Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru sana Kamati ya Katiba na Sheria na Kamati ya Sheria Ndogo kwa taarifa nzuri ambazo wameziwasilisha mbele ya Bunge hili. Mengi ambayo wameyaainisha katika ripoti zao kama mapendekezo tutayafanyia kazi ili kuboresha huduma zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Watanzania tuna bahati kubwa sana ya kuzaliwa katika nchi hii ya Tanzania na katika mfumo ambao unatoa haki na uhuru kwa watu kuliko nchi nyingi nyingine. Watanzania tuna uhuru, tuna haki ambazo zinalindwa na Katiba lakini viko pia viko vyombo vingi ambavyo vimeundwa kuhakikisha kuwa haki hizo ambazo ziko ndani ya Katiba zinaheshimiwa au zinafuatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni miongoni mwa nchi chache sana katika Bara la Afrika ambazo hazifiki nne, ambazo zimewaruhusu raia wake kuweza kuishtaki Serikali katika Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu. Hivi tunapozungumza sasa katika Mahakama hiyo yako mashauri 113 ambayo yamepelekwa na Watanzania dhidi ya Serikali. Nchi moja ya jirani baada ya kufanyiwa hivyo imejiondoa katika Mahakama hiyo. Tunavyozungumza leo asilimia 75 ya mashauri yote katika Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu yanatoka Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Watanzania sasa wana haki na wameitumia haki hiyo kwenda kufungua mashtaka dhidi ya Serikali kwa madai mbalimbali katika Mahakama ya Afrika ya Mashariki. Tunapozungumza sasa mashauri 13 ya Watanzania wanaodai kuwa haki zao za binadamu zimevunjwa yako katika Mahakama ya Afrika ya Mashariki. Nchi nyingine zimehakikisha raia wao mashtaka hayo hayaendi na sina haja ya kuzitaja kwa sababu zinafahamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunavyozungumza sana yako zaidi ya mashauri ya Kikatiba 40 katika Mahakama Kuu ya Tanzania; mashauri matano ya Kikatiba katika Mahakama ya Rufaa, hayo yote yanaonyesha kwamba tunao mfumo na taasisi zinazowawezesha Watanzania kusimamia haki zao. Ndiyo maana hivi karibuni Mahakamu Kuu, katika kesi ya Emmanuel Simphorian Masawe imetoa mwongozo wa jinsi ambavyo Mkurugenzi wa Mashtaka atatumia mamlaka aliyonayo kuhusu suala zima la kutoa certificate ya kuzua bail inapohitajika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi tunajadili suala la haki za binadamu hapa nchini bila kuangalia maamuzi ya Mahakama. Labda hilo nisiwalaumu Watanzania, nijilaumu mimi pamoja na Maprofesa na wasomi wengine ambao tumeshindwa kuandika commentary ya maamuzi ya Mahakama ya Rufaa ambayo yametoa tafsiri ya vifungu mbalimbali vya Katiba ndiyo maana kila mtu amekuwa anasoma Katiba ilivyo bila kwenda kwenye maamuzi mbalimbali ya Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuipongeza sana Mahakama, inafanya kazi kubwa. Kwa kweli Mahakama ya Tanzania iko mbali sana. Wote ambao walisikiliza hotuba ya Jaji Mkuu siku ya Jumatano, hotuba ya kurasa 40 na niko tayari, hotuba hiyo kuichapa na
kuwagawia Wabunge wote waone mambo aliyoyasema kwa ufasaha na umakini Profesa Ibrahim Hamis Juma. Jaji Mkuu wa mfano, Jaji Mkuu mweledi, Jaji Mkuu mcha Mungu alieleza wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Law Day, bahati mbaya sana Watanzania mambo madogo tunayafanya kuwa makubwa. Mimi naona aibu kubwa sana kuona Wanasheria nchi hii wanajadili suala la Mkuu wa Mkoa kupita kwenye red carpet wanasahau ile ilikuwa ni siku ya kuzindua Mwaka wa Mahakama na anayezindua Mwaka wa Mahakama ni Head of State na anayemwakilisha Head of State ngazi ya Mkoa na Wilaya ni RC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda muone Mwaka wa Mahakama unavyozinduliwa Uingereza, unazinduliwa na Askofu Mkuu wa Canterbury, kwa nini? Ni kwa sababu kwa Waingereza Askofu Mkuu wa Canterbury kwa protocol ni namba mbili na hakuna anayeuliza kwa sababu ni taratibu yao. Head