Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuwa kitinda mimba katika mjadala huu wa leo. Nami napongeza Kamati hizi tatu kwa taarifa zao nzuri. Pia nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amesimama kidete sana katika kusimamia ukusanyaji wa mapato na ndiyo maana tunaona matokeo haya sasa, tunazungumza ujenzi wa mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye Kamati, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI na Utawala. Kamati hii imetoa taarifa nzuri, nijazie tu kidogo kwa upande wa ukurasa wa 57 kuhusu ujenzi na ukarabati wa Vituo vya Afya pamoja na zile hospitali 67 na vituo 350. Pale tumefanya ziara katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, lipo tatizo dogo kwamba katika utoaji wa fedha hatukuangalia sana, tumetoa ile flat rate, hatukuangalia utofauti wa maeneo. Maeneo yanatofautiana, kuna mengine yana udongo mbaya, topography nyingine ni mbaya.

Mheshimiwa Spika, tulienda Kituo cha Afya Mlali, walipewa shilingi milioni 400. Kuna maeneo kweli zimetosha, lakini Mlali hazikutosha. Ukiona kile kituo, wanasema kimekamilika lakini ukiangali ubora wa majengo, kwa kweli hauko sawa sawa. Majengo yameanza kupasuka kabla hata hayajakabidhiwa. Kwa hiyo, utoaji wa fedha uangalie maeneo na maeneo.

Mheshimiwa Spika, kuna vituo vingine wamejenga, lakini fedha zimeisha na vituo havijakamilika, kwa maana kwamba walizingatia ubora. Sasa katika kuzingatia ubora, zile fedha zikawa hazitoshi. Serikali itoe zile fedha iongeze vituo vile vikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la elimu kidogo. Tunao Waraka wa Elimu Na. 2 wa mwaka 2016. Huu waraka unazungumzia ufaulu au kuruhusiwa Kidato cha Pili kurudia mwaka baada ya kufeli, kuvuka ile asilimia 30. Sasa hakuna waraka mwingine, ni huu katika private na shule za Serikali.

Mheshimiwa Spika, kuna taarifa ambazo tumeletewa katika Kamati, kuna shule zinarudisha wanafunzi au zinahamisha wanafunzi ambao wameshavuka hizi asilimia 30, wameweka viwango vya kwao 45 na 50, wakishindwa kuvuka hiyo wanarudishwa na wengine wanahamishwa kabisa wanaondolewa. Anaitwa mzazi kimya kimya, anaambiwa mzazi huyu mtoto hakufaulu, hapa siyo mahali pake, mpeleke shule nyingine.

Mheshimiwa Spika, natoa masikitiko yangu, huu ubaguzi unatoka wapi? Hawa watoto ni wetu. Vidole hivi ni vitano lakini havilingani pia. Hawa watoto ni wetu, tunalilia kujenga umoja, leo tunataka shule zetu watoto cream, yaani tunataka wawe na akili tu! Wote wanaofanana ili wapate Division One wote! Hii haikubaliki. Unaposema ahamishwe, apelekwe wapi? Wewe humtaki, nani atampokea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba huu Waraka, atakaposimama kama atapata nafasi Waziri anayehusika, mwenye dhamana, Profesa wangu, hebu atoe msisitizo kwa hizi shule ambazo zinakataa hawa wanafunzi ambao wameshafaulu kwenye hii asilimia 30 lakini wanaondolewa ili tu kulinda hadhi ya shule waweze kuvutia biashara. Hii siyo biashara, hii ni huduma. Hudumieni hawa watoto, ni wa kwetu sote hawa watoto, ni wa Taifa hili. Sasa mnapoanza kuwabagua…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mtuka. Nakushukuru sana kwa mchango wako, dakika tano zimeisha.

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hizi Kamati zote tatu kwa taarifa zao nzuri. Nakushukuru kwa nafasi hii, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Mtuka, ile Mlali uliyokuwa unasema ni ya Kongwa au ya wapi?

MHE. DANIEL E. MTUKA: Ya Kongwa.

SPIKA: Nashukuru sana.

MHE. DANIEL E. MTUKA: Ahsante.