Parliament of Tanzania

Questions By: Hon. Ester Alexander Mahawe

Supplementary Questions
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Kwa kuwa, fedha za own source hazitoshi wakati mwingine kulipa hata posho za Madiwani, ni kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa kupandisha hadhi Kituo cha Afya cha Dongobesh ili kuondoa msururu mkubwa katika Hospitali ya Haydom kwa ajili ya wananchi wa Mbulu Mjini na Mbulu Vijijini?
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa eneo hili la Simanjiro na hasa eneo la Orkesumet ambako ametoa majibu Mheshimiwa Waziri kuhusiana na suala la maji katika eneo la Orkesumet limekuwa likiimbwa kuanzia mwaka 2005. Orkesumet ni eneo dogo tu tofauti na maeneo mengine ambayo yana shida kubwa ya maji. Lile ni eneo la wafugaji ambako akina mama wanatoka kwa saa zisizopungua nane kwenda kutafuta maji. Naomba kauli ya Serikali ni lini haidhuru wananchi wa Simanjiro katika Kata za Narakauo, Kimotorko, Emishie, Naberera, Kitwai, Lobosoiret watapata maji? Pia ni lini hasa mradi huo utaanza rasmi?
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza linasema kwamba kuna uhaba mkubwa wa watumishi wa kada ya afya, hasa katika Mkoa wa Manyara kwenye zahanati na vituo vya afya. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuhakikisha hilo nalo linatatuliwa?
Mheshimiwa Spika, swali la pili tuna upungufu wa dawa hususan Mkoa wa Manyara kwenye hospitali zake zote Je, Serikali ina mpango gani na hili maana afya za wananchi ziko hatiani? Ahsante sana.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa muda mrefu sasa Halmashauri nyingi nchini zimekuwa zikipoteza mapato ambayo yamepotea kupitia kampuni mbalimbali za simu kwa kutokulipa hizo service levy katika maeneo mengi nchini.
Je, ni lini sasa Serikali itazibana kampuni hizo ili ziweze kulipa hiyo service levy?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kutokana na Halmashauri nyingi nchini kuwa na vyanzo vichache vya mapato. Je, ni lini Serikali itaweza kufanya mpango wa kuziongezea Capital Development Grants Halmashauri hizo nchini? Ahsante.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri baada ya kero hiyo kurekebishwa lakini bado driver guides wanapofika pale getini wanatakiwa kuandikisha majina ya wageni ambao wanawapeleka Ngorongoro ama Serengeti. Kwa hiyo, hilo nalo bado linaleta usumbufu mkubwa kwa sababu counter inayotumika katika uandikishwaji pamoja na ku-submit zile risiti ni moja. Je, Mamlaka haioni kwamba kuna ulazima sasa na umuhimu wa kuongeza madawati yale ya kutolea huduma hiyo ili kuokoa muda wa wageni unaopotea pale getini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa biashara yoyote inahitaji huduma bora kwa wateja yaani customer care na hili limeonekana likikosekana maeneo ya geti la Lodware na Naabi Hill. Je, Mamlaka haioni kwamba wafanyakazi wale wanahitaji kupatiwa indoor training ya mara kwa mara ili kuweza kufanya utalii wa ushindani na nchi jirani ambako customer care iko juu? Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika maeneo ya Mkoa wa Manyara hasa Wilaya ya Kiteto na Simanjiro katika Kata za Makame, Ndedo, Lolera kwa upande wa Kiteto na Kitwai, Naberera na vijiji vya Namalulu hali ni mbaya, ule ukanda ni wa wafugaji.
Naomba tu kumuuliza Mheshimiwa Waziri ni lini sasa watu hawa wataweza kupata huduma hii ya mabwawa kwa ajili yao wenyewe pamoja na wanyama?
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali langu lilikuwa kuhusu ukosefu wa nyumba za polisi katika Mkoa wa Manyara ikiwemo Ofisi ya RPC. Ni lini sasa Serikali itaona kwamba kuna umuhimu wa Jeshi la Polisi kupatiwa nyumba ili waweze kufanya kazi yao kwa ufanisi.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba uniruhusu nimshukuru sana na kumpongeza Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuamua kujenga ukuta katika eneo lote ambalo Tanzanite inachimbwa katika Mkoa wa Manyara hususan eneo la Simanjiro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niruhusu nimshukuru na kumpongeza sana Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano Mheshimiwa Job Ndugai ambaye alimua kwa dhati kabisa kuunda Kamati Maalum kwa ajili ya kuchunguza upotevu wa fedha kupitia madini hayo ya Tanzanite yanayopatikana peke yake duniani eneo la Simanjiro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu ya nyongeza ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uzoefu unaonesha kumekuwa na upotevu wa pesa kwa sababu wageni wanaotoka nje wanaokuja kununua Tanzanite hawalipi VAT, lakini wazawa waliopo pale eneo la Simanjiro, ama Arusha na Manyara wao ndio wanaolipa VAT. Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu jambo hili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa muda mrefu kumekuwa na mgogoro unaohusiana na mitobozano hususan kwa wachimbaji wadogo wadogo katika eneo hilo la Mererani, ni nini sasa kauli ya Serikali ili kuzuia migogoro hiyo isiyo ya lazima? Ahsante.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Waziri amekiri kwamba kwa sasa Mfuko wa Barabara unatoa asilimia chache sana ambazo ni asilimia 30 kwa barabara za vijijini ambazo ni nyingi kuliko barabara zinazohudumiwa na TANROADS na TANROADS zinapata asilimia 70. Je, ni lini Waziri sasa ataleta mabadiliko ya sheria hii katika Bunge hili ili tuweze kunusuru barabara ambazo zinatumiwa na wananchi wengi ambao ni maskini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Waziri ameona suluhisho la kudumu ni kuanzisha Wakala wa Barabara zinazohudumiwa na Serikali za Mitaa kama ilivyo kwa TANROADS. Je, ni lini hasa Wakala huu utaanzishwa?
