Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati kabisa na kwa niaba ya Kamati napenda niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao wamepata fursa ya kuchangia hoja ya Kamati ya Bajeti kutoka pande mbili zote za Bunge, nawashukuruni sana Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Aidha, pia napenda niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri ambao pia kwa namna fulani wamechangia lakini kwa kujaribu kufafanua baadhi ya maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge walihoji au wali- criticize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wajumbe waliozungumzia na kugusa ripoti ya Kamati ya Bajeti ni 17 na kwa sababu ya muda naomba nisiwataje majina yao. Hata hivyo si rahisi sana kwa muda nilionao kuweza kujibu hoja moja baada ya nyingine na kwa sababu hiyo nitajaribu kuchukua yale ya jumla jumla tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumziwa suala la ukuaji wa uchumi, lakini pia pongezi zimetolewa na wengine wame-criticize na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amejaribu kufafanua kwamba hakuna ubishi kwamba uchumi wetu unakua kwa kasi nzuri na kwa Afrika sisi ni miongoni mwa nchi tano yaani tupo kati ya kumi ambazo uchumi wake unakua kwa kasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo tunaweza tukajidharau lakini tunapojidharau katika mambo ya msingi yanayotupa heshima ni kama vile hatuitaki heshima. Kwa hiyo ni vizuri mimi niwasihi Waheshimiwa Wabunge kwenye mambo ambayo kama Taifa tunafanya vizuri ni vizuri tukasema tunafanya vizuri, lakini tukaboresha kwa maneno mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa hapa jambo la misaada na mikopo na msemaji aliyesema na wengine wamesema, lakini nimtaje Mheshimiwa Msigwa ambaye amesema bajeti yetu inategemea asilimia 40 kutoka kwenye misaada na mikopo, sijui hizi takwimu zinatoka wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikusihi Bunge lako liangalie matumizi ya takwimu ndani ya Bunge, kwa sababu sisi ni viongozi lakini Bunge hili limejaa wasomi watupu. Matumizi ya takwimu yaangaliwe, tusitajetaje tu na kuzungumza zaungumza tu. Ni vizuri tukazisema za kweli na
zilizopo kwa sababu takwimu ni tafiti na kama hujafanya utafiti huna haki ya kuzungumza. Sasa kama unatumia takwimu zisizo halali maana yake hukuwa na haki wala usahihi wa kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bajeti ya mwaka 2018/ 2019 mchango wa misaada na mikopo tulioutegemea kwa bajeti ya mwaka 2017/2018 fedha zenyewe tulizozihitaji ni trilioni 2.13 ambayo kwa bajeti yetu ya trilioni 32.475 kiwango hiki cha misaada na mikopo tulichokihitaji ni asilimia 6.55 tu. Kwa bajeti ya mwaka 2019/2020 ambayo tunaindaa sasa na tupo katika mchakato, kiwango tunachokihitaji kutoka kwenye misaada na mikopo its only 3.38 trilioni ambapo bajeti yake inatarajiwa kuwa trilioni 33.5; kiwango hiki ni sawasawa na asilimia 10.005. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake kama Taifa tumebadilika, hiyo asilimia 40 ilikuwa ni zamani sana, tunakwenda kwenye kujitegemea na kwa hiyo kuzungumzia suala la misaada na mikopo kama ndio mwarubaini wa kuondoka kwenye umaskini wa nchi yetu sio sahihi ni kujidhalilisha kwa sababu tumejenga uwezo wa kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa suala la kama vile nchi kama nchi tunadharau, hatuheshimu, hatuthamini private sector katika kujenga uchumi. Hakuna nchi duniani ambayo leo hii inaweza kujenga uchumi wake bila private sector na Tanzania tunaheshimu sana private sector na ndio maana Serikali imetengeneza blue print, tumeripoti kwenye taarifa yetu. Serikali imeleta hapa sheria ambayo tumeifanyia kazi na kwenye ripoti ya Kamati imeelezea kwenye ukurasa wa 9 na 10. Kwenye ripoti ya Kamati tumeelezea kwamba tumetengeneza Sheria ya PPP, PPP maana yake ni nini, ni Public Private Partnership.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumeelezea kwamba pia Serikali imeongeza diplomasia ya uchumi, mabalozi wote wameagizwa kwa ajili ya kuhamsisha wawekezaji mbalimbali kuingia nchini. Hata hivyo mafanikio yamejionesha na kwenye ripoti yetu tumesema kwenye ukurasa wa 10 kwamba hata kwa kipindi hiki kifupi cha mwaka huu tu viwanda vitano vya dawa vinajengwa, kwenye ripoti yetu tumeonesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inaposemekana kama Serikali au nchi yetu hatuthamini wawekezaji mimi nashangaa na hii taarifa mmeitoa wapi kwa sababu kwenye ripoti yangu niliyoleta nimesema na namna tulivyofanya na Serikali ambavyo inafanya. Mimi nadhani mambo mengine tuyaseme lakini tuwe na kiasi katika kuyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji mmoja mmoja wamesema na wamechangia mambo mengi ya msingi ambayo Serikali imeyachukua na sisi kamati tumeyasema kwenye taarifa yetu. yale ambayo Waheshimiwa Wabunge wame-criticize ni vizuri Serikali nayo ikayachukua; lakini unapo-criticize kwa jambo ambalo si sahihi, kwa mfano nimpongeze Mheshimiwa Silinde mara ya pili aliposimama kutoa taarifa amefafanua vizuri sasa kwamba fedha ya maji aliyokuwa anaisema si ya Mfuko wa Maji peke yake, ya Mfuko wa Maji yote ilipelekwa kama ilivyo isipokuwa Serikali haijapeleka fedha ya maendeleo kutoka Hazina. Kwa hiyo Mheshimiwa Silinde umefanya vizuri lakini mwanzo ulizungumza kwa ujumla kwamba hakujapelekwa fedha ya maendeleo ya maji. Kwa hiyo, kwa taarifa yetu umetutendea haki maana tulianza kushangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengine ambayo yamechangiwa sana na mimi niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge ni juu ya Serikali kuwa makini na ahadi ilizoziahidi na utekelezaji wake. Yapo yale maeneo ambayo Serikali tunakubaliana kabisa kwenye kamati, rai yangu kwa Serikali ni kwamba muhakikishe kwamba mnayatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, eneo la maboma ambayo tulikubaliana kwenye afya mmepeleka fedha vizuri lakini kwenye eneo la elimu hamjapeleka fedha vizuri kama tulivyokubaliana. Kwa hiyo, kwenye hili na Waheshimiwa Wajumbe wengi niwapongeze mmelisemea na Serikali wamesikia.

