Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa niseme mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na TAMISEMI na kwa sababu hiyo naunga mkono taarifa ya Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, mimi niko hapa mbele ulizoea kumwona Mbowe pale na Lissu hapa na wengine, sasa nipo peke yangu hapa kwa muda mrefu, kweli naumia na hivi nichukue nafasi hii kuwapa pole wenzangu Lissu, Mbowe na Matiko na kuwaombea Mwenyezi Mungu kwamba mitihani inayowakabili, basi waipokee na Mwenyezi Mungu ajalie siku moja tuweze kuwa pamoja tena hapa na najua itakuwa hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba nichangie kwenye utawala bora na nitazungumza kuhusu sheria mbili ambazo naona ni muhimu katika kipindi cha sasa nizizungumze. Sheria ya kwanza ambayo ningependa nizungumze kidogo ni The Regional Administration Act, 1997 ambayo ndio inawapa Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa mamlaka ya kuweza kuwaweka kizuizini Watanzania kwa masaa 24 au 48.

Mheshimiwa Spika, kabla sijasema hayo kwa sababu mimi ni muhenga, nimekaa nimeona utawala tangu Awamu ya Kwanza mpaka sasa ni kwamba zamani kulikuwa na utaratibu mzuri wa kuwapata viongozi hawa; Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa. Zamani kulikuwa na promotion walikuwa promoted kutoka kwenye miongoni mwa Makatibu Tarafa au Maafisa Ustawi wa Jamii na kadhalika. Sasa siku hizi wanapatikana namna gani sielewi, kwa sababu inavyoelekea wengi uzoefu wa kazi hiyo hawana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwa kweli Mzee Mkuchika Waziri amejitahidi sana kuwafunda na Katibu Mkuu TAMISEMI aliyestaafu Mzee Iyombe naye alijitahidi sana kuwafunda, lakini mambo haya yanaendelea na nayasema kwa sababu ni mambo ambayo yanaweza yakaleta chuki miongoni mwa jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sheria ile kifungu cha 7(2) na 15(2) pia vinaweka masharti ya namna viongozi hawa wanavyopaswa watumie ile sheria. Kwamba ili kumweka mtu ndani, Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa masharti manne lazima yazingatiwe. Jambo la kwanza, ni lazima kuwe na kosa la jinai; jambo la pili, kosa hilo lifanyike mbele ya kiongozi; jambo la tatu, kosa liwe linatishia na jambo la nne, kuwe hakuna njia nyingine yoyote ya kufanya zaidi ya kumweka ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi, viongozi hata na wawekezaji wamekuwa wakikamatwa kwa chuki. Mfano mdogo sana Iringa, waliwekwa ndani Diwani mwanamama Celestina Johansen kwa kosa ambalo lilifanywa na halmashauri kwa kuagiza nyumba ya mkazi mmoja ikavunjwe, mama kwa sababu ni Diwani wa eneo lile Mkuu wa Mkoa akaamua awekwe ndani kwa kosa ambalo sio la kwakwe. Mkuu wa Mkoa huyu huyu juzi alimkamata mwekezaji mmoja kwa kutolipa Cess, lakini polisi walivyochunguza wakagundua kwamba yule mwekezaji hana kosa lakini ameshawekwa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huko Ukonga pia Diwani Nancy Disunte naye alikwishawekwa ndani. Hai ndio usiseme, ni kila kukicha Madiwani wanawekwa ndani, Arumeru Mheshimiwa Diwani Elisa Mungure, Mbozi Mheshimiwa Pascal Haonga. Juzi Mkuu wa Mkoa wa Mara alimweka ndani Diwani wa Kata ya Mwema kisa alikunja nne akiwa kwenye mkutano wake.

Mheshimiwa Spika, mambo haya sio mazuri na nayasema kwa dhati kabisa kwa sababu naipenda hii nchi. Kwa maana mambo haya yanaweka chuki miongoni mwa wale wanaowekwa ndani na tusisahau wale wana jamaa zao na chuki hii ikiendelea kuvimba itazaa kisasi, upendo kwenye jumuiya utakosekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali kwanza ifanye vetting ya kutosha kuhusu viongozi hawa, lakini pili iwape mafunzo ya kutosha kwa sababu haya wanayofanya mwisho wa siku ni Serikali inaaibika. Hii ni kwa sababu hawa wote na wengine sikupenda niwataje, wakienda mahakamani watashinda kesi zao.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema tangu mwanzo, utawala bora ni utawala wa sheria na sisi viongozi tunalumbana na mambo yaliyo chini ya sheria. Kwa mfano jana tulisikia hapa juu ya upelelezi wa kesi ya Mheshimiwa Lissu, Waziri alisimama hapa akaeleza lakini Waheshimiwa viongozi humu ndani wana sheria mko wengi sana.

