Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja za Kamati zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nishukuru na kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati, ama kweli ripoti hii wameitendea haki. Vilevile nichukue nafasi hii kumpongeza jemedari wetu, Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa namna anavyoiongoza nchi na kwa namna anavyoonesha mwelekeo, wapi tunataka kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivyo; lazima niweke kumbukumbu sawasawa, lazima tukumbuke kwamba, mimi sio mtu wa kuweza kunukuu vifungu vya Biblia au Quran lakini zipo sehemu ambazo watu wanasema, kwamba mdomo unaumba, lakini sio hivyo tu, kuna kauli nyingine unaambiwa kwamba sauti ya wengi ni sauti ya Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli ni zao la dua za Watanzania. Sikuwepo kwenye Bunge lililopita lakini nilikuwa nasikiliza ni namna gani Wabunge walivyokuwa wanaomba kwamba tunataka Rais mwenye msimamo, tunataka Rais anayekwenda kusimamia rasilimali za Taifa hili. Kwa sababu Mwenyezi Mungu anasikia, kilio cha wengi ni kilio cha Mungu, ndiyo akatupatia zawadi tukapata Rais ambaye sasa ni kweli anakwenda kuyatekeleza hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale ndugu zangu wanaobeza ni kwa sababu ya ubinadamu, kwamba binadamu ameumbwa ni mtu mwenye kusahau. Wameshasahau kwamba wao ndio waliopendelea wakamwomba Mwenyezi Mungu tupate Rais wa namna hiyo, kwa hiyo nilikuwa naweka kumbukumbu sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Wabunge tukumbuke moja ya majukumu yetu ni kutunga sheria. Sasa naomba nitoe ushauri kwa Wabunge; tunapokwenda kutunga sheria lazima tuwe makini kuhakikisha sheria hizi zinakwenda kufanya kazi ile ambayo tumeikusudia, lakini tunapokwenda kufanya kazi hii kwa kulipua matokeo yake tunakuwa wa kwanza kulalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewahi kusikia hapa kuna mchangiaji mmoja alikuwa analalamikia Sheria ya Korosho, kwamba kuna Mkuu wa Wilaya amewakamata watu wanatoa korosho kutoka Msumbiji kuleta Tanzania, lakini wanasahau kwamba kosa lile sisi ndio tumelifanya kwa sababu kwenye Sheria yetu ya korosho ukiangalia tunakataza korosho kutoka nje kuingia Tanzania na sio korosho tu, kuna mazao mbalimbali tumekataza kwenye sheria zetu, kwamba hakuna mtu anayeruhusiwa kutoa mazao nje ya nchi yetu kuyaleta Tanzania. Sasa hawa watekelezaji wanakwenda kutekeleza hizi sharia, bado kwenye Bunge hilihili sisi tunaona kwamba wale wanafanya makosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena kuna Mbunge mmoja alikuja akasema kwamba hii ni shame, ni jambo la aibu, kwamba eti kwa nini Msumbiji wanataka kuleta korosho, kuinua uchumi wetu, tuongeze pato letu tunawakataza, lakini anasahau kazi hiyo ameifanya yeye hapa Bungeni na ndiye aliyelipitisha jambo hili. Kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge tunapoifanya kazi hii tuifanye kwa umakini, tujue kwamba sisi ni wawakilishi wa wananchi na makosa haya mara nyingi yanafanywa na sisi wenyewe. Kwa hiyo hilo ndilo jambo ambalo nimeona kwamba niweze kulisemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nirejee kwenye utunzi wa sheria. Naomba kuanza na sheria ndogo, Mheshimiwa Mwenyekiti ametoa mapendekezo hapa na ametaja kasoro mbalimbali zinazotokana na utunzi wa sheria ndogo. Kuhusu jambo hili naomba niishauri Serikali, hapa tunasema hizi sheria ndogo, lakini sheria hizi ndizo ambazo ziko karibu na wananchi wetu, ndiko ambako wanakwenda kuzi-practice hizi sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninachoomba kwa Serikali ni lazima tuhakikishe kwamba, hawa Wanasheria tunaowapeleka kwenye halmashauri zetu ni Wanasheria waliobobea katika fani hii ya sheria. Vinginevyo tunapoacha kupeleka Wanasheria waliobobea kwenye halmashauri zetu tunakwenda kuziangusha halmashauri zetu na ndiyo maana tunapata hizi kasoro ambazo zinaletwa kwenye marekebisho ya sheria ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu, kuna matatizo mengi sana kwenye halmashauri, kuna kesi nyingi sana kwenye halmashauri ambazo halmashauri zinashindwa