Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI MHE. GODBLESS JONATHAN LEMA (MB)

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI MHE. GODBLESS JONATHAN LEMA (MB)

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye azimio hili la Kamati ya Maadili ya Bunge.

(Hapa baadhi ya Wabunge wa Kambi Rasmi ya Upinzani walitoka Ukumbini)

SPIKA: Mbona mmeanza kukimbia tena? Mmeshaingia baridi?

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nikupongeze kwa jinsi unavyoliongoza Bunge letu, unatuongoza vizuri kama Wabunge.…

SPIKA: Hapana, mtu yeyote asifanye fujo. Anayetoka atoke. Mtu yeyote asifanye fujo. Leo Bunge hili litaendeshwa kisayansi. Msiwe na wasiwasi. Mheshimiwa Mariam Kisangi.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, sawasawa. Wewe ndio kiongozi, tumekuchagua na wewe ndio mwenye mamlaka ya kuweza kupanga taratibu zote za Bunge.

SPIKA: Namwambia Serjeant-at-arms, habari ya watu kutoka hapo nje mara sijui Waandishi wa Habari na nini, marufuku! Anayetaka sijui kuongea ongea nini, nje ya geti.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Sawasawa.

SPIKA: Anayetaka kuongea, aongee humu ndani. Naomba Serjeant-at-arm awe macho hapo. Endelea Mheshimiwa Mariam.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, nia yako ni njema. Unapomwambia mtu yeyote ambaye amelikosea Bunge kumpeleka kwenye Kamati ya Maadili, kwa maana nyingine ulikuwa unawasaidia watu hawa kwa sababu Kamati ya Maadili siyo Kamati ya kuadhibu mtu tu, bali ni Kamati ambayo inazingatia maelezo ambayo mtu anatoa; na pale anapoomba msamaha, Kamati hii haiwezi kuacha kumsamehe.

Mheshimiwa Spika, lakini watu wanapokuja kwenye Kamati ile na kuendeleza ubabe na kuendeleza maneno yasiyofaa, ile Kamati, sisi ni Wabunge lakini pia tunao uwezo wa kufikiri na kuangalia nini kinachoendelea katika maisha na taratibu za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bunge leo ni mhimili. Mhimili wa Bunge unaunganisha viongozi mbalimbali wa Kitaifa wakiwemo Waheshimiwa Mawaziri, Waziri Mkuu, Mheshimiwa Spika mwenyewe na viongozi mbalimbali. Sasa inapotokea mtu akasimama akasema kwamba Bunge ni dhaifu, hatuwezi kukubali.

Mheshimiwa Spika, sisi Waheshimiwa Wabunge tumepata taabu kugombea leo hii kuja kuwawakilisha wananchi hapa. Leo hii akili zote hazipo, ziko Majimboni. Tunapofika hapa Bungeni tukasema dhaifu, ina maana sisi dhaifu? Siyo sawa. Serikali yetu, Wabunge ndio tunaopitisha Bajeti, ndio tunaopitisha miradi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, leo katika Mkoa wa Dar es Salaam miradi yote muhimu; mwendokasi, barabara nane, miradi kibao imeenda, kazi yote hiyo na Mbunge, iweje leo Bunge hili liambiwe kuwa ni dhaifu? Hiyo haiwezekani.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono azimio hilo. Nasema yote yaliyopendekezwa kwenye Kamati ni sawa sawa. Tuchukulie pia hili Bunge kuna watu mbalimbali wanakuja kujifunza humu ndani ya Bunge. Tunao vijana huko juu, wanafunzi wa Shule za Msingi, Sekondari, Vyuo Vikuu, wanakuja kujifunza katika kwenye Bunge hili, tafiti mbalimbali zinafanyika katika Bunge hili, leo anatokea mtu huko anakuja kusimama kwamba Bunge hili ni dhaifu, sisi tukubaliane naye! Hatuwezi kukubali, tunaungana nawe Mheshimiwa Spika, lazima Bunge letu sasa liwe na nidhamu. Wabunge tuwe na nidhamu, tuangalie mazingira gani ambayo unaweza ukaongea maneno gani.

Mheshimiwa Spika, upotokaji wa maadili unazidi kuwa mkubwa ndani ya Bunge. Kwa maana hiyo, azimio hili la Kamati iwe fundisho sasa kwa Wabunge wengine na viongozi wengine walio nje au ndani ya Bunge kwamba wauheshimu mhimili wa Bunge. Bunge linafanya kazi kubwa sana na linapitisha mipango mbalimbali ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, pia napenda nitoe angalizo kwa Waheshimiwa Wabunge wetu vijana, kama Mheshimiwa Godbless Lema, sisi tunawategemea vijana, sisi ni watu wazima, umri unaenda, tutafika sehemu itabidi tuwaachie vijana hawa waendeleze nchi yetu. Leo Mbunge anasimama anaongea maneno yasiyofaa ndani ya Bunge, anatuambia nini sisi kama wazee ambao tunawatarajia wao tuwape nafasi hizi waendeleze Taifa hili? Je, viongozi kama hawa tukiwapa nafasi wataliacha salama Taifa letu kwa utovu huu wa maadili?

Mheshimiwa Spika, tumekumbana na hii hali kwa muda mrefu, sasa umeamua na sisi tuko tayari kuku-support, hatuwezi kukubali kwamba Bunge liwe mtu anasimama anatukana anafanya hivi na hivi kisha anaachiwa. Hiyo haikubaliki hata kidogo. Lazima taratibu za Bunge zifanywe.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuambiwa huyu Godbless Lema kwamba yeye amekosea aliambiwa siku moja kabla kulikuwa na masaa 24 kwa mtu huyu kutafuta njia mbalimbali za kutubu na kuomba msamaha kwa kosa lake. Bunge kuna taratibu mbalimbali kwa mujibu wa kanuni. Kuna hoja binafsi, kuna kumwandikia Spika, kuna kumwomba Spika, lakini Mbunge huyu hakutaka kufanya taratibu yoyote ya kutaka kujinusuru na kuona kwamba labda kauli ile niliitoa kwa bahati mbaya aweze kupata msamaha.

Mheshimiwa Spika, kwenye Kamati tulimwomba sana; je, kijana wetu huwezi kujutia hilo tatizo lako? Kwa mapenzi makubwa. Anasema mimi nimekubali, kama kufungwa nitafungwa, nimefungwa sana, jambo ambalo siyo sawa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono Azimio hili la Bunge na niwaombe Wabunge wenzangu kwamba sasa ifike sehemu awe Mbunge gani kama ulivyoongea kwamba awe Mbunge wa Chama gani, bila kujali Chama, wote kwa pamoja tuzingatie nidhamu na maadili ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.