Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba ya Kamati hizi mbili; Kamati ya Katiba na Sheria pamoja na Kamati ya Sheria Ndogo katika kuweka mambo sawa juu ya sheria zetu na mambo yanayoendelea ndani ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi kabisa, naomba niruhusu nianze kwa kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati zote mbili, Mheshimiwa Chenge, Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria Ndogo na Mheshimiwa Mchwengerwa, Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. Hakika kazi zao zinaonekana na binafsi napenda kuwaambia kuwa waendelee kupambana hivyo hivyo kwa sababu sheria inataka wasimamizi wazuri kama wao na wanafanya kazi nzuri, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, nishukuru na kupongeza sana sana Kamati ya Katiba na Sheria kwa jinsi ilivyoendesha mchakato wa usimamizi wa utungaji kama si urekebishaji wa Sheria ya Vyama vya Siasa. Hakika mchakato ule ulikuwa mgumu kutokana na makundi mengi kuwa na interest katika jambo lile. Kwa kweli jinsi mchakato ulivyoendeshwa vyama na wadau walivyoweza kushirikishwa mpaka mwisho tumekuja kupata marekebisho yaliyotokana na lile pendekezo la Serikali, kwa hakika ni jambo zuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwaambia wanasiasa wenzangu kwamba siku zote tusitegemee kupata kitu kilichokamilika kwa asilimia mia moja isipokuwa kwa hii hii asilimia 90 tuliyoipata tushukuru na pale kwenye upungufu basi twende katika taratibu za vyombo vya sheria ili kuweza kupata kilicho haki yetu au kile ambacho tunakiona kimekosewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, niendelee kuzungumza na Mheshimiwa Waziri wa Sheria, mara zote tunapokutana kwenye Kamati ya Sheria Ndogo kilio chetu sisi kama Wanakamati kimekuwa ni dosari zinazojitokeza katika utungaji wa sheria. Makosa ya kiufundi katika uandishi, makosa ya kutotambua au kutoangalia sheria mama inasema nini, makosa ya kiuandishi kwa maana ya copy and paste na kusahau mamlaka, ni mambo ambayo yamekuwa yakiendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitoa mawazo na maoni yetu katika mchango wetu kikao kilichopita kwamba Wizara yenu Profesa wangu, Mheshimiwa Kabudi ijikite zaidi kuangalia jinsi gani inatengeneza waandishi wazuri ambao watakuwa na weledi wa kutosha ili siku nyingine tutakapokuja tuwe na kazi ya kuelezea mazuri au upungufu wa kisheria na si ya kimuundo kama ambavyo tumekuwa tunafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini Kamati yetu hatuna wataalamu wa kutunga sheria, hivyo Waziri kupitia ofisi yake anaweza kutusaidia kufanya kazi hii ya kuweka vizuri miundo ya kuangalia vizuri dosari zinazojitokeza ili tuendelee kuwa wenye kufanya kazi ndogo ambayo imetuleta Bungeni. Bungeni hapa hatukuletwa kwa ajili ya kuangalia miundo tumeletwa kwa ajili ya kutunga sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, niendelee kuishukuru Serikali katika kufanya kazi yake kubwa imeendelea kukamilisha miundombinu ya Mahakama. Pamoja na kazi nzuri ambayo imeendelea kufanywa hakuwezi kuwa na Mahakama kusipokuwa na nyumba na nyumba hiyo lazima watu wakutane ili haki ziweze kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zama hizo haki zilikuwa zinatolewa chini ya miti lakini katika dunia ya sasa Mahakama zetu zinahitaji majengo mazuri, teknolojia za kisasa pamoja na kuwa na miundombinu rafiki zaidi ili kusaidia ile shughuli ya kutoa haki iweze kufanyika. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa jinsi ambavyo ameendelea kulisimamia jambo hili lakini pia nimeona kupitia hotuba ya Kamati na taatifa mbalimbali za Wizara kwamba kuna Mahakama za Mwazo zaidi ya tano ambazo zimeshakamilika ikiwemo ile Mahakama ya Bagamoyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya watu wa Bagamoyo nitumie nafasi hii kukushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu watu wetu wakati mwingine walikuwa wakitamani wakae nje ya Mahakama kwa sababu ya kuogopa kuangukiwa na dari za majengo ya Mahakama hizo. Pamoja na hilo, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa jinsi ambavyo ameendelea kutoa mchango mkubwa sana katika tasnia ya sheria lakini pia kuonesha kwamba ni Profesa wa Sheria na kuendelea kusaidiana nao kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita Kamati yetu imeweza kuangalia na kutoa mapendekezo mbalimbali ya jinsi sheria zinavyoweza kukaa vizuri. Hata hivyo, bado upo upungufu ambao unaendelea kuonekana hasa katika sheria, kwa mfano, ile ya Baraza la Sanaa ambayo mapendekezo yake tumeyatoa na kupitia Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe tulimpa taarifa. Binafsi nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe kwa sababu alishafika mbele ya Kamati yetu na kueleza hatua ambazo zimeshachukuliwa na kwa kweli sisi kama Kamati tumeridhika. Namwomba Mheshimiwa Waziri aendelee kusimamia tasnia na wasanii wetu ili waendelee kunufaika naye. Pamoja na hilo, yapo mapungufu ambayo tumeendelea kuyaeleza kama ya kiuandishi na kimuundo ambayo yanatakiwa yawekwe sawa ili sheria ile iweze kuchukua nafasi ya utelelezaji na tusije tukapata mikwamo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limeelezwa jambo lingine juu ya kodi zetu kuwa si rafiki. Katika kitabu cha hotuba ya Wizara ya Sheria imeelezwa kwamba ipo baadhi ya migongano inayotokana na sheria ambazo zipo katika maeneo mengi, hasa katika sheria za vijijini kama zilivyoelezwa na Mheshimiwa Getere hapa, leo hii kuna baadhi ya vijiji ikionekana mtu amejenga nyumba ya bati basi kuna ushuru mkubwa kwake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimkumbushe tu Mheshimiwa Waziri katika utaratibu ambao tumeshajipangia ni kwamba nchi hii kakuna mtu ambaye atatozwa kodi mara mbili. Ipo kodi tunayolipa tunapokwenda kununua mabati na cement, je, iweje leo hii tufike sehemu ya kulipa kodi nyingine ambazo ziko kinyume na utaratibu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini si mwisho kwa umuhimu, ziko baadhi ya sheria ambazo zinahitaji sana marekebisho. Katika kitabu chetu cha hotuba ya Kamati ya Sheria Ndogo zimeelezwa na jinsi ambavyo zimeendelea kuonekana zinakinzana na sheria mama lakini pia zinakinzana na sheria nyingine zilizopo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)