Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Nazipongeza Kamati zote tatu kwa taarifa ambazo zimewasilishwa mapema leo asubuhi na naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, pili, nina kila sababu kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uthubutu, upeo mpana alionao na ujasiri anaouonyesha hasa pale ambapo anaziona fursa za kusukuma mbele Taifa hili. Nasema hivyo kwa sababu mwaka jana tulitembelewa na Rais wa FIFA na alipofika Mheshimiwa Rais aliacha ujumbe mfupi sana na huo ujumbe aliuwasilisha Waziri Mkuu wetu Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwamba Rais anachotaka ni viwanja kumi vizuri.

Mheshimiwa Spika, nafikiri Rais wa FIFA hajazoea vitu kama hivyo, kwa kweli aliupokea huo ujumbe kutoka nchi ambayo imedhamiria kazi. Alichoahidi tu ni kwamba atashirikiana na nchi yetu na kuisaidia kuifungulia TFF haraka ile kesi iliyokuwa imefungwa na ana uhakika kwamba tutapata viwanja hivyo na tutawasiliana naye. Naomba tu nitoe taarifa kwamba sasa hivi tumefunguliwa na FIFA, msaada wa FIFA umeanza kuja. Kwa kweli ile rai ya Mheshimiwa Rais tutaanza kuitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kifupi napenda kusema kwamba tumekaa na wenzetu wa TFF na sehemu ya fedha fedha ambayo tumepata tutaitumia kuboresha viwanja kumi nchini kwa kuanzia kama ambavyo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alivyotaka. Kwa sababu Aprili, Rais wa FIFA Gianni Infantino atakuwa hapa si ajabu akaulizia kuhusu hilo, ndiyo maana kwa kweli tumeona hilo lazima tulitekeleze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbali na viwanja hivyo kumi, tutakarabati upya kabisa Uwanja wa Karume, kujenga hostel mpya, ofisi na majukwaa ya uwanja huo. Mimi naahidi hatutarejea tulikotoka maana kulikuwa na udokozi mkubwa kweli TFF. Miaka kadhaa iliyopita nchi tano, sita kila nchi tulipewa dola 400,000, sisi tukaishia kujenga vile vibanda pale Ilala, lakini Rwanda na Sudan wana maghorofa, huwezi kuamini tulipewa pamoja. Vilevile tutajenga Hosteli ya TFF Tanga, madarasa na ukumbi mkubwa pamoja na kiwanja, kwa hiyo tunaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika fedha iliyoanza kuingia ilikuwa shilingi milioni kadhaa mara moja nimeona TFF wakitenga pesa kwenda ZFA, zaidi ya shilingi milioni 100. Tutaendelea na ushirikiano namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuna hoja aliyoitoa leo asubuhi Mheshimiwa Khatib Haji kuhusu uhusiano kati ya TFF na ZFA. Kwa kifupi sana TFF na ZFA ni mashirikisho dada, nikitumia muktadha wa Kiingereza kama sister federations. Moja inasimamia soka upande wa Tanzania Bara na nyingine Tanzania Zanzibar. Mashirika haya mawili ni wanachama wa CECAFA wanaojitegemea, CECAFA ina nchi 11 lakini tukienda CAF vilevile tunajitegemea lakini ujumbe wa Zanzibar siyo kamili sana kwa sababu ni mwanachama ambaye ni associate, ni mshiriki. Ndiyo Zanzibar anapata kila kitu lakini hawezi kupiga kura. Tunapokwenda FIFA (Shirikisho la Mpira Duniani), hapa ndipo ambapo Zanzibar hawana nafasi kabisa inabidi kwa kweli wasimamiwe na wenzao wa TFF.

