Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kabla sijachangia naomba niwashukuru sana wananchi wa Sikonge kwa kuniamini kuwa Mbunge wao kwa mara ya kwanza. Naomba niwatoe wasi wasi, wasiwe na wasiwasi wowote hapa kazi tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaingia katika hotuba, naomba nieleze kwamba nikiwa Mbunge nilifadhaika sana siku Mheshimiwa Rais alipotoa hotuba yake. Wakati Mheshimiwa Rais anaingia humu ndani, zilizuka fujo ambazo zilinifanya ninyong‟onyee kwa muda, nikishangaa
kwa sababu sikutegemea hadi wenzetu wakatoka wakisusia, hawakutaka kumsikiliza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini leo...
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Leo nimefarijika kuona badala ya kumsikiliza siku ile Mheshimiwa Rais, leo wenzetu wamesoma vizuri hotuba yake na wakisimama wanamsifu bila vurugu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ustaarabu huu uliooneshwa leo Watanzania wanauona na sisi Wabunge wote kwa ujumla naomba tuuzingatie ustaarabu huu siku zote, ili kama kuna hoja ijibiwe kwa hoja badala ya vurugu ambazo zinatufanya sisi wote tupoteze heshima yetu nje ya
Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nije kwenye hotuba. Kiwango cha commitment kilichooneshwa na Mheshimiwa Rais katika hotuba yake ni cha hali ya juu sana. Ni kiongozi ambaye yuko tayari kwa kauli na vitendo kupambana na vikwazo vyote ambavyo kwa muda mrefu vimekua vikimsababishia Mtanzania kero nyingi katika juhudi za kujikwamua kutoka kwenye umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, matumaini ya sasa ya Watanzania ikiwemo Wanasikonge ni makubwa mno, kwamba, baada ya miaka 10 ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli akiwa Rais uwezekano wa kufikia malengo ya Dira ya Maen deleo ya Taifa ifikapo mwaka 2025 si wa kutilia
shaka tena, kinachotakiwa kila mtu kutimiza wajibu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Rais ya tarehe 20/11/2015 na utendaji wake wa Rais na Serikali yake hadi sasa, umeongeza matarajio ya wananchi kuhusu kufanikiwa katika mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi, kuboresha ukusanyaji wa mapato ya Serikali, kudhibiti
matumizi, kuimarisha uadilifu, uaminifu na uzalendo na vyote hivi vinaashiria matokeo makubwa katika kupunguza umaskini. Ili tufanikiwe katika yote hayo, yale majipu ambayo Mheshimiwa Rais aliyaahidi kuyatumbua, majipu makubwa, majipu madogo na hata vijipu uchungu, vyote lazima vitumbuliwe bila kuona huruma. Mheshimiwa Rais ameahidi na tayari utekelezaji unaendelea, tunamshukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Sikonge walifurahishwa sana na hotuba ya Rais na wamekaa mkao wa hapa kazi tu, wanatimiza majukumu yao hususani katika sekta ya kilimo kwa kulima sana mashamba ya tumbaku na mazao ya chakula, kutengeneza mizinga kwa ajili
ya asali na nta na kutumia fursa nyingine zozote zilizopo kupambana na umaskini.