Mheshimiwa Spika, kuna ya The Mutual Assistance in Criminal Matters Act ambayo ina uwezo kabisa ikitumika wa kuchukua maelezo popote na hatua zikachukuliwa. Lissu hawezi kushindwa kufuatwa Nairobi, Ubelgiji au popote alipo kwa kutumia sheria hii ambayo tuliitunga wenyewe hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tukitoa matamko ambayo yanakinzana na hii sheria, watoto wetu wanakuja kusoma Hansard, watoto wetu wanakuja kufanya mitihani yao kwa kufanya reference ya haya tunayosema tunaonekana sijui ni Wabunge wa namna gani. Kwa hiyo, ombi langu kwa viongozi wa nchi yetu na Wabunge wote kwa pamoja tufuate sheria ambazo tunazitunga hapa itatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Mheshimiwa Selasini japo unamlaumu Waziri lakini kwa mfano dereva, kwa nini sheria hiyo ifuate si arudi tu aje atoe ushahidi?

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, wote hawa wawili wapo kwenye matibabu na wanaoweza kueleza kiwango cha namna miili yao imepokea matibabu ni Madaktari wao, lakini hii sheria Serikali, Wizara ya Mambo ya Ndani inaweza ikaitumia hata huyo dereva popote alipo akahojiwa.

SPIKA: Hao madaktari wameshaandika chochote kile kuleta huku?

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, lakini unaniwekea muda wangu eeh?

SPIKA: Muda wako nautunza kwa sababu…

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, ninachosema ili kuondoa hizi sintofahamu na kelele miongoni mwa jamii sheria hii ifuatwe popote pale walipo na haki itatendeka tu.

SPIKA: Lakini pia Madaktari si waandike ripoti ije?

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, sawa…

SPIKA: Mtunzieni muda wake, endelea Mheshimiwa.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza ni kuhusu uteuzi wa Wakurugenzi wetu. Zamani na nasema hili kwa sababu uliniweka kwenye LAAC katika kipindi chote cha Ubunge wangu kipindi kilichopita na tulipoanza Bunge hili uliniweka tena kwenye LAAC. Niligundua kwamba utaratibu uliokuwa unatumika ni kwamba Wakurugenzi walikuwa wanateuliwa miongoni mwa Wakuu wa Idara ambao tena wametumikia idara zao kwa sio chini ya miaka saba na kwa sababu hiyo Wakurugenzi walikuwa wana uzoefu mkubwa sana katika kazi zao, walizielewa halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, uteuzi ambao unafanyika sasa hivi tumewapata Wakurugenzi ambao sio wazoefu na matokeo yake imekuwa ni kama trial and error. Kwa mfano, Halmashauri ya Moshi (Moshi DC) miaka mitatu hii tayari imeshakuwa na Wakurugenzi watano na matokeo yake ni kwamba yaani ule utendaji unakuwa sio sawasawa na wengine ndio hawa tunaowasikia kwamba wanafanya kazi zao kibabe. Juzi tulisikia kwamba Mkurugenzi kapiga mtu risasi kanisani na mambo kama hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo hili pia ningeliomba Serikali iwe makini katika kuangalia kwamba ni nani tunawateua…

T A A R I F A

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, kabla sijaipokea nimweleze yeye kama Waziri anajua kwamba moja kati ya kazi za Bunge hili ni kumshauri Rais na kitu ninachofanya hapa ni kushauri. Kama yeye ni Waziri wa namna hii ina maana hamsaidii Rais, ndio maana anaogopa kumshauri. Mimi sijasema kwamba Rais apoke ushauri wangu, lakini ninachosema mamlaka za uteuzi zinazomsaidia Rais zihakikishe kwamba watu hawa wamekuwa vetted vizuri ili tupate watumishi wa kufaa katika kutumikia hii nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la mwisho ambalo ningependa kuzungumza naona nimepigiwa kengele…

SPIKA: Ooh kengele ya pili imeshalia. Ahsante sana Mheshimiwa Selasini. (Makofi)