Mheshimiwa Spika, nachotaka kusisitiza hapa ni kwamba tutambue kwamba TFF na ZFA si idara za Serikali, hizi ni taasisi huru zenye vyombo vyake vya maamuzi, Wizara sisi tunao tu ule ushawishi wa kisera. Nataka niendelee kuamini kuwa ZFA itaendelea kupokea misaada mbalimbali kutoka FIFA kupitia TFF. Pale penye utata, vyombo hivi viwili viendelee kujadiliana na ukiwa mkubwa zaidi basi wasisite kutuona sisi. Kwanza nisisitize tu kwamba wenzetu ZFA wasinyamaze wakiona kuna tatizo na pengine kutafuta mpaka Wabunge waje waliongee suala hilo ndani ya Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Haji nikusisitizie tu kwamba tunaongelea Uwanja wa Gombani kama tulivyosema leo asubuhi tumeutolea mfano, ni kama vile ambavyo tunatoa mfano hapa wa viwanja viwili tu pamoja na ukubwa wa nchi hii; ni Uwanja wa Kaitaba na Uwanja wa Nyamagana. Ni kwa sababu tulikotoka kwa kweli matumizi ya pesa hayakuwa mazuri sana; pengine tungepata viwanja kumi kumi kama tungekuwa waangalifu lakini sasa tumefungua ukurasa mpya kama nilivyosema.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la Mheshimiwa Nkamia na Mheshimiwa Kabati kuhusu Ligi ya Wanawake na ligi za Daraja la Kwanza na nyingine, pale ambapo ligi hizi hazina ufadhili (sponsorship) kwa kweli kuandaa home and away matches ni kuwatesa sana vijana wetu. Nawahakikishia kwamba tutakaa chini tuliangalie upya na nawaonea huruma Waheshimiwa Wabunge wengi sana wanabeba mizigo hiyo ya kusafirisha timu na kuzilaza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mwamoto ameongelea kuhusu mashindano ya AFCON. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mwamoto kwamba limekaa vizuri kama ambavyo Mheshimiwa Waziri Mkuu amelielezea vizuri leo asubuhi. Tuna Local Organizing Committee ambayo naiongoza mimi lakini ina wajumbe wengi kutoka taasisi mbalimbali za Serikali na tuna viongozi mbalimbali kama wajumbe akiwemo Waziri wa Maliasili na Utali, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Jenerali wa Uhamiaji na viongozi wengine mbalimbali na kwa kweli tumejipanga ili mwezi Aprili kisiharibike kitu. Tarehe 12 naongea na Wahariri wa vyombo vya habari kuhusu ugeni mkubwa tutakaoupata na tutaanzisha hiyo kampeni nchi nzima. Vilevile tarehe 14 tunakutana tena kuweza kujadiliana kwa kirefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mara nyingi umeshakuwa mgeni rasmi kwenye mechi, Uwanja wa Taifa uko katika ukarabati mkubwa sana. Vilevile Uwanja wa Uhuru uko kwenye ukarabati mkubwa ambapo tunang’oa kabisa zile nyasi na nyasi zake za bandia ziko melini na tutaziweka baada ya muda si mrefu pale uwanjani. Uwanja mwingine wa Chamanzi ambao utatumika ukarabati wake unamaliziwa, kwa hiyo umekaa vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Joseph Mbilinyi ameshangaa CCM kumiliki Channel Ten na Magic FM, sijui kama yupo…

MBUNGE FULANI: Hawezi kuwepo.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, atapata ujumbe tu kwamba asisahau kuwa CCM ina vyombo vya habari vyenye umri sawa na uhuru wa nchi hii. Vyombo vingine kimkakati ni kawaida duniani kushikiliwa na wapenzi wa chama na si kitu cha ajabu sana. Kwa mfano, gazeti la Tanzania Daima linamilikiwa na mpenzi wa CHADEMA, si la CHADEMA ni la mpenzi wa CHADEMA lakini siku litakapohamia CHADEMA utashangaa kweli? Huwezi kushangaa! Sasa unashanga kwa nini anashangaa mpenzi wa CCM aliyekuwa na chombo kwenda CCM, asishangae ndivyo mambo yanavyokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kabati ameongelea soka la kike. Naomba nimhakikishie kwamba soka la kike linakwenda vizuri, mimi mwenyewe nimefarijika sana. Naomba niwakumbushe tu wenzetu hapa kwamba tuna Twiga Stars, tunasahau tunashikilia tu timu za wanaume, Twiga Stars ni ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamechukua kombe la CECAFA mara mbili mfululizo; mwaka 2016 na 2018. Hawa akina mama ni mashujaa kweli kweli na kwa kweli soka la kike tunalikazania sana. Kuna wenzao wengine Kilimanjaro Queens nayo imekuja juu; mmesikia hivi karibuni ikichukua ubingwa wa Afrika Mashariki kwa mara ya kwanza. Sifa ya timu hii ni kutokuwa na huruma inapocheza, inabamiza watu magoli mengi sana. Kwa mfano, mchezo wa kwanza na Burundi watu wengi walishangaa, ilikuwa ni taarifa Afrika nzima, baada ya kuipiga Burundi magoli nane kwa moja. Akina mama hawa hawana huruma kabisa, mchezo wa marudiano ikiwa tano bila. Ni timu nzuri sana na naomba nimtaje mfungaji bora ambaye ni Mwanahamisi ambaye peke yake alifunga magoli saba. Tumezoea kuwataja wanaume tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie tu kwa kuwaomba Waheshimiwa Wabunge ushiriki wao katika maandalizi ya AFCON ambayo yatafanyika Aprili na yatahusisha nchi nane bora katika Bara la Afrika. Tuiombee Serengeti Boys, timu ambayo kwa kweli imebeba matumaini ya Watanzania. Ikishinda mechi mbili tu Tanzania kwa mara ya kwanza tangu uhuru tutashiriki katika Kombe la Dunia kupitia timu ya Serengeti.

Mheshimiwa Spika, sipendi uniambie nikae chini, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)