Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Mimi labda nianze kwa kusema machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, sisi kama nchi lazima tufikirie kujitegemea zaidi hapa ndani kwetu kuliko kutegemea watu wengine. Wakati wa kuanza kufikiria kujitegemea ni wakati huu. Sasa kama fikra zetu bado zitaendelea kudhani kwamba kuna mtu atatusaidia ili kama nchi tuweze kusonga mbele kimaendeleo mawazo hayo hayapo kwa ulimwengu wa sasa. Kwa sababu hata waliokuwa wakitusaidia na kutuonea huruma zamani mazingira yao yamebadilika sana. Yamebadilika kwa kiasi kikubwa na wao wakati huu wanaanza kufikiria nani atawasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu kwamba lazima tuanze kuwaza kujitegemea wenyewe badala ya kufikiria kwamba kuna mtu atatusaidia kututoa hapa tulipo. Ukisikiliza mazungumzo yanayosemwa bado tunafikiri sana kwamba labda tuko miaka ya 1970, miaka ya 1980, wakati ambapo tulikuwa tunalelewa tu mpaka asilimia 60 ya bajeti zetu zilikuwa zinategemea misaada. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nakumbuka wakati Mzee Mwinyi anachukua madaraka nchi ilikuwa kwenye hali isiyo nzuri, mbaya. Mzee Mwinyi alitoa hotuba wakati fulani akasema, baada ya kupata urais nimekuta kwenye chungu cha Hazina hakuna kitu. Sasa nimejaribu kutembea Ujerumani, Marekani na nchi mbalimbali kote huko wananiambia nenda kakubaliane na IMF au World Bank.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaweza kuona ni kwa namna gani ikiwa unataka kusaidiwa kila wakati masharti utakayoongezewa, utakayopewa ili uyatimize kupata huo msaada ni masharti ya namna gani. Sasa katika dunia ya leo masharti yameongezeka zaidi, zaidi ya kukubaliana na World Bank, zaidi ya kukubaliana na IMF, kuna masharti mengine ambayo hayaruhusu kabisa tabia, mienendo na tamaduni za Kitanzania. Sasa tukiendelea kufikiria kwamba lazima tu tusaidiwe ili tutoke hapa tulipo basi mimi nachelea kusema inawezekana tukaamua kuuza uhuru wetu, uhuru unaotunza utamaduni wetu, uhuru unaotunza mienendo na desturi na mila zetu, tukauza ili tupate hiyo misaada. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, misaada tunaihitaji, lakini iwe katika misingi ile inayokubalika katika utamaduni na mila zetu, ndiyo maana hata kwenye kipindi tunachokijadili, kwenye taarifa hii, bado kuna misaada tuliyopata kutoka kwa wasamaria wema, misaada ambayo haikuambatana na masharti ambayo ni hasi kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ukurasa wa 29 wa taarifa ya Kamati ya Bajeti tulitarajia tungeweza kupata misaada ya trilioni 2.6, lakini tulipata bilioni 878. Mimi niseme kama tulipata misaada ya namna hii basi ndiyo misaada iliyokuwa haina masharti ya kutufanya tuuze uhuru wetu, tulipata, si kwamba hatukupata kabisa kama wenzetu wanavyoweza kusema. Misaada tunapata, lakini ni ile ambayo wanakubaliana na masharti yetu sisi pia, sio tu tuuze kila kitu, tukubali kila kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu habari ya mikopo hiyo kila mtu anakopa. Mtu binafsi anakopa, nchi inakopa na unakopa kwa kulinganisha na hali yako ya kulipa. Sasa ukiona hali yako ya kulipa haiendi sawasawa basi unakwepa huo mkopo kwa hiyo, kama nchi kwa kweli, lazima tufikirie kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niseme tu kwamba ninamuunga mkono sana Mheshimiwa Rais anaposema tujitegemee, lazima Watanzania tuamue kujitegemea. Anasema tutaumia kidogo, lakini tutakwenda. Kwa hiyo, ni lazima tukubali na sisi ndani ya Bunge lako ndio watu wanao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa…

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja, ahsante sana.