Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii muhimu. Kwanza naunga mkono asilimia 100 kwa sababu kupandisha hadhi mapori haya ni muhimu sana hasa kwa sisi tunaotoka Kagera. Tulikuwa tunapata wakati mgumu kupita kwenye mapori ya Biharamulo, hali ilikuwa mbaya lazima muwe na Polisi vinginevyo mlikuwa mnavamiwa. Baada ya kupandisha hadhi mapori haya tunaamini usalama utakuwepo na tutasafiri salama. Pia wale majangili ambao walikuwa kwenye yale mapori tunaamini hawatakuwepo tena na usalama utakuwa mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono pia kwa sababu mapori mawili ya Ibanda na Rumanyika yako Kyerwa. Mapori haya ni muhimu na yana wanyama ambao kwa kweli ni muhimu sana. Ninaamini Serikali baada ya kupandisha hadhi mapori haya sasa tutaenda kupata watalii na Serikali inaenda kuongeza kipato tutakapokuwa tumeweka mazingira mazuri.

Mheshimiwa Spika, baada ya kupandisha hadhi mapori haya tunatamani tuone wananchi wetu wanapata elimu ya kutosha ili wasiweze kuvamia tena mapori yale kwa sababu wengine walikuwa wanategemea kwenda kutafuta kuni na kadhalika. Kwa mfano, kule Kyerwa kwangu kuna miti inaitwa Emisambyia, ni miti muhimu sana na ni mirefu sana ikilindwa mazingira yetu yatakuwa mazuri. Nachoomba sana Serikali iendelee kutoa elimu ili wananchi wajue umuhimu wa kupandishwa hadhi mapori haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tunatamani waweke mazingira rafiki hata kwa watalii wanaokuja. Pawepo na barabara, mahoteli mazuri ili kuwavutia watalii kufika kwenye maeneo yale. Tunatamani hata wananchi ambao wanazunguka maeneo haya waweze kunufaika. Wananchi waone shule zinajengwa kupitia mapori haya na miundombinu mingine mizuri inaimarishwa ili wananchi waendelee kuiunga mkono Serikali na kuyalinda mapori haya kwa sababu tunajua wananchi wengi ndiyo wamezunguka mapori haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, mimi naiunga sana mkono Serikali kwa kupandisha hadhi mapori haya. Kule kwangu kuna Majimoto Mtagata, niwakaribishe sana Waheshimiwa Wabunge yale maji yanatoa moto na watu wengi wamekuwa wakienda pale wakiamini katika yale maji kupokea uponyaji. Tunawakaribisha sana Waheshimiwa Wabunge mfike Kyerwa, mjionee maajabu ya Mungu.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)