Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili niweze kutoa mchango wangu jioni hii ya leo, nikimshukuru Mungu kwa kuniweka niweze kutoa maoni. Awali ya yote, napenda nipongeze Wizara kwa kutuletea mpango mzuri ambao umeambana na utekelezaji wa shughuli za maendeleo uliotekelezwa kwa vipindi vilivyoainishwa katika kitabu cha mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango utajielekeza kwa kupongeza Serikali kwa kazi ilizozifanya kwa kuwa tumeletewa utekelezaji wa miradi ya maendeleo pia na kutoa ushauri katika Mapendekezo ya Mpango kwa mwaka wa fedha 2019/2020. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais na kumshukuru kwa ziara aliyoifanya Mkoani Simiyu mapema mwezi Septemba ambapo alifungua Hospitali ya Mkoa ya Rufaa. Kufunguliwa kwa Hospitali ya Mkoa katika Mkoa wa Simiyu kutaenda kuwapunguzia wananchi kutembea umbali kwenda Hospitali ya Rufaa ya Bugando pamoja na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyango ambapo kulikuwa kuna umbali wa kilometa 140. Kwa kufanya hivyo pia tutaweza kunusuru vifo ambavyo vilitokana na kusafirishwa kwa mgonjwa na kufariki kabla ya kupatiwa hata huduma wakati wa kufika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais akiwa Mkoani Simiyu alizindua vituo vya afya, maabara pamoja na wodi 39 na aliweka jiwe la msingi katika Daraja la Mto Sibiti na utekelezaji wa daraja hilo uko kwa asilimia 79.8. Daraja hilo litakapokamilika litakuwa lina manufaa kiuchumi katika Mkoa wa Simiyu na mikoa mingine ya jirani kwa sababu itasaidia bei ya vifaa vya ujenzi kupungua. Kwa mfano, cement katika Mkoa wetu inauzwa kwa Sh.18,500 kutokana na gharama kubwa ya usafirishaji. Cement mpaka ikafike mkoa huo inazungukia Mkoa wa Shinyanga ndiyo irudi kuingia katika Mkoa wa Simiyu. Kwa hiyo, kuna manufaa ya kiuchumi kuwepo kwa Daraja la Sibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi walikuwa wakisafiri kwenda Dar es Salaam kwa muda wa siku mbili. Walisafiri mpaka Shinyanga na kulala Shinyanga na kuanza safari ya kwenda Dar es Salaam. Kwa hiyo, kuwepo kwa daraja hilo kutasaidia wananchi kusafiri kwa muda mfupi na kuokoa fedha zao ambazo wangezitumia katika usafiri wa siku mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijikita katika mpango, naomba nishukuru Serikali kwa ujenzi wa reli kwa kiwango cha Standard Gauge. Wakati Kambi Rasmi ya Upinzani ikiwasilisha hotuba yake ilisema kwamba Standard Gauge haitakuwa na manufaa kwa sababu muda mwingi itasafirisha abiria, siyo kweli, yapo manufaa ya kiuchumi kwa kutumia reli hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Standard Gauge ina manufaa katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa pamoja na Magharibi. Tukumbuke kwamba Kanda ya Ziwa pamoja na Mikoa ya Magharibi haina viwanda vya cement. Kuwepo kwa Standard Gauge kutasaidia kuokoa gharama ya usafirishaji wa saruji. Kwa mfano, saruji kutoka Pwani pamoja na Mbeya kwa malori ingesafirishwa kwa gharama kubwa lakini kuwepo kwa Standard Gauge tutaweza kuokoa Sh.5,000, kwahiyo bei ya saruji pamoja na vifaa vingine vya ujenzi itapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanda ya Ziwa inazalisha pamba ya kutosha, marobota yanasafirishwa Dar es Salaam kwa kutumia magari. Kuwepo kwa reli hiyo marobota ya pamba yatasafirishwa kutoka Kanda ya Ziwa kwa gharama ndogo. Wafugaji watasafirisha ng’ombe zao kwenda Dar es Salaam na mikoa mingine kwa kutumia reli hiyo, kwa hiyo, tutaokoa gharama za usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia itatumika kupeleka na kutoa mizigo katika nchi jirani ya Rwanda. Kwa hiyo, wanaobeza kwamba Standard Gauge haina manufaa ya kiuchumi, manufaa ya kiuchumi yapo. Nashauri sasa katika mpango waweke fedha ya kutosha kwa ajili ya usanifu wa mazingira ambapo mradi huo utapitia ikiwemo pia ulipaji wa fidia. Serikali ifanye juhudi ya kumpata mwekezaji kwa ajili ya kujenga kipande cha Isaka-Rusumo. Kanda ya Ziwa inategemea bandari ya nchi kavu iliyopo Isaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia niishukuru Serikali ndani ya miaka mitatu imeweza kuongeza bajeti ya dawa kutoka shilingi bilioni 31 mpaka shilingi bilioni 269. Hii hatua ni kubwa sana, imeweza kusaidia upatikanaji wa dawa ambao siyo chini ya asilimia 80. Wauzaji wa dawa binafasi wanalalamika biashara yao imekuwa mbaya, hii ni kwa sababu kuna dawa za kutosha katika hospitali zetu. Serikali imewasaidia wananchi kuwapunguzia gharama za kununua dawa katika hospitali na pharmacy za watu binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mazuri yanayofanywa na Wizara ya Afya kuna changamoto katika kutoa huduma kwa wazee. Wazee wetu wanapewa huduma kwa kupewa vitambulisho lakini ikumbukwe kwamba vitambulisho hivyo vinatolewa ndani ya Wilaya. Wazee wetu wanapopata rufaa vitambulisho vile havikubaliwi. Nashauri kuwepo na mpango wa kuweka fedha kwa ajili ya kuwakatia bima ya afya sambamba na kupatiwa dawa muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazee wetu hawa wanaugua magonjwa ya moyo, sukari ikiwemo saratani, ni dhahiri kwamba magonjwa haya mengine hayatibiwi katika hospitali za Wilaya. Kwa hiyo, wazee wanayo changamoto ya kutokuwa na fedha ya kutosha kwa ajili ya kwenda kutibiwa nje kwa sababu vibali vile havikubaliki. Kwa hiyo, nashauri kuwepo na bima ya afya kwani itasaidia kuwepo na mzunguko wa fedha katika Hospitali za Wilaya. Wazee wetu wanatibiwa bure na Serikali kwa sasa hivi haifanyi marejesho ya fedha walizotibiwa wazee. Nashauri wazee hawa wapatiwe bima ya afya ambayo itazisaidia hospitali zetu kuwepo na mzunguko wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja mkono, nashukuru sana.