Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ili kusudi niweze kuchangia katika hotuba za Kamati zetu mbili Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama pamoja na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini. Taifa lolote ulimwenguni linapimwa uwezo wake na nguvu zake kutokana na nguvu za kiuchumi na nguvu za kiulinzi na usalama. Vyombo vyetu vya ulinzi na usalama katika Taifa letu vimefanya kazi kubwa kwa uhakika na tunaendelea kupata heshima ndani na nje ya mipaka ya nchi yetu kutokana na uzalendo wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niiambie Serikali tu kwamba kuna jambo moja ambalo linajitokeza ambalo si jema sana la ugomvi baina ya vyombo vyetu vya ulinzi na usalama na wananchi hasa katika suala zima la ardhi. Migogoro ya ardhi imekuwa inatia doa amani yetu na kwa maana hiyo naishauri Serikali ichukue hatua za makusudi kuhakikisha kwamba maeneo yote ya Jeshi la Wananchi na Jeshi la Magereza na vyombo vingine vyote vya Ulinzi na Usalama ikiwemo Jeshi la Polisi ardhi zake zipimwe na zijulikane kabisa kwamba hairuhusiwi raia yoyote kusogea na kujenga karibu na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, imeonekana wazi kwamba vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama vimekuwa vikichukua maeneo makubwa muda mrefu lakini raia kutokana na kwamba tunazidi kuongezeka, tumeendelea kuwa tunasogea kwenye maeneo haya na kuchukua maeneo na hatimaye kuanzisha mizozo isiyokuwa na umuhimu. Kwa maana hiyo naiomba Serikali itenge pesa makusudi kabisa ili kusudi maeneo yetu vyombo vya Ulinzi na Usalama yapimwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusiana na beacon, ni alama ambazo zinaonyesha ramani yetu au mipaka yetu ikoje katika mustakabali wa usalama wa Taifa letu na kwa maana hiyo kwa sababu kuna beacon ni mbalimbali zimeng’olewa katika mipaka yetu na nchi jirani ambazo zinatuzunguka, basi ni jambo la muhimu kuhakikisha kwamba Serikali kupitia Wizara yetu ya Mambo ya Nchi za Nje pamoja na Wizara ya Ardhi wafanye jitihada kuhakikisha kwamba beacon zetu zinarejeshwa mahali ambapo zilikuwepo hapo mwanzo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala zima la diplomasia ya uchumi, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa jitihada ambazo ameendelea nazo za kufufua Shirika letu la ndege. Diplomasia ya uchumi isingewezekana kama kusingekuwa na jitahada mahususi za Mheshimiwa Rais wetu za kuhakikisha kwamba tunakuwa na Shirika la Ndege ambalo litakuwa linatuunganisha na Mataifa mengine ya nje. Kwa maana ya kwamba wawekezaji wanaotaka kuja kuwekeza nchini kwetu hata kama wangekuwa wanapatikana huko nje ingekuwa ni tatizo zaidi kuwafikisha katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata watalii vilevile wanaweza wakaja pamoja na kuhakikisha kwamba uchumi wa nchi yetu unaendelea kuimarika kutokana na kwamba mchango wa shirika hili utaendelea kuonekana. Niiombe sasa Wizara ya Fedha ihakikishe kwamba vyombo vyetu vya ulinzi na usalama muda wote vipatiwe pesa zake kwa wakati hasa katika masuala mazima ya miradi yake ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala zima la nishati na madini, niipongeze Wizara yetu ya Nishati kwa jitihada nzuri na za makusudi ambazo zimeendeelea kuonekana na hasa kwa jitihada kubwa ambazo Mheshimiwa Rais wetu ameendelea kuzionyesha na kwa kuthubutu kuhakikisha kwamba mradi mkubwa wa Stiegler’s gorge unaanza kutekelezwa mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata jana tumeshuhudia uendelezaji wa mradi wa Rusumo katika Mto Kagera mradi ambao utaendelea kutuletea huduma ya umeme wa megawati karibu 27 ambazo zitakuwa zinagawanywa katika Taifa na sisi tutanufaika kwa utaratibu huo. Kwa maana hiyo nchi yetu itakapokuwa inaendelea katika sera yake ya kukuza viwanda na kuwa Tanzania mpya ya viwanda ninaamini kwamba matarajio hayo tunaweza kuyafikia muda si mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama vimeendelea kuwa na mashirika yake ya uzalishaji mali ikiwemo Shirika la SUMA JKT na hata Magereza, Jeshi la Ulinzi na Usalama linayo Mashirika yake ya Mzinga na Nyumbu. Vyombo hivi vimekuwa vikifanya kazi zake nzuri na kwa maana hiyo naiomba Serikali kwa makusudi mazima ihakikishe kwamba inaviongezea nguvu kuhakikisha kwamba vinashiriki katika uzalishaji mali na kuweza kuchangia katika ukuzaji wa uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala zima linalohusiana na suala la vitambulisho vya Taifa. NIDA wamekuwa ni wakala wa kuzalisha hivi vitambulisha vya Taifa, lakini kimsingi wameshindwa kufikia malengo kutokana na kwamba wanapungukiwa pesa pamoja na vitendea kazi vingine zikiwemo mashine za kuzalisha hizo kadi za vitambulisho vya Taifa. Kwa maana hiyo naomba Serikali kwa makusudi mazima ijipange vizuri kuhakikisha kwamba NIDA wanawezeshwa ili kusudi waweze kuvitoa vitambulisho hivyo ambavyo ndio vitakuwa vinaonesha uraia halali wa Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tukiendelea kuiona kwamba nchi yetu inasonga mbele, tuwe katika utaratibu unaokubalika kwa kuhakikisha kwamba vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama vinakaa katika utaratibu unaokubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika Wizara ya Madini, kwanza niishauri tu kwamba katika kile kikao cha wadau cha tarehe 22 na tarehe 23 naomba Wizara iyatekeleze maazimio yote ambayo yaliazimiwa na kikao hicho cha wadau. Pendekezo lingine ninalotaka kulitoa kwa Serikali ni kuhakikisha kwamba Mataifa mengine yaliyoendelea yamekuwa yakishindana katika uzalishaji na kulimbikiza silaha za maangamizi. Naishauri Serikali yangu ya Tanzania yenyewe ijitahidi katika kuhakikisha kwamba tunalimbikiza vitu vya thamani ikiwemo dhahabu na Benki yetu Kuu ihakikishe kwamba inanunua dhahabu na kuiweka katika Hazina ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja ya Kamati zote mbili. Ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)