwa nini? Kwa mfano miradi kutoka Kijiji cha Bumila, Iyoma, Mima na Mnzasa, ni zaidi ya miaka kumi haijakamilika. Wakandarasi hawalipwi kwa nini na hapa Bunge tunapitisha bajeti, kama tunapitisha bajeti hiyo hela kwa nini isiwalipe wakandarasi? Kwa hiyo, nashauri wakandarasi wote nchi nzima walipwe ili miradi ya maji iendelee ili wananchi waweze kupata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni ujenzi wa Vituo vya Afya katika Majimbo yetu au katika Wilaya zetu. Hili ni jambo jema, kwa sababu tunawasogezea wananchi huduma katika maeneo yao. Kwa sababu ukishajenga Kituo cha Afya, Wataalam kwa mfano Madaktari watakuwa pale, Manesi watakuwa pale hata hizo minor operations labla, mama ameshindwa kujifungua, kwa hiyo, zile operations ndogo ndogo zinafanyika pale badala ya kuwapeleka Hospitali ambako ni mbali. Kwa hiyo, hili ni jambo jema.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatoa shilingi milioni 500, kujenga hivi vituo, lakini nilikuwa nashauri TAMISEMI mjitahidi basi, mtoe kila Wilaya angalau fedha kidogo za kujenga Zahanati. Tusiishie tu kwenye Vituo vya Afya, hapana. Tunaomba sana, kwa sababu Vituo vya Afya viko mbali na Vijiji vingine havina Zahanati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali kwamba pamoja na na kutoa shilingi milioni 500 kwenye ujenzi wa Vituo vya Afya, kwa mfano kama kwangu pale wamejenga Kituo cha Afya Mima na pale Jimbo la Kibakwe, pamoja na Pwaga. Kongwa vilevile wamejenga Kituo cha Afya pale, wamekarabati maana yalikuwa ni majengo ya zamani kwa hiyo, wamejenga mpya pale maeneo ya Mlali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nashukuru sana, ni mpango mzuri sana. Mjitahidi sasa mwanze mpango wa kutoa fedha kidogo kidogo kwa ajili ya ujenzi wa zahanati. Zahanati ni muhimu sana, hasa maeneo ambayo hayana huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, tunajenga zahanati; wananchi wameambiwa kila Kijiji kiwe na zahanati, lakini tatizo ni kwamba wahudumu hawatoshi kabisa. Lengo la Wizara ya Afya ilikuwa ni ku-train Watabibu Wasaidizi na Tatibu, yaani Clinical Officers na Clinical Assistants, lakini mpango huo umesimama na watumishi bado wanaendelea ni wale wale, ambao tunasema kwamba hawa Medical Auxiliary wanafanya kazi nzuri sana, lakini Medical Auxiliary amekuwa trained kwa ajili labla ya kugawa dawa na mambo mengine. Medical Auxiliary huyo ndiye atibu, huyo ndiye achome sindano, huyo ndiye a-prescribe dawa. Kwa hiyo, inakuwa ni kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba Wizara ya Afya mwendelee na utaratibu ule wa ku-train wale Clinical Officers na Clinical Assistants na kuwasambaza katika zahanati zote nchi nzima. Kwa hiyo, itasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nizungumzie mapato katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Serikali za Mitaa ni Serikali kamili. Katiba Ibara ya (145), (146) inatambua kabisa kwamba tutakuwa na Serikali za Mitaa hapa Tanzania. Kwa hiyo, nilikuwa naishauri Serikali jambo moja, mnapochukua vyanzo vya mapato vya Serikali za Mitaa, basi mshauriane na wale wenye vyanzo vile, itasaidia kuwapa ushauri. Juzi tumepitisha Sheria ya Kukusanya Kodi ya Majengo, ni jambo jema, hatupingi sisi, lakini Kodi ya Majengo TRA wakusanye mwaka mzima, halafu ukiisha mwaka ndiyo Halmashauri zianze kupewa fedha. Hiyo miradi ya Halmashauri itakuwa imesimama! Kwa nini?

Mheshimiwa Spika, maana yake miradi inatolewa taarifa quarterly kila miezi mitatu. Sasa fedha gani ukusanye halafu uziweke mpaka mwaka uishe?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nashauri kwamba angalau wangejitahidi kukusanya miezi sita halafu wazipatie Halmashauri ili ziweze kutekeleza miradi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, sisi Wabunge tuko hapa miezi mitatu kwa ajili ya kupitisha bajeti ya Serikali, lakini jambo la kushangaza, bajeti tunayopitisha na fedha inayofikishwa kwenye Wilaya zetu na Mikoani, kuna fedha mahali pengine hata asilimia 50 haifiki. Ndiyo maana kunakuwa maboma. Kuna miradi mingi sana imelala tu, haijatekelezwa. Maboma ya shule, zahanati, yamelala wala hayatekelezwi kwa sababu fedha hazitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba Bajeti ambayo tunapitisha Bungeni hapa, basi Serikali ijitahidi kufikisha pesa mapema. Kwa mfano, kama Wilaya ya Mpwapwa imetengewa shilingi bilioni kumi, basi ziende shilingi bilioni kumi siyo zipelekwe shilingi bilioni nne, haiwezekani. Shilingi bilioni nne utatekeleza nini? Kwa hiyo, nilikuwa nashauri sana.

Mheshimiwa Spika, la mwisho ni hali ya hewa katika Mkoa wa Dodoma. Wote ni mashahidi mnapita barabara hii…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hasa kule mwisho kule, sitaki kuwataja majina Waheshimiwa mliosimama na nini, mmeanzisha club huko, naomba mkae.

Halafu pili, naomba yaani wewe mwenyewe ukiona sauti imekuwa kubwa, unaanza kwa kushusha ya kwako kidogo. Tuelewane. Pia kuwa ma-back bencher siyo ruhusa ya kuwa ni vituo vya vikao visivyokubalika. Niendelee. Nyie mmenichonganisha eeh! (Kicheko)

Mheshimiwa Lubeleje, endelea. (Kicheko/Makofi)

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, niendelee...

Mheshimiwa Spika, la mwisho nimesema hali ya hewa. Kwa mfano, katika Mkoa wetu wa Dodoma, kwa kweli mwaka huu hatutegemei kama tutavuna chochote. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu kama tutakuja kuomba msaada Viongozi wa Mkoa wa Dodoma, msije mkafikiria kwamba wananchi wetu hawakulima, hawakufanya kazi, hapana. Mvua analeta Mwenyezi Mungu, lakini bahati mbaya mvua zimekatika mwezi wa Pili, mimea yote imekauka. Kwa hiyo, naomba sana, hili suala ni muhimu, lazima tupate chakula cha kutosha katika Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie na kama muda wangu bado kidogo, nimalizie la mwisho… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Lubeleje.

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, niendelee!

SPIKA: Nakushukuru sana, inatosha. Mheshimiwa Magdalena Sakaya.

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono. (Makofi)