Wanakumbuka ahadi nzuri zinazojenga matumaini za Mheshimiwa Rais kwamba Serikali itawaboreshea zaidi mazingira ya kufaidika na jasho lao.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ambayo ningependa kukumbusha kwa sababu yako katika hotuba ya Mheshimiwa Rais, la kwanza, linalohusu eneo langu, kuondoa kero kwenye zao la tumbaku kwa kumwezesha mkulima apate pembejeo kwa urahisi na kwa muda muafaka
na kwa bei nafuu kwa kutumia mfumo rahisi ambapo mkulima kupitia Chama chake cha Msingi, akae kitako na mnunuzi ili waingie mktaba wa mnunuzi kukopeshwa pembejeo au pembejeo zitolewe kwa mkulima wakati wa msimu wa malipo kabla kilimo hakijaanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia mfumo wa malipo uboreshwe kuondoa malipo kuchelewa kwa zaidi ya miezi mitatu na Serikali imlinde mkulima asiibiwe wakati wa kubadilisha viwango vya fedha kutoka kwenye dola ya Kimarekani kwenda kwenye shilingi ya Kitanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kilimo kuna mambo mengi sana ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi. Watu wa Ushirika wanahitaji kuwasaidia wakulima katika maeneo mengi, COASCO ambao ni auditors wa ushirika ni tatizo kubwa, wamekuwa siyo wa kweli, ni bora tu
kuwaondoa ili mfumo wa ukaguzi ubaki chini ya ukaguzi wa ndani wa Halmashauri na CAG, hili litatusaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mengi mno kwenye kilimo yatazungumzwa na wengine, naomba wakulima waonewe huruma, wasaidiwe na Serikali pamoja na wadau kuondokana na adha wanazozipata.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa nilizungumzie ni kuboresha uhusiano kati ya wananchi na maeneo ya hifadhi, kwa mfano, mfugaji wa nyuki ni rafiki mkubwa sana wa misitu kwa sababu yeye anategemea kuweka mizinga yake kwenye misitu, kwa nini mfuga nyuki aonekane adui kwenye hifadhi eti tu kwa sababu tu anatumia mzinga wa gome la mti! Kwa nini Serikali isitoe elimu na huu ni ushauri kwa wafuga nyuki, ili watumie mizinga ya kisasa itakayofanya hatimaye wawe na uhuru wa kuingia hifadhini kwa sababu watakuwa
wamesajiliwa, hata wavuvi wadogo wadogo nao wanahitaji kusaidiwa kwa elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo napenda kuzungumzia kama kukumbusha kwa sababu liko kwenye hotuba, ni miundombinu. Barabara za lami na sisi tunahitaji kuunganishwa na Mikoa mingine kama Tabora - Katavi, Tabora – Mbeya - Singida, Tabora – Kigoma, kuboresha reli ya kati, miradi ya umeme vijijini na mitandao ya simu. Wilaya yangu ya Sikonge karibu 70% ya maeneo ya makazi hayajaunganishwa na mitandao ya simu. Ni muhimu sana kwenye awamu hii suala la mtandao lishughulikiwe kwa jicho kamilifu. Naomba maeneo yote yaliyo nyuma kwa miundombinu yapewe kipaumbele na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine Serikali iendelee kuwekeza kwenye elimu. Katika Wilaya yangu kuna maeneo 49 ambayo yanahitaji shule mpya kabisa za msingi. Katika maeneo 19 wananchi wamejenga madarasa, Halmashauri haina fedha za kukamilisha, kwa hiyo, Serikali
Kuu bado tunaomba iendelee kuwekeza kwenye elimu ya msingi, siyo kwamba MMEM ilikwisha, basi hakuna uwekezaji mpya unao endelea, tunaomba tuendelee kuwekeza kwenye elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye afya tuna upungufu mkubwa sana wa zahanati, watumishi na dawa, vyote viendelee kuwa katika mipango ya Serikali. Kwenye maji tuna matumaini makubwa na mradi wa Ziwa Victoria, tunaomba ukamilike.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, naomba nimalizie kwa kusisitiza kuhusu barabara ya lami kutoka Tabora-Ipole-Mpanda. Tunaomba fidia ilipwe mapema, barabara ijengwe mapema kuondoa adha wanayoipata wananchi amabo ni watumiaji wa barabara hiyo.
Design yake ifanyiwe mapitio ili tuta la barabara ya lami liwe juu…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kakunda muda wako umekwisha.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, namalizia, yaongezwe madaraja na makalvati…
NAIBU SPIKA: Naomba ukae tafadhali…
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: ...ili barabara itakayojengwa iwe ya kudumu. Naomba kuwasilisha, ahsante sana. (Makofi)