Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia taarifa za Wizara hizo mbili, ambazo zipo mezani. Kwanza nianze kwa kuunga mkono taarifa hizo.

Mheshimiwa naibu Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi ambazo anaendelea nazo za kukutana na makundi mbalimbali katika kuendelea kuimarisha ili nchi yetu iendelee kusonga mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini kwa nzuri ambazo anazifanya za kuendelea kuimarisha katika kutoa huduma mbalimbali, lakini kwa dhamira njema ya kuhakikisha tunafikia malengo ya kuzalisha Megawatt 5000 katika kuhakikisha sasa Tanzania tunakwenda katika uchumi huo wa viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia ni mpongeze kwa dhati kabisa Mheshimiwa Waziri wa Madini, Mheshimiwa Dotto kwa kuteuliwa kwake na kuwa Waziri katika Wizara hii ya Madini. Ni Wizara mpya lakini ni Wizara ambayo inakwenda vizuri, tunafanya nayo kazi vizuri. Kwa kipindi kifupi tumeona jitihada kubwa sana wanazozifanya katika kukuza uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie upande wa REA ambao Waheshimiwa Wabunge wengi wameuzungumzia. Upande wa REA kwanza naipongeza nchi yetu kwani tumeweza kuwashawishi wawekezaji kuja kufungua viwanda vya uzalishaji wa nyaya, uzalishaji wa transformer, LUKU na vifaa mbalimbali pamoja na nguzo za umeme na kufanya kazi ya usambazaji wa umeme kuwa rahisi na kutumia muda mfupi katika utekelezaji wa usambazaji huu wa umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitegemea kwamba Wakala wa Umeme Vijijini kwa kutumia fursa hii wa uwepo wa viwanda ndani ya nchi, wangeweza kufanya kazi kwa speed ambayo tuliitarajia ya kusambaza umeme katika vijiji vingi nchini Tanzania. Tunajua kwamba mradi huu wa REA ndiyo mkombozi kwa wanyonge kule vijijini. Tumeona maeneo ambayo tayari umeme huu umefika, namna ambavyo vijana wamefurahia na wanahangaika kujiajiri katika kuendesha shughuli mbalimbali zinazotumia umeme. Kwa hiyo, umeme wa REA umekuwa ni mkombozi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kwa sababu tumetenga fedha kwa ajili ya mradi wa REA, lakini ukiangalia kiwango cha mafuta tunachoagiza na kuingizwa nchini na kiasi cha mafuta kinachouzwa: Je, kinalingana na ile fedha ambayo REA wanaipokea? Kwa hiyo, tunayo changamoto ya upatikanaji wa fedha ya kusukuma miradi hii ya REA kuhakikisha Watanzania umeme unawafikia. Pia tungeongeza Wakandarasi ili kusukuma hizi kazi ziweze kwenda kila kona na kuhakikisha umeme unafika kwa wakati kwa wananchi kule vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kuwapongeza Baraza na Mawaziri na kuipongeza Serikali kwa namna ambavyo wameweza kuondoa VAT katika umeme kule Zanzibar, wamefanya jambo la kiungwana sana. Kwa kweli hoja hii ilikuwa ina manung’uniko mengi sana, hata sisi Wanakamati tulikuwa tunajiona kwamba hatuna amani. Kwa hiyo kwa uamuzi ambao Serikali imeufanya kwa kweli tumefarijika sana, kwa sababu tumeona tunaendelea kuimarisha Muungano wetu ili twende vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie upande wa TANESCO, kwanza nilipongeze shirika kwamba linakwenda, totauti na pale zamani. Shirika hili sasa limeanza kulipa madeni kwa TPDC, kwa hiyo ni hatua nzuri sana kwa sababu sasa wanaweza kwenda. Shirika linaonesha sasa linajiimarisha. Rai yangu kwa Serikali, zile ofisi za Serikali ambazo zina madeni makubwa ziungane kwa pamoja kuhakikisha tunawaunga mkono TANESCO kwa kuwalipa madeni yao, ili sasa waweze kujiimarisha katika kuhakikisha wanatoa huduma iliyokuwa bora kwa wateja wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia kwa hatua mbalimbali ambazo wamezifikia, leo Watanzania tunanunua umeme kupitia simu zetu, wametupunguzia mzigo mkubwa tofauti na zamani, imeleta tija sana lakini pia imepunguza madeni, imeweza kufunga umeme wa LUKU, haya ni maeneo makubwa kwa Shirika hili la TANESCO.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada hizo kubwa ambazo wanazifanya kulikuwa na wizi wa umeme lakini wamejitahidi katika kudhibiti wizi ule wa umeme ambao ulikuwa unatokea. Kwa hiyo wote kwa pamoja tuungane katika kuhakikisha tunaendelea kulilinda shirika hili kwa kuwasaidia panapotokea tunaona katika maeneo umeme unabiwa, basi tuweze kutoa taarifa ili mara moja watu hao washughulikiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nipongeze juhudi kubwa zinazofanya na Serikali kupitia Wizara hii, tumeweza Serikali kupanua bandari pale Dar es Salaam kupunguza msongamano lakini Bandari ya Tanga na kule Mtwara ili kuweza kusogeza huduma kwa wananchi, ni maendeleo makubwa sana, kwa sababu kama wananchi wa Mikoa ya Kusini wanapata mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa kule Mtwara, kwa kweli ni faraja kubwa sana na ni maendeleo kwetu kwa sababu yanaweza kuongeza ajira katika sekta mbalimbali. Kwa hiyo nipongeze juhudi ambazo zinafanywa na Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie upande wa LNG; tunajua yanayoendelea Serikalini ya kukamilisha mazungumzo mpaka hapo mwaka 2023/2024. Naiomba sana Serikali katika eneo lile ambao inakwenda kutekeleza mradi LNG wapo wananchi ambao wanaishi pale na kwa kipindi kirefu sasa karibu miaka mitano walishaambiwa kwamba wasiweze kujiendeleza pale, kwa maana tumewambia maendeleo yao yakae likizo kwa muda fulani, naiomba sana Serikali yangu kwa kipindi karibu cha miaka mitatu mfululizo fedha inatengwa kwa ajili ya kuwapa fidia hao wananchi lakini fedha hiyo haitoki. Sasa ningependa wakati Waziri ana wind up aniambie ni kwa nini fedha hii haitoki kwenda kupewa fidia wananchi wale wa Kata ya Mbanja, Kijiji cha likong’o.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie upande huu wa madini, nimshukuru sana Waziri wa Madini na Naibu wake, kwa kweli walitoa ushirikiano katika kuhakikisha tozo mbalimbali kwa wazalishaji wa chumvi hasa wale wa Lindi ambao walikuja hapa Dodoma tukakaa nao pamoja na kuona baadhi ya tozo ziondolewe ili kuwafanya wazalishaji wa chumvi waweze kuingia katika ushindani wa masoko, lakini tuweze kuwa na viwanda vya chumvi nchini Tanzania. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Waziri, Mheshimiwa Dotto pamoja na Naibu wake, lakini hata wakati ule dada yangu Mheshimiwa Angella Kairuki alifanya kazi kubwa ya kutusaidia na hatimaye wananchi wale wanaendelea vizuri katika uzalishaji wa chumvi, lakini kuna Halmashauri ambayo

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hamida kengele ya pili imeshagonga, ahsante sana.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)