Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja iliyopo mbele yetu. Kwanza kabisa, napenda kuanza kwa kusema kwamba ninaunga mkono hoja za Kamati tatu ambazo zimewasilishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee kabisa, nami nichukue nafasi hii kuishukuru na kuipongeza kwa dhati kabisa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendelo ya Jamii kwa namna ambavyo wamekuwa wakitushauri kwa maoni na mchango mzuri. Hakika nikupongeze na wewe kwa namna ambavyo uliisuka hiyo Kamati, ina watu ambao wanajali kabisa na wana michango mizuri. Niseme mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba Kamati hii ni tofauti kabisa na namna ambavyo watu walikuwa wanai-perceive wakati unaiunda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli tunafanya nao kazi vizuri, wamekuwa wakitupa maoni mazuri na tumekuwa tukisonga mbele kwa sababu kuna ushirikiano mzuri na maoni mazuri kutoka kwa Kamati. Kwa hiyo, baada ya shukrani hizo niseme tu kwamba tumepokea maoni na ushauri wa Kamati na Serikali itayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kutolea ufafanuzi baadhi ya hoja ambazo zimejitokeza katika mjadala wa hoja iliyopo mezani leo hii. Kwanza kabisa, kuna suala ambalo limezungumzwa la upungufu wa Wahadhiri hasa wale wenye kiwango cha Shahada ya Uzamivu pamoja na Maprofesa na hasa katika Chuo Kikuu cha Dodoma.

Mheshimiwa Spika, niseme kweli kuna upungufu wa Wahadhiri katika vyuo hivyo na ndiyo maana Chuo Kikuu cha Dodoma hakijaweza kudahili wanafunzi capacity yake ni 40,000 lakini tunafahamu kwamba chuo kikuu siyo majengo tu ni pamoja na kuwa na Wahadhiri wenye sifa. Nilihakikishie Bunge lako kwamba Serikali inafanyia kazi suala hili kwa nguvu zote na katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Serikali ilitenga shilingi bilioni 4 ambapo tayari kuna Wahadhiri 68 ambao wanafadhiliwa na ufadhili wa Serikali kwa ajili ya Shahada za Uzamivu na kati yao 14 wanatoka Chuo Kikuu Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na juhudi za Serikali kutoa fedha zake kusomesha Wahadhiri lakini pia Serikali imeendelea kutafuta scholarship mbalimbali. Tuna scholarship 77 ambapo wameenda kusoma China, 30 wameenda kusoma Hungary, 26 wameenda kwa utaratibu wa Commonwealth pamoja na scholarship nyingine.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nimshukuru Mheshimiwa Rais, pamoja hizi scholarship 77 za China lakini kwa juhudi yake aliongea na Serikali ya China akaomba tuongezewe kwenye fani ya udaktari ambako tuna upungufu mkubwa. Serikali ya China ikaongeza scholarship nyingine zaidi kufuatia ombi la Rais. Kwa hiyo, nilihakikishie Bunge lako kwamba Serikali inafanyia kazi uhaba wa watumishi wa vyuo vikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo limezungumziwa ni umuhimu wa kuimarisha mafunzo ya ufundi stadi na kuhakikisha kwamba tunakuwa na watu ambao wamebobea na ambao wanaweza hata kujiajiri. Naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba Serikali inaona umuhimu wa kuimarisha mafunzo ya ufundi stadi na tumekuwa tukiendelea kuwekeza katika vyuo vya ufundi stadi. Kwa mfano, sasa hivi tunaendelea na ujenzi wa VETA za Mikoa katika Mikoa ya Rukwa na Geita lakini taratibu za kumpata mkandarasi Simiyu zinakamilika na kwa watani wangu Kagera nilikuwa huko juzi kuangalia maandalizi ya kiwanja ambacho kimeshakamilika na mkandarasi anaweza akaanza kazi wakati wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeendelea pia kuimarisha VETA za Wilaya na hata hivi karibuni mwezi Januari Serikali imetoa kiasi cha fedha shilingi bilioni 1 kwa ajili ya kuimarisha majengo ambayo Halmashauri imeipatia Serikali ili yaendelezwe kama vituo vya ufundi stadi. Tumepeleka fedha Ileje, Palamawe kule Nkasi, Kamachumu, Urambo, Cherekeni pamoja na Kitangali kwa ndugu yangu Mheshimiwa Mkuchika. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba tunaendelea kuimarisha vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi. Sasa hivi pia tunaendelea na ukarabati wa vyuo 20 vya maendeleo ya jamii. Yote hii lengo lake ni kuongeza ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo napenda kulitolea ufafanuzi ni mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu. Waheshimiwa Wabunge wengi wamelizungumzia lakini pia hata katika taarifa ya Kamati wamezungumzia suala la vigezo vya mikopo na mambo mengine na kama nilivyosema ushauri wa Kamati tumeupokea. Hata hivyo, napenda kutoa ufafanuzi wa mambo machache, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, vigezo vya mikopo vimekuwa vikiboreshwa kila mwaka ili kuangalia changamoto zilizojitokeza na kutoa fursa kwa mwaka ujao. Kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge, kama wana maeneo mahsusi ambayo wangefikiri ni muhimu Serikali iyazingatie katika utoaji wa mikopo, iko tayari kuyapokea na kufanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni la wanafunzi wanaohama kutoka chuo kimoja kwenda kingine. Utaratibu ni kwamba mwanafunzi anapohama anahama na masomo aliyokuwa anasoma na mkopo wake kama alivyokuwa anapata. Kama nilivyotoa taarifa wakati Mheshimiwa Ester Mmasi alivyokuwa anazungumza, iwapo kuna wanafunzi wanakwenda na kusoma kitu ambacho ni tofauti hilo ni tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna wanafunzi 208 kati ya 1,699 ambao walihama na mpaka leo bado hawajapata mkopo. Hii inatokana na changamoto za taarifa zao kwa sababu kuna baadhi ya wanafunzi ambao unakuta taarifa zile za kozi aliyokuwa anasoma awali inatofautiana na kozi aliyokuwa anakwenda, ikitokea hivyo kwetu inakuwa ni tatizo mpaka hizo taarifa tuzihakiki lakini pia kuna ambao wana tatizo la masuala ya mitihani.

