Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Kamati zote hizi mbili. Awali ya yote, naunga mkono Kamati zote mbili. Vile vile namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia na hatimaye kuweza kusimama hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kabisa, naishukuru Serikali hasa Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa kweli niwapongeze sana kwa jitihada kubwa wanazofanya katika kuhakikisha makundi maalum na hasa kundi la watu wenye ulemavu ambalo leo hii nitapenda zaidi nilizungumzie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nisiisahau pia Wizara ya Katiba na Sheria, nawapongeza sana kwa jinsi ambavyo wamekuwa nao katika suala la Sseria kuzingatia masuala ya watu wenye ulemavu. Vilevile kwa kuwa katika ukurasa wa 25 wamezungumzia makundi maalum, wakiwemo pia watoto, nichukue nafasi hii pia kukemea mauaji yanayoendelea huko Mkoani Njombe hasa ya watoto na Mwenyezi Mungu pia awajalie familia ambazo zimepoteza watoto. Pia wale watoto waliotangulia mbele ya haki, basi Mwenyezi Mungu awalaze mahali pema Peponi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kwa kuzungumzia suala zima la michezo kwa ajili ya watu wenye ulemavu; na nitapenda pia kunukuu Mkataba wa Umoja wa Mataifa, Ibara ya 30 unaelekeza nchi wanachama kushirikisha watu wenye ulemavu kwenye michezo. Vilevile Sheria yetu ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2010 Sheria Na. 9 inatoa haki ya watu wenye ulemavu kushiriki kwenye michezo kupitia Kifungu cha 52.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Kimataifa inazungumzia inclusive policy ambayo Tanzania pia imekubali na imeridhia. Ni kweli nchini kwetu tumekuwa tukizungumzia masuala mbalimbali, hasa katika michezo, tunazungumzia kwa ujumla na hasa mpira na michezo mingine ambayo inawahusisha wenzetu ambao kwa namna moja au nyingine wako kamili kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa watu wenye ulemavu, kwa kweli Serikali bado imekuwa nyuma pamoja na kwamba tumeridhia hii sheria, bado michezo kwa watu wenye ulemevu haijapewa kipaumbele na wala haijatiliwa mkazo. Nasema hivyo, kwa sababu hakuna fungu lolote, hakuna mahali ambapo Serikali imejitoa katika kusaidia watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano; walikuja wenzetu ambao ni kutoka katika Chama cha Watu Wenye Ulemavu ambao wanahusika na michezo. Kwa bahati nzuri sana mwaka huu kuna mashindano yatafanyika hapa nchini kwetu mwezi wa Sita yatahusisha watu wenye ulemevu kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati. Jumla ya nchi 12 zitashiriki, lakini mpaka sasa bado wanahangaika hawajui wapi ambako kwa kweli wanaweza wakasaidiwa. Ni heshima kubwa kwa michezo hii kufanyika hapa nchini mwetu, lakini ningeiomba Serikali katika majibu yao watakapokuja kutueleza, watueleze kwamba katika hili wamejiandaje basi ili kufanikisha michezo hii, lakini kama tunavyofahamu michezo ni ajira, michezo ni afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia michezo hii inatukutanisha kwa pamoja walemavu kutoka sehemu mbalimbali. Kwa hiyo katika ile michezo inakuwa ni faraja kwetu pia, kwa hiyo niombe tu kwamba Serikali ione kwamba inatekeleza sera hizi katika kusaidia hawa watu wenye ulemavu kwenye michezo kwa sababu pia itawasaidia kuongeza kipato cha kwao wao binafsi pia na familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili naomba sana Serikali waweze kuliona kwa sababu katika Kamati yetu ni kweli tunasimamia Ofisi ya Waziri Mkuu na kipekee mimi nawapongeza kwa sababu kuna jitihada kubwa sana ambazo zimefanyika na niseme tu kwa kweli kwa Mheshimiwa Rais wetu nampongeza sana kwa moyo wangu wa dhati kabisa, kwa jinsi ambavyo ameyapa kipaumbele masuala watu wenye ulemavu. Hilo kwa kweli tunajivunia na hata kwa Afrika Mashariki kitendo cha kuwa na Naibu Waziri katika Baraza la Mawaziri, hii ni faraja kubwa sana na ni mfano ambao hata wengine wenye ulemavu wakiona kwamba kwenye Baraza kuna mtu ambaye amefikia hatua hiyo, wanapata ile ari ya kusoma na kuweza kuwa na ndoto kwamba na wao siku moja watakuja kufika huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Rais wangu Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, nampongeza sana kwa hili kwa kutambua na kuwapa umuhimu na niseme tu kwamba sasa hivi watu wenye ulemavu tumekuwa na heshima kubwa hata wazazi wale ambao walikuwa wanaona kwamba kuwa na mtoto mwenye ulemavu ni tatizo, sasa hivi wanaona kwamba kumbe akipata elimu na kwa kuzingatia kwamba sasa hivi elimu ni bure, kwa kweli hizi pongezi namwombea sana Mheshimiwa Rais wetu, Mwenyezi Mungu aweze kumpa maisha marefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo ningependa kuzungumzia mwishoni mwa mwaka jana nilipata bahati ya kuhudhuria kama mdau katika Ofisi ya Waziri Mkuu, walikuwa wanaandaa mwongozo ambao utawezesha kuwa na Mfuko Maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu na hili nimelizungumzia sana katika Bunge hili, ni matarajio yangu kwamba Mheshimiwa dada yangu mpendwa Jenista kwamba kwa mwaka huu ni matarajio yangu kwamba kwa sababu katika Bunge na hasa Ofisi ya Waziri Mkuu tuna fungu kwa ajili ya Bunge, tuna fungu kwa ajili ya vijana, tuna fungu kwa ajili ya masuala mengine, lakini hakuna fungu maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu kwa kweli nitakuwa mpinzani wa Mheshimiwa Waziri endapo hatokuja na fungu maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu. Matokeo yake kwamba sasa tumekuwa tukidandia tu katika haya mafungu mengine, vijana wanalo fungu lao na katika fungu hili mpaka katika mikoa yote wana ofisi zao. Sasa kama masuala haya tumeshayachukua na tumeshayapa kipaumbele ni muhimu sasa na hili pia wakati mwingine hata Naibu Waziri aweze kufanya kazi zake vizuri inakuwa ni busara zaidi akiwa na fungu lake, anajua kabisa kwamba hapa Mheshimiwa Waziri nitamshauri tufanye hivi, nitamshauri tuendeleze hivi, lakini pasipokuwa na fungu wakati mwingine unaweza ukaambiwa kwamba hakuna fedha kwa ajili ya masuala hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo dada yangu mpendwa namjua uwezo alionao, Mheshimiwa Jenista Mhagama namfahamu yeye ni mwanamke shupavu, ni mwanamke hodari amekuwa mfano bora na isitoshe kama mama basi hili atalibeba kwa hekima kubwa na ataliangalia pia kwa jicho la ziada kuhakikisha kwamba katika bajeti ya mwaka huu tunakuwa na fungu maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu na sio kudandia katika mafungu mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kuzungumzia kuhusiana na watu wenye ulemavu, naendelea kupongeza kwa sababu naona mabadiliko makubwa na ndio maana naendelea kujivunia, mwaka jana tulipitisha sharia…

MWENYEKITI: Ahsante kengele ya pili.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)