of State (Malkia) hawezi kuhudhuria ile sherehe, anayehudhuria ni number two, ni Archibishop of Canterbury. Kwa hiyo, hii ni Head of State na wala tusiikuze kwa sababu ni kuzindua Mwaka wa Mahakama. Nawaomba Wanasheria Tanzania wazingatie mambo muhimu yaliyozungumzwa na Jaji Mkuu, tuache nani kapita kwenye red carpet, yellow carpet au green carpet, hayo siyo mambo ya msingi kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuipongeza sana Mahakama. Mahakama imefanya kazi kubwa sana katika kupunguza mlundikano wa mashauri. Kwa Mahakama ya Mwanzo imejipa muda kwamba ndani ya miezi sita mashauri yawe yamekwisha na mpaka sasa mashauri ambayo yamevuka miezi sita ni 16 tu. Mahakama ya Wilaya imejipa mwaka mmoja kuwa imemaliza mashauri na mpaka sasa kesi ambazo zimezidi mwaka mmoja ni 837. Katika Mahakama Kuu ni miaka miwili na kesi ambazo zimevuka miaka miwili ni 1,860. Katika Mahakama ya Rufani ni miaka miwili na kwa kesi ambazo zimevuka miaka miwili ni 729.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa kuiongezea Mahakama idadi ya wafanyakazi mwaka jana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutumia mamlaka aliyonayo ndani ya Katiba akishauriwa na Judicial Service Commission aliteua Majaji wawili (2) wa Mahakama ya Rufaa na Majaji kumi (10) wa Mahakama Kuu. Mwaka huu kwa kutumia mamlaka yake hayo hayo, akishauriwa na Judicial Service Commission amechagua Majaji sita (6) wa Mahakama wa Rufaa na katika Majaji hao wanne (4) ni wanawake na wawili (2) ni wanaume, namba kubwa sana. Kwa hiyo, pia akina mama ndani ya nchi hii mjipongeze na kujisifia kwamba mwaka huu mmeweza kutoa Majaji wa Rufaa wanne (4). Hayo ndiyo mambo ya kujadili badala ya kujadili mambo madogomadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais ameteua Majaji wa Mahakama Kuu kumi na tano (15). Kwa mara ya kwanza katika Majaji hawa kumi na tano (15), Mheshimiwa Rais ameweza kuteua Mahakimu wa Kawaida (Resident Magistrate) mmoja (1) kutoka Bukoba, kijana mdogo na mwingine kutoka Shinyanga aliyekuwa Hakimu wa Shinyanga ili kuonyesha kwamba Ujaji unaendana pia na weledi lakini pia ujasiri na kusimamia sheria na haki. Kwa hiyo, niipongeze sana Mahakama kwa kufanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la Mahakama zinazotembea (Mobile Court) tulisema hata wakati ule tulipondoa hiyo hoja katika Bunge, tuliondoa hoja hiyo kwa sababu Jaji Mkuu ana mamlaka ya kuzianzisha Mahakama hizo bila kuleta sheria Bungeni. Ametumia mamlaka aliyonayo, Mahakama hizo amezianzisha na zitaendelea kufanya kazi. Tayari magari mawili yamefika na yataanza kufanya kazi katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mkoa wa Dar es Salaam Mahakama hizo zinazotembea itakuwa Bunju Wilaya ya Ilala, Chanika Wilaya ya Temeke, Buza na Kibamba Wilaya ya Ubungo. Kwa Mkoa wa Mwanza ambao pia una mashauri mengi, gari linakwenda Mwanza na litatoa huduma hizo kwenye Wilaya ya Ilemela huko Buhongwa na Igoma na Wilaya ya Nyamagana kule Buswelu. Baadaye magari yatakapoongezeka huduma zitasambaa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mlivyomsikia wenyewe Mheshimiwa Rais ametoa maagizo linunuliwe gari La Mobile Court na gari hilo liwe na Mahakimu wanawake kwa ajili ya kushughulikia kesi za mirathi za wanawake. Tutatekeleza maagizo hayo ili tuhakikishe tuna Mahakama inayotembea kwa ajili ya kushughulikia kesi za mirathi ya wajane ambazo Mheshimiwa Rais amesema kesi zao zinachukua muda na wanaonewa. Kwa hiyo, Mahakama hizo zinazotembea zitaendelea kufanya kazi na hakuna mahali tulipovunja sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa watu wayajue magari haya. Ndani ya magari hayo kuna huduma nyingi, kuna televisheni kwa ajili ya kurekodi ushahidi, kuna computer, printer na lifti ya kuwainua watu wenye ulemavu, kuingia na kushuka. Kwa hiyo, hiyo