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba huu ni uzembe wa baadhi ya vyuo na hatuwezi kuendelea kuwaumiza wanafunzi kwa masuala ambayo wao siyo wanaopeleka taarifa. Tayari Bodi ya Mikopo ilishaviandikia vyuo barua tangu tarehe 17 Januari wahakikishe huu utata wa taarifa unaondolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa nasema hivi, ikifika tarehe 15 Februari, kusiwepo na mwanafunzi hata mmoja ambaye amehamishwa na bado hajapata mkopo wake kwa sababu kumekuwa na mvutano. Napendekeza Tume ya Vyuo Vikuu ingeangalia katika sheria yake namna ya kuviadhibu vyuo ambavyo vinashindwa kutoa taarifa za wanafunzi kwa wakati na matokeo yake wanafunzi wanaumia wakati hawana tatizo lolote. Hilo nadhani ni eneo ambalo tungeangalia kuvibana zaidi vyuo katika sheria zetu ili viache huo mfumo ambao wakati mwingine kutokana na taarifa hizo wanafunzi wanakuwa wanacheleweshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala limezungumzwa la usajili wa shule kwamba kutokana kazi nzuri ya Mheshimiwa Rais wetu ya kutoa elimu bila malipo mwitikio wa wananchi umekuwa ni mkubwa, sasa ifike mahali Serikali iruhusu wanafunzi wakasome maturubai au madarasa ya nyasi. Mimi sioni kama tumefika hapo, kwanza Serikali inafanya kazi kubwa sana ya kukabiliana na ongezeko la wanafunzi ambao wanajiandikisha shuleni kutokana na elimu bila malipo na Serikali imekuwa ikijenga miundombinu lakini pia Halmashauri zetu tumeona kazi kubwa inafanyika. Niseme hapa elimu ni haki ya kila mtoto lakini pia ni jukumu la Serikali kuhakikisha ulinzi na usalama wa watoto.

Mheshimiwa Spika, leo hii tulivyokuwa tunatoka mvua ilikuwa inanyesha, Waheshimiwa Wabunge wote hakuna aliyekuwa anakwenda, walikuwa wamekaa wanasubiri kwanza mvua iondoke. Hatuwezi tukaruhusu miundombinu ambayo ni hatarishi kwa maisha ya watoto wetu. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba kabla ya kuruhusu shule isajiliwe, itakaguliwa kuhakikisha kwamba miundombinu yote ambayo shule imeiandaa iko salama kwa ajili ya watoto wetu, waweze kupata elimu lakini tuna jukumu pia la kulinda usalama wa watoto wanapokuwa shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo limezungumziwa ni kuhusu kuboresha mfumo wa elimu yetu lakini pia lugha ya kufundishia. Nashukuru hili suala kila linapojitokeza kunakuwa na mjadala ambao upande mmoja unaona tutumie Lugha ya Kiswahili lakini pia kuna hoja ya kwamba lugha peke yake siyo jawabu, suala ni kuangalia changamoto kwa nini wanafunzi hawafanyi vizuri. Nafurahi kwamba katika mjadala tumeonesha kwamba hesabu kwenye shule za msingi wanafundishwa kwa Kiswahili lakini hawafanyi vizuri. Kwa hiyo, ushauri nimeupokea, jambo la msingi ni kuangalia zile changamoto zinazosababisha wanafunzi wasifanye vizuri na Serikali izifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kwa ridhaa yako nizungumzie suala la uhaba wa walimu. Ni kweli kuna baadhi ya maeneo kuna uhaba wa walimu, kwa hiyo, tutaendelea kuomba Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuangalia pale ambapo kuna walimu ambao wamezidi kuwe na mgawanyo sawia. Mheshimiwa Kapteni Mkuchika ameshazungumzia suala la kuajiri kuziba zile nafasi za wastaafu ili zile shule ambazo kweli hazina walimu kabisa tuweze kuzipatia walimu kwa haraka. Pia Serikali itaendelea kuwasimamia walimu wafanye kazi yao vizuri na kuwapatia mafunzo kazini ili wawe na weledi wa kutosha na hivyo basi tuongeze ubora wa ufaulu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na kwa mara nyingine naunga mkono hoja. (Makofi)