MHE. HALIMA J. MDEE: (Hapa alizungumza bila kutumia kipaza sauti).

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI: Tatizo lenu mnajua ku-criticize ndio kusema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Msigwa amelinganisha ukuaji wa uchumi na hali ya utoaji wa huduma. Huduma hizi haziwezi kuimarika kama misingi muhimu kama ambavyo Mheshimiwa Dkt. Mpango amezungumza, lakini kama pia alivyozungumza mjumbe wangu wa Kamati, Balozi. Amesema kwamba ni lazima tuimarishe kujenga ukubwa wa uchumi. Tunaweza tukawa na uchumi unaokuwa lakini uchumi huo ukawa mdogo, we have to strengthen the economy, so how do we strengthen the economy ni kuhakikisha kwamba miundombinu muhimu inayojenga uchumi inashughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kunahitaji maamuzi ya makusudi kujenga reli, ukijenga reli uchumi wako lazima utaimarika. Tukiwa na umeme wa kutosha kama tunavyojenga Stiegler’s Gorge ni maamuzi ambayo unayafanya leo lakini yatautunza uchumi kwa muda mrefu. Kama tunavyojenga miundombinu ya barabara, kama tunavyojenga miundombinu na kuhakikisha kwamba watoto wetu wanasoma vizuri; una-invest kwa watu, huko ndiko kuimarisha uchumi utakaokuwa na uimara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Serikali iangalie pia namna ya kuimarisha katika eneo la ICT. Duniani sasa na nchi matajiri duniani wame-invest zaidi kwenye ICT na makampuni matajiri sana duniani ni wale wanaofanya biashara ya ICT. Kama Taifa ni vizuri na sisi tukaona tu-invest zaidi katika eneo hili kwa sababu hili eneo nalo tukifanya masihara nalo lina connection kubwa na uchumi wa kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tuna Mkongo wa Taifa ambao Serikali imewekeza hela nyingi sana, lakini utasikia internet low, malipo yanachelewa, efficiency inapungua. Sasa kwa nini tuwekeze fedha nyingi halafu tusipate faida ya jambo hilo? (Makofi)

Kwa hiyo rai yangu kwa Serikali ni kwamba ICT area ni muhimu sana iwe kwenye perfection na iwe kwenye precision kwa sababu bila kuwa na uhalisi na usahihi hatuwezi kupata tija na payback ya uwekezaji tulioufanya. Sasa tatizo hapa tatizo ni nini ni watu, software ama ni hardware? Hapa kama taifa tujaribu kutoka na wale ambao wanajua katika eneo hili wasitubabaishe zaidi tusiojua. Mimi naamini kama Serikali ime-invest lazima itulipe na malipo yake ni sasa wakati dunia inaishi kwenye maisha ya ICT. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu michango ilikuwa mingi lakini kwa sababu ya muda nipende kurudia tena kuwashukuru wote kabisa ambao mmechangia maoni ya kamati yetu. Sisi kama kamati tunapongeza sana aina ya michango iliyotolewa inaweza ikawa mingine ilikuwa inakwenda kinyume lakini ukinyume huo ndio unaohitajika ili kufanya tufikiri zaidi. Kwa hiyo kimsingi yote yanahitajika katika muktadha wa kuchambua unachokifanya hasa katika utekelezaji wa bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya kwa niaba ya Kamati ya Bajeti naomba kutoa hoja.

MHE. ALBERT O. NTABALIBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.