bei ya gari siyo gari tu ni pamoja na facilities nyingine ambazo ziko ndani ya gari hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuipongeza sana Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali. Ni Ofisi ambayo imeanza hivi karibuni lakini imefanya kazi kubwa sana. Imesimamia kesi nyingi za mashauri ya usuluhishi na mpaka sasa inasimamia mashauri 42 ya usuluhishi kwa weledi mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuboresha jambo hilo pia tutaanzisha kitu ambacho kinaitwa Haki Mtandao. Hivi karibuni Mahakama imeshaweka mtandao siyo lazima wafungwa au mahabusu watoke gerezani kwenda Mahakamani. Mambo ya kuahirisha kesi yatafanywa hukohuko mfungwa akiwa gerezani na Hakimu akiwa Mahakamani, kwa kutumia video link kesi hiyo itamalizwa na itaondoa tatizo la kubeba mahabusu kwa magari. Ni kweli kabisa mahabusu wako wengi na Serikali inachukua hatua mbalimbali za kuhakikisha kuwa tunapunguza idadi ya mahabusu hasa wale wa kesi ndogo ndogo kwa kuwapeleka katika community service.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo limezungumzwa hapa na napenda nilizungumzie pia, nalo ni suala la haki ya tendo la ndoa kwa wafungwa. Napenda kusema kwamba tendo la ndoa si haki ya msingi ni jambo la hiari, ndiyo maana wako Waseja na Watawa wa hiari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tusilifanye suala la tendo la ndoa kuwa suala la msingi. Ni moja ya haki ambayo mfungwa anaweza kunyimwa kwa sababu siyo haki ya msingi. Hanyimwi chakula, mavazi na maji kwa sababu ni haki ya msingi lakini tendo la ndoa ni la hiari. Wako ambao ni rijali lakini kwa hiari wameamua wasilifanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, si vyema tukaanza kujiingiza katika mambo hayo ambayo kwa kawaida si utamaduni wa Waafrika kuanza kuzungumzia mambo ya tendo la ndoa. Ndiyo maana sisi ni mambo binafsi mno. Sasa tusianze kuiga mila nyingine, hata huko kwenyewe tendo la ndoa, kwa sisi tunaofahamu huko halifanywi gerezani, wale wafungwa huwa wanaruhusiwa kwenda kutembelea familia zao. Wenzetu kule ukihukumiwa mwisho wa mwaka huendi gerezani, unaripoti gerezani tarehe 2 Januari, ni utaratibu wao. Kwa hiyo, wale wenye umuhimu wa kufanya hivyo wanaruhusiwa kwenda huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda kabisa Bunge hili lisichukue muda mrefu katika jambo hili. Suala hili liliwahi kuwa ni moja ya maeneo yaliyofanyiwa utafiti na Tume ya Kurekebisha Sheria na likaonekana kwa nchi yetu halifai. Nchi moja ya jirani walitaka kufanya hivyo walishindwa kwa sababu ni suala la faragha, sasa kila mtu anajua mnaingia, hata uwezo unapotea. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo tumelipokea tutalifanyia kazi ni kuwachanganya wafungwa wenye umri tofauti, vijana na watu wazima. Hili ni suala la msingi sana na tutalifanyia kazi. Tutazimbelea Mahakama na kwa kweli tutahakikisha kwamba wafungwa hawa wanatenganishwa, hili ni moja ya jambo ambalo tunalipokea. Tayari Tume ya Kurekebisha Sheria imetoa ripoti inayoitwa Review of Police and Prisons Legislation, tutaona nini kifanyike ili kuhakikisha kwamba jambo hili linazingatiwa ili tutenganishe wafungwa kwa rika na umri wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la matumizi ya Kiswahili katika utungaji wa sheria, ni kweli kabisa wakati umefika wa kuanza kuzitunga sheria zetu kwa Kiswahili. Hata hivyo, napenda nitoe indhari siyo tahadhari maana ipo tofauti kati ya tahadhari na indhari. Ni kwamba hata tutakapoanza kuandika sheria nyingi kwa Kiswahili na sasa tayari tunaandika Miswada mingi kwa Kiswahili lakini someni Miswada ya Kiswahili si Kiswahili cha mtaani, ni Kiswahili chenye istilahi mbalimbali za kisheria ambazo ina maana baada ya muda itabidi tena watu wajifunze na wazielewe istilahi hizo na nyingine zinaweza kuwa zinakera masikioni kwa sababu hazijazoeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukiangalia Sheria ya Kiswahili ya Usimamizi wa Mazingira neno monitoring ni kupelemba lakini upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania neno kupelemba lina maana tofauti kabisa na ukienda huko usilitumie maana yake ni kumtongoza mwanamke. Kwa hiyo, hata huko pia tutakapoanza kutumia Kiswahili tujue kutakuwa na istilahi ambazo pia itabidi watu wazifahamu lakini ni kweli kabisa ni muhimu kuanza kutunga sheria zetu nyingi kwa Kiswahili badala ya Kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uchelewashaji wa kesi, hili tumeshaliwekea mkakati wa kuhakikisha kwamba tunapunguza ucheleweshaji wa kesi. Ucheleweshaji huo wa kesi unachangiwa na uchunguzi na sasa tunafanya jitihada kubwa kuhakikisha kuwa uchunguzi wa masuala mbalimbali ya kesi unamalizika kwa muda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto, zipo kesi nyingine zimechukua muda mrefu kwa sababu uchunguzi unahusisha kupata ushahidi kutoka nje ya nchi. Nashukuru kwa kuanza kutumia huu mtindo wa e-Justice hivi karibuni kuna kesi ambayo imesikilizwa ambapo shahidi alikuwa Ufaransa na kesi imefanyika Tanzania na shahidi aliweza kutoa ushahidi kutoka Ufaransa bila yeye kulazimika kuja. Kwa hiyo, ni moja ya maeneo ambayo tutayafanyia kazi ikiwa ni pamoja na kuongezewa idadi ya Majaji na Mahakimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndugu zangu napenda kusema kwamba tunaishukuru sana Kamati kwa mambo mengi ambayo imeyaorodhesha. Kwa Watanzania kwa ujumla, napenda sana tujue hatuna nchi nyingine nje ya Tanzania na labda tunaichezea kwa sababu hatujaenda kuona nchi nyingine ambazo zimechezea amani yake zimeishia wapi. Siyo lugha nzuri na wala haipendezi kutaka kuleta mabadiliko kwa kuanza na vitisho, nchi hii itaendelea kuwepo na itaendelea kuwa na amani kama sisi wenyewe tutaamua kuwa na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni lazima Watanzania tuwe na staha, tumefika mahali sasa tumeanza kukosa staha. Baadhi ya lugha tunazozisikia ndani na nje ya nchi haziendani kabisa na Utanzania wetu, utanzania ni pamoja na kustahi/kuyaheshimu mamlaka. Mkuu wa nchi ni taswira ya nchi hii, mkuu wa nchi anawakilisha nchi hii, kwa hiyo, siyo vyema tunapoanza kumbeza, kumzalilisha na kumdharau na tukadhani kwamba hiyo ndiyo demokrasia. Ni lazima tutofautishe kati ya demokrasia na laxity, there is a big difference between democracy and laxity. Tulizoea laxity na wakati wa laxity umekwisha. Kwa hiyo, demokrasia ni pamoja na kujua na mipaka yako na heshima hasa kuheshimu mamlaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa uvumilivu mkubwa sana alionao. Amevumilia upumbavu, upuuzi na ujinga mwingi lakini tusiendelee kufanya hivyo kwa sababu sisi wengine
ambao tumepewa kazi ya kuhakikisha heshima hiyo inalindwa tutatekeleza wajibu wetu na tutatekeleza bila tashwishwi hata kama baadaye watu watasema tumebadilika kwa sababu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Dakika moja Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja za Kamati zote mbili. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, mobile court, kutokana na msongamano ulivyo na tulishawahi kushauri kwa nini Mahakama nazo haziendi jela au mahabusu na kupunguza msongamano?

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo hilo limechukuliwa na moja ya hatua ambazo tumekubaliana, tunaanza katika awamu hii ni kuanza kutemebelea Magereza. Mkurugenzi wa Mashtaka pamoja na Mahakimu wakitembelea Magereza wana haki ya kutoa maamuzi ya kuwaachia baadhi ya wafungwa pale ambapo Mkurugenzi wa Mashtaka ameridhika kwamba watu hao kwa kweli kesi zao ni ndogo na tayari amekwishafanya hivyo. Katika hotuba ya bajeti tutaeleza idadi ya mahabusu walioachiwa baada ya ziara za DPP kuanza katika Magereza mbalimbali.