Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Lucy Thomas Mayenga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kutoa mchango wangu kwenye taarifa hii ya Kamati. Naomba kwa nafasi ya kipekee, kwanza kabisa nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akiifanya katika suala zima la kusimamia Sekta ya Madini hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kikao ambacho amekifanya tarehe 22 Januari, kwa uamuzi aliouchukua kuongea na wadau kusikiliza matatizo yao. Vile vile, tumeweza kuona kwamba Mheshimiwa Rais anaumia sana na suala zima la kutaka
wananchi wake tuwe na maisha mema, kiasi ambacho amekuwa akiingilia hata hizi sekta nyingine licha ya kwamba yeye ni Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi hizi ninazisema, lakini vile vile Mheshimiwa Rais wetu ni msikivu sana. Nilisimama hapa kwenye Bunge la mwezi Tisa, nikaomba kwamba Mheshimiwa Rais aweze kusaidia kuhamisha TIC kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara kwenda Ofisi ya Waziri Mkuu au Ofisi ya Rais na baada ya wiki moja alifanya hivyo. Namshukuru sana na ninampongeza sana, kwa sababu kwa uamuzi huo sasa ina maana tutakuwa tunaanza kuzungumza lugha moja kwenye masuala mazima ya uchumi na hasa kwa kutegemea kituo chetu cha uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa 31wa taarifa hii ya Kamati, inasema hivi, naomba kunukuu: “Hadi sasa mchango wa Sekta ya Madini ni asilimia 4.8.” Taarifa hii inasema kwamba, “Wizara ya Madini pamoja na Tume ya Madini inapaswa kuendelea na usimazi na udhibiti wa utoroshwaji wa madini yote nchini kwa kuimarisha ulinzi kwa maeneo yenye migodi mikubwa na ya kati.”

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe wazo langu na ushauri. Ninaomba Serikali, niseme wazi kwamba siyo Tume ya Madini wala siyo Wizara yenye uwezo wa kudhibiti utoroshwaji wa madini hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema namna hiyo? Kwa sababu biashara ya madini kwanza kabisa inafanana sana na madawa ya kulevywa. Nasema hivyo kwa sababu ni biashara ambayo inahusisha pesa nyingi sana; ni biashara ambayo crime yake huwa ni very organized kiasi ambacho Tume ya Madini au Wizara peke yake haitakuwa na uwezo wa kufanya control.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni nini? Naomba Serikali iweze kuunda Mamlaka ya Udhibiti wa utoroshwaji wa madini hapa Tanzania, pamoja na usimamizi wa kodi. Kwa sababu lazima tujiulize, hawa watu kwa nini wanatorosha madini? Maana kutorosha madini ni suala lingine na kuweza kuwadhibiti ni suala lingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye biashara hii ya madini, kuna kodi nyingi sana. Hizi kodi ndizo zinazofanya watu hawa waweze kutorosha. Kuna VAT, Withholding Tax, kuna vitu vingi, kuna Service Levy, kuna vitu vingi sana kama inspection fees na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na haya, mtu anaona akipata madini, kuliko aende Serikalini kulipa kodi zote hizo, bora kutorosha. Kwa binadamu yeyote kwenye suala linalohusu pesa, tutalaumiana, tutafukuzana, tutafanyiana kila aina ya vitu, lakini inabidi nasi, hasa Serikali, tuweze kubadilika jinsi ya kuweza ku-deal na watu wanaofanya biashara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbaya zaidi, yapo mambo ambayo tunafanya kama maamuzi lakini baadaye yanakuja kututokea puani. Suala la ku-declare dhahabu umeitoa wapi? Huu ni uamuzi ambao siyo wa busara. Naomba suala hili Serikali iweze kuangalia upya. Kwa sababu kama tunavyofahamu kule kwetu Shinyanga na maeneo mengine huko Usukumani, mtu amepata dhahabu yake, anakwenda Serikalini ili aweze kukadiriwa kodi. Akifika kule, anaanza kuhojiwa kwanza utueleze ulipoitoa hii dhahabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, huu utaratibu kwa