Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye hizi taarifa za Kamati mbili.

Mheshimiwa Spika, wakati ukimuagiza Mheshimiwa Lusinde apeleke invoice kwa Waziri wa Maliasili na mimi kwangu tembo wameingia lakini kwangu wamekula maembe. Kwa hiyo, nami nitapeleka invoice. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimepitia ripoti ya Kamati hii inayoshughulika na kilimo na naunga mkono mapendekezo yao mengi sana. Nitaomba tufanye maboresho maeneo machache lakini kwa kweli wamefanya kazi nzuri ya kuchambua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina mazao mengi, yako mazao yale ya biashara lakini yako mazao mchanganyiko. Hapa nataka nizungumzie suala la Bodi ya Nafaka ya Mazao Mchanganyiko. Tunazo Bodi kwenye mazao mengine mengi lakini hii ya mazao mchanganyiko ambayo of course sasa hivi inafanya kazi ya kusimamia ununuaji wa zao la korosho, kwa mujibu wa sheria imeandikwa hapa kwamba hii ni taasisi ya Serikali ambayo inajiendesha kibiashara.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana na mwaka juzi sisi ambao tuna wakulima wanalima mazao mchanganyiko na hasa sisi wa mbaazi tulipata matatizo kwa sababu tunadhani hii bodi haikutimiza wajibu wake sawasawa na ni kwa sababu ya ukosefu wa fedha kwamba hawakupewa fedha za kutosha. Kazi yao moja ni pamoja na kuyanunua haya mazao mchanganyiko kwa bei ya soko lakini kuyatafutia soko na hasa nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, Kamati imeonesha hapa moja ya changamoto kubwa ambayo imewapata wenzetu wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko ni kutopewa fedha. Ushauri wangu nadhani kwa kuwa, ni Bodi ambayo inaweza kujiendesha kibiashara badala ya kuendelea kutengewa fedha na Serikali kutoka kwenye Mfuko Mkuu, kwa nini Serikali isitengeneze utaratibu wa kuwadhamini Bodi ya Mazao Mchanganyiko wapate fedha kutoka kwenye taasisi za kifedha kwa maana ya kwamba wafanye kibiashara, wakakope, wanunue, wauze, Serikali iwe ni guarantor tu badala ya kupeleka fedha kule. Tuwa-guarantee, wapewe fedha na vyombo vya fedha wakanunue haya mazao wakatafute soko, wakulima wetu wangekuwa wako sawasawa kabisa na leo tungekuwa hatuzungumzi kabisa tatizo la mbaazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, habari nilizonazo waliomba fedha hawakupata, wakaomba kwenda kukopa kwa kupewa guarantee na Serikali nayo wakanyimwa, matokeo yake sasa wakabaki wako tu. Sasa wamebaki wako loose, tumeenda kuwachukua kuwapeleka kununua korosho, mimi nadhani siyo sawasawa. Tuwawezeshe, tuwadhamini, wakachukue fedha kwenye vyombo vya fedha kibiashara wafanye biashara kwa kuwa sheria inasema hivyo na mapendekezo ya Kamati hapa yanaonesha wakipewa fedha watafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili ni mapendekezo juu ya korosho. Kamati imechambua vizuri sana suala zima la korosho. Nami naamini tumejifunza mengi namna korosho ilivyoenda na bila shaka mafunzo yake yatatusaidia kuboresha namna ya kuendesha mazao yetu ya kibiashara nchini. Tumevuna tulichopanda lakini sasa tujifunze badala ya kuendelea kulaumiana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la utata wa takwimu ambazo zimekuwa zikitolewa na wenzetu wa Serikali. Kila mara Serikali imekuwa ikitoa takwimu mbalimbali juu ya zoezi zima la ununuzi wa korosho. Mimi nataka niwatahadharishe, takwimu nyingi mnazozisema Serikali ukienda kule chini ukweli unakataana. Mnachokisema mmelipa na hali halisi ilivyo, ukweli unapingana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sijui kama kuna sababu ya kuendelea kutoa takwimu. Takwimu hizi kila siku zinakua, nikienda Jimboni kwangu hali ya malipo bado mbaya lakini takwimu zinaonesha mambo yanakwenda, nadhani hili tulirekebishe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna mambo yametokea kwenye zoezi zima na hili nadhani kwa sababu ya kuchanganya. Tumei-suspend Bodi ya Korosho, tumeweka Bodi ya Mazao Mchanganyiko na Jeshi, kuna matendo ya dhuluma yamefanyika kwenye maeneo haya. Nashauri Serikali tufumbue macho, twende tuchunguze na tuchukue hatua, dhuluma haitakufa kama hatutachukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu katika korosho, zoezi la uhakiki bahati mbaya sana limeanza kutumika kama kichaka cha kulinda uzembe wa kupunguza kasi ya kulipa wakulima. Bahati mbaya limeanza muda mrefu siyo korosho tu kila mahali tukitaka kuchelewa kulipa tunasema tunafanya uhakiki ambao unachukua muda mrefu watu wanaumiaa inafika mwisho basi inapotea hewani hivi. Wasiwasi wangu uhakiki kwenye zao la korosho isipotelee hewani, uhakiki utupe matokeo, kama kuna korosho tumeamua kuitaifisha tuseme kiasi gani tumetaifisha na kwa nini tumetaifisha. Suala hili la uhakiki tukiweka wazi kila mtu atatuelewa na tutasonga mbele pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mtama nataka kuchukua nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais na hapa nataka tujifunze kidogo kuweka akiba ya maneno hasa tunaposhutumiana bila sababu. Mheshimiwa Rais wakati wa uchaguzi sisi Jimbo la Mtama tulipeleka maombi ya kufuta baadhi ya mashamba makubwa yaliyotelekezwa. Namshukuru Rais na Waziri wa Ardhi, moja ya shamba lililofutwa ni shamba Na. 37 lipo Maumbika – Mtama, Mkoa wa Lindi. Aliyelipeleka kuomba lifutwe ni mimi Mbunge, nilimpelekea Waziri, Waziri akapeleka kwa Rais, Rais akafuta. Nataka niwaombe wenzangu kwanza kwa niaba ya wakulima nimshukuru Waziri na Rais kwa kulifuta shamba hili kwa sababu sasa tutaenda kugawana vizuri. Kwa hiyo, wakati mwingine tunapolishwa maneno tukaanza kusema, tuweke akiba ya maneno juu ya nani anapinga nini, anasema nini, itatusaidia sana kama wanasiasa tukiwaweka akiba ya maneno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)