Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. JASSON S. RWEIKIZA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru tena kwa kunipa nafasi ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kuhitimisha hoja yangu niliyoitoa asubuhi.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja yangu ni Wabunge 18. Awali ya yote nawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri; Mheshimiwa Jafo, Mheshimiwa Mkuchika na Waheshimiwa Manaibu Waziri; Mheshimiwa Kandege, Mheshimiwa Waitara na Mheshimiwa Mwanjelwa kwa michango yao ambayo imesaidia kutoa baadhi ya majibu.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya Wabunge kadhaa wamechangia sana kuhusu elimu. Kamati yangu inakubaliana na Wabunge hawa kwamba elimu kwa kweli kuna kazi za kufanya kubwa sana mbele yetu. Tunahitaji kuboresha Sekta ya Elimu na lazima Serikali iwe na mpango mkakati mzuri, mpango madhubuti wa kuboresha elimu. Walimu bado ni haba sana. Wanaostaafu nafasi zao hazijazwi, lakini wasomi wapo ambao wamesomea Ualimu na ingekuwa vizuri sana kuboresha sekta hii kwa kuajiri Walimu wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, huwezi kuwa na shule ina wanafunzi 600, una Walimu watatu. Kwa keli hutoi elimu, isipokuwa tu wanapita pale, wanahitimu, wanaondoka, lakini hawaelimiki. Vifaa, madawati, majengo, madarasa, vyoo; ni vizuri mkakati ukaboreshwa kusudi elimu iweze kuwa bora zaidi. Ndiyo maana hapa Mheshimiwa mmoja ametoa takwimu, amelinganisha shule binafsi na shule za Umma. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri Waitara akijibu, akasema kwamba shule binafsi zinakaririsha. Nitangaze maslahi kwamba mimi niko kwenye sekta hii ya shule binafsi.

Mheshimiwa Spika, kuna wakati ilikuwa ni fedheha kusoma shule binafsi huko nyuma miaka ya 1970, 1980; ilikuwa ni fedheha kwenda shule binafsi. Baadaye wazazi wakawa wanepeleka watoto wao Uganda, Kenya na nchi nyingine huko kupata elimu bora, lakini baadaye pia tena Watanzania wakajiongeza, wakajizatiti wakajenga shule humu ndani Tanzania nami ni mmojawapo. Sasa kwa kweli hawa wa binafsi wanazingatia sana ubora. Kwa hiyo, ndiyo tofauti iliyopo.

Mheshimiwa Spika, Serikali ikiboresha hivi vitu; Walimu, vifaa, madawati, vyoo na vifaa vingine, elimu itakuwa bora. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli kwa kusema elimu ni bure. Baadaye shule hizi zitakufa zenyewe tu, zitaondoka zenyewe kwa sababu zina gharama kubwa kuziendesha na ndiyo maana tunasema kama mpango wa elimu bure utafanikiwa, shule za binafsi zitakufa zenyewe. Hakuna haja ya kuzipiga vita, tunafanya kazi moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge wamechangia kuhusu suala la Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kunyanyasa wananchi na kuwaweka ndani na mambo mengine. Nashukuru Serikali imechukua hatua, Mheshimiwa Mkuchika na Mheshimiwa Jafo wamepambana sana na hawa watu, walikuwa wanakiuka sheria. Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli na Mheshimiwa Waziri Mkuu wamekemea sana tabia hii, lakini haijaisha, bado ipo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuna haja bado ya kuendelea kuwadhibiti Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya waache kunyanyasa watu. Kazi yao siyo kunyanyasa watu, ni kuwatendea kazi, kuwasaidia kwenye harakati za kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Nkamia amezungumzia jambo la uchaguzi kwamba maendeleo hayaji kwa uchaguzi. Ni kweli jambo hili linazungumzika na linafikirisha. Sisi tumeingia humu tuna miaka mitatu, leo homa imeshaanza ya uchaguzi wa mwaka kesho. Watu Majimboni wanapita huko, wanajipitisha huko, wanasumbua; tunakaa humu nusu nusu, uko nusu; mguu mmoja ndani, mmoja nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tungekuwa na miaka saba, labda mtu angekuwa ametulia hapa mpaka 2022. Sasa kwa sababu tunaelekea mwakani kwenye uchaguzi, homa imeshaanza humu, presha inapanda, inashuka. Sasa inakuwa taabu sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kuna nchi nyingine nyingi Afrika humu, Rais anagombea vipindi vingi tu miaka mitano, mitano, hata mara 10 kama ana uwezo huo na anaendelea na wanafanya vizuri; nimeziorodhesha hapa nchi kama 22 au 21; Chad, Cameroon, Comoro, Congo, Djibout, Equatorial Guinea, Ethiopia, Gabon, Gambia, Liberia, Lesotho, Libya, Swaziland, Morocco, Mauritius, Sudan, Togo na Uganda hata Rwanda, nirudi nyuma tena sasa.

