Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JUSTIN M. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda nimshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa mpango huu ambao ametuletea hapa Bungeni ili sisi nasi tuweze kuupitia na kutoa mapendekezo na maoni yetu. Wamefanya kazi kubwa na tunaanza kuona kwamba upo mwanga mkubwa wa kuweza kutekeleza miradi mingi ambayo tumeikusudia na ambayo ipo katika mpango wa miaka mitano wa 2016-2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la ukusanyaji wa mapato. Katika taarifa tulizozipata na za kiutendaji katika mwaka wa fedha 2016/2017 na 2017/2018 zinaonyesha kwa kiasi fulani tumeshindwa kufikia malengo ya ukusanyaji wa mapato. Pamoja na kwamba TRA wamefanya kazi kubwa lakini tumeshindwa kufikia malengo ya ukusanyaji wa mapato na hatimaye mipango au miradi ya maendeleo mingine imeshindwa kufikia asilimia 100 kwa namna tulivyokuwa tumepanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe na nishauri, zipo changamoto ambazo Mheshimiwa Waziri amezitaja, nami nataka nijikite katika baadhi ya changamoto hizo ili kusudi tuweze kuona namna gani ambavyo tunaweza tukapata mapato au kubadilisha mbinu za ukusanyaji wa mapato na kuweka miradi mingine ambayo pia inaweza ikatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ambalo limeelezwa hapa ni ugumu wa ukusanyaji. Tunao ugumu wa ukusanyaji wa mapato kwa sababu ya uwepo wa sekta isiyo rasmi ambapo tunaishindwa kukusanya mapato yake. Nakubaliana na changamoto hii na wewe mwenyewe ni shahidi, mimi natoka Mkoa wa Singida na wewe hapa Dodoma sisi ni wakulima wa alizeti. Tunazo biashara nyingi sana ambazo zinafanyika kwenye barabara. Wakulima wanakwenda wanakamua alizeti, wanaweka kwenye madumu, wanafanya kazi ya kusubiri wanunuzi kwenye barabara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili likiwekewa utaratibu mzuri tunaweza kabisa tukapunguza ukubwa wa tatizo hili la biashara zisizo rasmi. Mfano tunatumia fedha nyingi sana katika kuingiza mafuta ya kula kutoka nje na sisi ni wazalishaji wazuri wa mbegu za mafuta yakiwemo ya alizeti. Ni kwa nini katika mpango huu tusipunguze kiasi cha fedha za ununuzi wa mafuta na tukawekeza katika ununuzi wa mashine za kufanyia double refining ili kuongeza thamani na ubora wa mafuta yetu tukaweza kuuza kwenye masoko ya ndani na masoko ya nje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezo wa kukusanya mafuta yote ambayo yanauzwa barabarani na wananchi upo tukiwa na viwanda vya kutosha vya double refining. Tukifanya hivyo tutakuwa tumewatafutia wakulima wetu masoko yenye uhakika maana watakuwa hawana sababu tena ya kusubiri barabarani, wanaweza wakapata masoko kule kule wanakokamua alizeti na viwanda vya double refining vikachukua mafuta yale kwa ajili ya kwenda kuyachakata kwa mara ya pili na yaweze kwenda kwenye masoko ya ndani na nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivyo, tutakuwa pia tumepunguza changamoto hiyo ambayo imeelezwa katika kipengele cha sita, changamoto ya masoko na bei ndogo za mazao. Wakulima wetu hawa wanapokuwa wanafanya biashara zisizo rasmi wanapoteza muda mwingi. Walioko barabarani walipaswa wauze yale mafuta na waende wakafanye shughuli nyingine badala yake wamekaa wakisubiri na mafuta yanaweza yakakaa kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo changamoto ambayo imeelezwa iliyopunguza mapato yetu, nayo ni kukosekana kwa ajira. Pamoja na juhudi kubwa ambazo Serikali yetu imefanya za kuongeza ajira lakini bado tunao upungufu mkubwa sana wa ajira katika maeneo yetu. Nitatolea mfano katika Halmashauri yangu ya Singida DC, kwenye sekta ya kilimo peke yake tunao watumishi 23 kati ya 105, kwa hiyo, tuna upungufu wa watumishi 88, sekta ya elimu ya msingi tuna watumishi 831 kati ya 1,629, sekta ya mifugo, watumishi 23 kati ya 84 na sekta nyingine nyingi, tunahitaji walimu wa sayansi 70 katika halmashauri pale, kwa hiyo, utaona zipo nafasi nyingi za ajira. Niiombe sana Serikali itenge fedha kwa ajili ya kuajiri kwenye maeneo haya ambayo yana upungufu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona madhara yake, kwa mfano kwenye sekta ya elimu. Mkoa wa Singida ni moja ya Mikoa ambayo haijafanya vizuri sana kwenye sekta ya elimu lakini tuna upungufu mkubwa wa walimu kama nilivyowaeleza na walimu wengine wanafundisha madarasa zaidi ya wanafunzi 100 hata wengine kufikia 150. Katika hali hii hatuwezi tukatoa elimu iliyo bora na elimu itakayotosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji katika sekta ya kilimo unahitaji kuongezwa. Sekta ya kilimo ndiyo inayochangia sana katika uchumi wa wananchi wadogo. Serikali hii ya Awamu ya Tano ndiyo imejipambanua kuwa Serikali ya wanyonge ambao zaidi wako vijijini. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali, nimuombe sana Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, utakapokuja na mpango tungetarajia tuone asilimia ngapi ya bajeti ambayo itakuwa imetengwa kwenda kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi tumekuwa tukiomba kufikia asilimia 10 ya bajeti nzima lakini hapa sasa tunaona bajeti ya maendeleo kwa asilimia 37 lakini tungependa tuone sekta ya kilimo, uvuvi na mifugo imetengewa asilimia ngapi. Tumeomba kwa muda mrefu, Mheshimiwa Dkt. Mpango najua wewe ni msikivu, muende mkafanye utaratibu ili kusudi tuweze kugusa maisha ya wananchi walio wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama cha Mapinduzi ilisema, tuna umasikini wa asilimia 28.2, kwa hiyo, tunayo kazi kubwa ya kufanya. Bila kugusa sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi hatuwezi kugusa kundi hili kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa miradi ya maji, zipo takwimu zimeonyeshwa hapa, viko vituo vingi ambavyo vimeongezeka na mimi niipongeze sana Serikali kwa kuongeza vituo vingi lakini mashaka yangu makubwa ni katika idadi ya wanufaika ambayo imeelezwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Dkt. Mpango kwenye ukurasa wa 31. Inawezekana katika visima mabavyo tumechimba hasa
vijijini, unaweza ukachimba kisima kimoja, visima viwili, visima vile kama tunaweza tukachukulia kwamba ndiyo vinatoa maji safi na salama kwa kijiji kizima tutakuwa tumefanya makosa makubwa sana. Tunataka tuone ni kwa kiasi gani tumetekeleza Ilani ya CCM ya kuweza kusogeza huduma za maji karibu na wananchi angalau kwa mita 400. Basi utakapokuja Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango tuone tumetekeleza Ilani kwa kiasi gani katika eneo hili la miradi ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika sekta ya elimu. Wananchi wetu wamejitahidi kwa muda mrefu zaidi ya miaka mitano katika kujenga miundombinu ya elimu ikiwa ni pamoja na madarasa, nyumba za walimu na maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali tufanye juhudi za makusudi kukamilisha miradi hii ya wananchi ambayo imekwishakuanza na kuwatia moyo wananchi wetu waendelee kuchangia kwenye miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kuchangia uliyonipa.