kweli naomba Serikali iangalie upya, kwa sababu mtu huyu huyu akitoka hapo, akivuka border tu pale Sirari akapita Kenya, anaenda kuisajili kama dhahabu ambayo imetoka Kenya. Wenzetu wanamaliza hapa, wanakwenda kuuza nje kama vile dhahabu ambayo imetoka Kenya. Matokeo yake Tanzania kuna madini mengi sana, migodi mingi sana lakini ukiangalia takwimu za uuzaji wa dhahabu nje, zinasikitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nasisitiza sana uundwaji wa hii mamlaka. Ninafahamu kwamba mamlaka hii itafanya kazi kama ilivyo Mamlaka ya Udhibiti wa Madawa ya Kulevywa ili tuweze kupata mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, tuweze kuangalia mashine zetu (scanners) kwenye maeneo ya Airport, Bandarini na na kadhalika, zina uwezo kiasi gani? Watu wanatorosha madini. Hata juzi kuna mshiriki mmoja wa kile kikao cha Mheshimiwa Rais, aliweza kusema jinsi wanavyotorosha madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ku-declare interest, mimi nimekuwa Mjumbe wa Williamson Diamond for nine years, kwa hiyo, najua kinachofanyika. Ukichukua dhahabu ukafunga na hizi karatasi za sigara, ukaweka katikati sponge ya nusu inchi au ya inchi moja, hakuna mashine ina-detect.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa watu wamekuwa wakifanya hivi. Vile vile, lazima tuweze kuangalia kwamba kama watu hawa wanaweza kuwa na mbinu kama hizi, ingawa wengine taarifa zinapelekwa wanakamatwa: Je, Serikali inachukua hatua gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu Serikali kununua dhahabu. Naomba Serikali kabla haijafikia uamuzi wa kununua dhahabu, iweze kukaa chini na kupitia mfumo mzima, tangu mtu anavyoanza kuchimba dhahabu mpaka kufikia kwenye mauzo. Nasema hivyo kwa sababu wachimbaji wadogo, tujiulize, pesa wanatoa wapi? Watu hawa siyo mitaji yao, mitaji inatoka Uarabuni, India na kadhalika. Wanapokuja kupata fedha ndiyo wanaingiza kwenye biashara hii. Wakiingiza kwenye biashara hii hawawezi kuuza dhahabu Serikalini hata mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu watu hawa sasa hivi pesa zinaingia, ingawa tuna Sheria ya Money Laundering, ndiyo maana nimesema kwamba Serikali lazima ikae ijipange sana. Hata hii Mamlaka ya Kudhibiti Utoroshaji wa Madini naomba sana ihusishe vyombo vya ulinzi na usalama, ihusishe wataalam kwa maana ya Maprofesa na kadhalika, vile vile ihusishe wale ambao ni wachimbaji local kabisa, ili muunganiko wao huu, wale ambao ni wako kabisa, waweze kutoa experience wa kile ambacho wanakifanya on the ground. Tusikae kutegemea tu kwamba ni wataalam peke yao watakaa chini, wao watakuwa wanafanya experience ya makaratasi wakati on the ground mambo ni tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie pia airports zetu jinsi zilivyojengwa. Maofisi ya Maafisa katika airports zetu. Unaingia kwenye Ofisi ya Afisa wa Airport, una uwezo wa kutoka kwenye ndege ukapita kwenye Ofisi ya Afisa bila kupita kwenye scanner. Naomba Airport ya Mwanza iangaliwe na airport nyingine zote ziangaliwe. Hii ndiyo mianya ambayo inasababisha madini yetu yanatoroshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine Mheshimiwa Heche alikuwa analizungumzia hapa kwamba tunafaa kuongoza au hatufai, naomba kumwambia Mheshimiwa Heche, yeye mwenyewe anapumulia mashine, hali yake ni mbaya sana. Akae tu avumilie, milango tulishaifunga. Yeye mwenyewe alishakaa akasema anataka kurudi huku lakini mambo yamekuwa magumu. Asubiri ikifika mwakani, aende nyumbani kwake apumzike. Maana kuna watu wakikaa, kila siku Serikali haifanyi kazi, Serikali haifanyi hivi; Serikali inajitahidi, lakini ninyi wenyewe mkikaa, mna matatizo lukuki! Hayo matatizo yenu ambayo yanasababisha mpaka mnafikia hapo mlipo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)