Mheshimiwa Spika, hawa hawana limit ya kugombea, hata kwa nafasi ya Rais, anagombea hata vipindi vitatu, vinne, vitano, kumi. Margaret Thatcher alikaa miaka 11, Waziri Mkuu wa Uingereza; Angela Markel ana miaka 16 na tusiseme kwamba sisi tumeendelea kuliko wao. Hata hao Waafrika, Ethiopia wanatuzidi maendeleo, Mauritius wanatuzidi maendeleo; Togo wako juu kuliko sisi, lakini wanagombea kwa muda mrefu na wanakaa. Wengine katika hawa wana vipindi vya miaka saba, saba kama Cameroon miaka saba, Gabon miaka saba na hakuna ukomo. Kwa hiyo, jambo hili ni la kuzingatia na inafaa kulijadili ili ikiwezekana Mheshimiwa Nkamia alete hoja yake hapa Bungeni tuijadili halafu tuone inakwenda vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa wamechangia kuhusu TARURA. Kamati inasema kwamba TARURA ina kazi kubwa sana imeifanya. Tangu imeanzishwa muda mfupi uliopita, imesimamia kazi za barabara za vijijini na mijini. Barabara ndogo ndogo nyingi za Dar es Salaam ni za TARURA. Kwa hiyo, TARURA ina kazi kubwa sana lakini haina pesa. Kwa hiyo, tunasisitiza kwamba TARURA iongezewe fedha kutoka Mfuko wa Barabara (Road Fund) badala ya asilimia 30 iwe asilimia 50 ili barabara za TARURA ziweze kutengenezwa ziende vijijini kule kwenye mazao, zipeleke pembejeo mwaka mzima tuwe na huduma nzuri vijijini.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili la barabara za TARURA na TANROADS, barabara kuu zimekamilika bado kidogo tu; Katavi, Kigoma na sehemu nyingine. Kwa hiyo, ikienda asilimia 50 TANROADS itatosha kukarabati barabara ambazo zipo na kujenga zile mpya chache, lakini asilimia 50 iende TARURA ili nao waweze kupata uwezo wa kujenga barabara zao.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamechangia kuhusu TASAF. TASAF imefanya kazi nzuri sana ya kupigiwa mfano, lakini tunasisitiza kwamba Serikali itoe mchango wake kwenye TASAF, tusitegemee tu wafadhili pake yake. Serikali itoe mchango wake kusudi wale wa asilimia 30 ambao hawapati mchango wa TASAF wapate huduma hiyo na waweze kupata tija ya hela ya TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge wamechangia kuhusu Sekta ya Afya. Naipongeza Serikali sana kwa kujenga hospitali 67 za Wilaya na Vituo vya Afya 650 kwa muda mfupi. Ni jambo kuba sana la kusifia, la kuishukuru Serikali. Kujenga hospitali moja inahitaji shilingi bilioni saba na nusu; fedha iliyotolea ambayo tunashukuru ni shilingi bilioni moja na nusu. Tunasisitiza kwamba hii iliyobaki shilingi bilioni sita itolewe kusudi hospitali hizi zijengwe ndani ya muda unaotakiwa na zikamilike kwa ukamilifu wake.

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa lingine, wataalam watafutwe, waanze kuajiriwa na kuandaliwa. Kwa sababu mwezi wa Sita siyo mbali sana, Madaktari, Wauguzi, Manesi na wengine wawepo kwa sababu hospitali 67 ni nyingi sana Vituo vya Afya 350 ni vingi kiasi cha kutosha.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamechangia kuhusu maji vijijini na hali ya maji vijijini haijawa nzuri, bado ni mbaya. Tumesema sana humu Bungeni kwa miaka mingi kwamba tuunde Wakala wa Maji Vijijini. Tunashukuru kwamba juzi juzi hapa sheria imepitishwa hapa ya RUWASA kuunda Wakala wa Maji Vijijini.

Mheshimiwa Spika, Wakala huu tunataka uanze kazi mara moja, upewe fedha, uwezeshwe, kazi ianze. Kamati inaunga mkono kwamba ile shilingi 50 kwenye petrol na diesel ikatwe kusudi iende kwenye mfuko huu ambao unaanzishwa chini ya Wakala wa Maji kusudi huduma iweze kuwa nzuri kwa watu wa vijijini ambao wana shida kubwa sana ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nimalizie kwa kusema kwamba, tumekuwa na dhana ya D by D (Devolution by Decentralization); kazi nyingi zinafanyika kwente Halmashauri kule, kwenye Madiwani, kwenye vijiji, kwenye vitongoji, na mitaa. Kumekuwepo na mwelekeo sasa hivi wa kuondoa huduma hizi huko kuzirudisha Makao Makuu ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, mambo ya maji, Hospitali za Mikoa zimesharudi Wizarani, kuna mambo ya ardhi yanarudishwa Wizarani. Sasa hii itakatisha tamaa, Halmashauri zitakosa kazi za kufanya; na iko kwenye Katiba kwamba Decentralization iendelee kuwepo ili wananchi waone kwamba wanamiliki miradi hii na wafanye kazi kwenye miradi hii kwa moyo na kwa kupenda.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba sasa michango hii na mapendekezo haya ya Kamati yaweze kuazimiwa na Bunge hili ili Serikali iweze kuyatekeleza.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Spika, naafiki.