kwa sababu tu hatuna Wanasheria wenye weledi, hatuna Wanasheria waliobobea na matokeo yake tunashindwa kwenye kesi mbalimbali matokeo yake halmashauri zetu zinaingia kwenye madeni mbalimbali, kulipa fidia na kulipa faini mbalimbali. Hii yote ni kutokana na uchache au weledi wa Wanasheria wetu. Kwa hiyo hapa mimi naishauri Serikali kuimarisha kitengo hiki cha sheria kwenye halmashauri zetu ili tuepukane na hizi adha ambazo tunaweza kuzipata kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka nichangie kuhusiana na uhaba wa upatikanaji wa huduma ya sheria hasa kwenye ujenzi wa Mahakama. Halmashauri zetu nyingi hazina Mahakama; kwa mfano Halmashauri yangu ya Wilaya ya Liwale ni halmashauri ambayo iko tangu mwaka 1975, lakini leo naongea 2019 hatuna jengo la Mahakama ya Wilaya. Si hivyo tu, Wilaya ya Liwale kwa mfano ina tarafa zaidi ya tatu na kata zaidi ya 20, lakini mpaka leo naongea kwenye Bunge hili tuna Mahakama moja tu ya mwanzo; hatuna Mahakama nyingine ya Mwanzo; na hiyo Mahakama yenyewe ya mwanzo ni Mahakama ambayo ilijengwa na wananchi; lakini mpaka leo liko tu jengo la tope na Mhudumu yuko mmoja tu, Hakimu ambaye ndiye Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hapa naweza kuishauri Serikali, kwamba ili tuweze kwenda na wakati na mnajua dunia sasa hivi dunia hii ni kama kijiji; kwa hiyo uhitaji wa Mahakama ni mkubwa sana. Kwa hiyo, naishauri Serikali ipanue hii huduma ya Mahakama ili tuweze kutoa huduma kwa wananchi wetu. Hili jambo ni la muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kwenye Mahakama za Mwanzo; Mahakama nyingi za Mwanzo zina uhaba mkubwa sana wa wafanyakazi, hasa Mahakimu. Si hivyo tu, kwa sababu ya uchache tulionao kwenye Mahakama imepelekea sasa kuwe na vitendo vingi vya rushwa, ili mtu kesi yake labda iishe mapema, inabidi atoe rushwa. Si hivyo tu, ule upeke kwanza exceptionalist wa mtoa huduma ambaye yuko pale na kesi zile zilikuwa ni nyingi. Kwa hiyo inakuwa ni miongoni mwa vivutio vya kuweza kuendeleza hii rushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naiomba Serikali, kuna sera inahusu wazee. Ukiingia kwenye huduma mbalimbali unakuta kuna mahali pameandikwa wazee kwanza, mpishe mzee, fanya hivi, lakini ukiangalia kwenye Bunge hili hatujawahi kutunga sheria inayohusu wazee. Hawa wazee ambao wanambiwa wapishwe labda wawahi wazee ni wazee wa aina ipi? Sheria haijawatambua wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali kwamba itulee sheria ya wazee ili hawa wazee ambao tunawaongelea siku zote tuweze kuwatambua, na tukiweza kuwatambua ndipo tutaweza kuwatendea haki. Vilevile tukumbuke sisi wote humu ndani ni wazee watarajiwa. Kwa hiyo naomba niishauri Serikali sikivu ya Chama cha Mapinduzi, ilete hii Sheria ya Wazee ili hawa wazee waweze kutambuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naomba niishauri Wizara ya Sheria na Katiba. Kumekuwa na tatizo kubwa sana la ucheleweshwaji wa kesi Mahakamani. Jambo hili linakuwa linaongeza sana mlundikano wa mahabusu kwenye magereza zetu. Kwa hiyo naiomba sana Serikali iongeze bidii ili wananchi hawa watendewe haki yao; kwa sababu haki iliyocheweshwa ni sawa kabisa na mtu aliyeikosa haki hiyo. Kwa hiyo naiomba Serikali iongeze watumishi kwenye Idara za Mahakama na vilevile kuongeza ofisi kwenye idara hizi za mahakama ili kesi mbalimbali ziweze kwenda kwa wakati na ziweze kwisha kwa wakati ili kupunguza mlundikano kwenye magereza yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye huo huo utunzi wa sheria; mara nyingi nimeona Serikali ikileta sheria hapa ili zifanyiwe marekebisho; zile ambazo zimepitwa na wakati. Kwa mfano unakuta sheria inataja labla mtu akifanya offence fulani atapata adhabu ya kulipa 2,000 au 5,000. Hizi ni sheria ambapo zimepitwa na wakati. Kwa hiyo Serikali wamekuwa wakizileta hizi sheria hapa kuzifanyia amendment ili kuongeza hivi viwango kulingana na wakati tulionao. Hata hivyo bado tunasahau kuzifanyia marekebisho zile sheria ambazo zitawasaidia wananchi wetu. Mathalani kuna sheria inasema kwamba mwananchi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)