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa mlima Kilimanjaro ni kivutio kikubwa na kinachoingiza pesa za kigeni kwa kiwango kikubwa kama kilivyotajwa. Je, ni lini sasa Serikali itaboresha miundombinu ya upandwaji wa milima huo kama inavyofanyika katika nchi zingine za Brazil, kule Rio De Janeiro na Cape Town, South Africa kwa kutumia cable ili kuongeza mapato zaidi kupitia mlima huo?
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa ruzuku hii iliyotajwa hapa kila Halmashauri imejipangia namna gani itatumia hizo ruzuku na hakuna uniformity katika matumizi hayo, na kama ambavyo tulimaliza suala la upungufu wa madawati na maabara nchini, je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kutoa maagizo makali kidogo ili kumaliza suala hili la upungufu wa vyoo mashuleni?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; wanaoteseka sana katika suala zima la upungufu wa vyoo nchini ni hasa mabinti walioko kwenye shule za sekondari. Kila mtu anafahamu wanapokuwa kwenye mzunguko ule kidogo wanapata taabu kulingana na ukosefu wa vyoo tena vyenye maji safi.
Je, ni lini sasa hususani katika Mkoa wetu wa Manyara Serikali itachukua hatua ya kumaliza tatizo hili hasa katika shule ya Komoto na Bagara Sekondari pale Babati Mjini? Ahsante.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wahenga wanasema samaki mkunje angali mbichi. Nakumbuka zamani tulikuwa tunajifunza masomo ya kilimo katika shule za msingi na sekondari nchini, lakini kwa bahati mbaya sana masomo hayo yakafutwa. Sasa labda tupate Kauli ya Wizara ya Elimu ni kwa nini masomo haya yalifutwa na tunategemea vijana baada ya kumaliza vyuo vikuu ndio wanaoweza kupata sasa ajira kupitia kilimo na ufugaji wakati hawakuandaliwa tangu mwanzo?
Swali la pili ambalo linasema ni maeneo gani hasa yaliyoandaliwa na yaliyotengwa kwa ajili ya kilimo kwa ajili ya vijana hawa wanapohitimu masomo yao ya Vyuo Vikuu na kukosa ajira katika maeneo mengine? Ahsante.
MHE. ESTHER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina na maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa bajeti ya Wizara ya Elimu inapopangwa inahusisha wanafunzi wote wanaotakiwa kuanza elimu yao ya msingi na sekondari na kwa kuwa wazazi wa hawa wanafunzi wanakuwa tayari wamechangia bajeti kuu ili kuweza kusomesha wanafunzi hawa kwa kupitia elimu bure. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kuendelea kuondoa kodi na tozo ambazo sio lazima kwa wazazi hawa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa moja ya malengo ya fedha za mitihani ni pamoja na kutafsiri mitihani kazi ambayo kimsingi ni jukumu la Baraza la Mitihani na siyo kwamba wazazi hawa wanaosomesha watoto katika shule ambazo sio za Serikali ni matajiri. Je, Serikali haioni kwamba kwa kuondoa tozo hizo watapata nafasi ya wanafunzi wengine wengi kusajiliwa katika shule hizo? Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mkoa wa Manyara ni mkoa mkubwa tu na una wilaya tano na majimbo saba na haiwezekani kuwapeleka wazee wote katika kituo kimoja tu kinachopatikana Magugu. Je, ni nini juhudi za Serikali katika kuhakikisha Wilaya ya Hanang’, Simanjiro, Kiteto na Mbulu tunapata kituo kingine cha wazee? Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Asilimia 90 ya wanariadha wanatokea Mkoa wa Manyara, lakini pia wapo wengi na taarifa iliyosomwa hapo na Naibu Waziri ni kuanzia miaka ya tisini kurudi nyuma, wapo wengi, akina John Yuda Msuri, Fabian Joseph, Andrew Sambu Sipe; wote hawa rekodi zao hazijavunjwa mpaka sasa kwa kuwa walikuwa wameshiriki mbio mbalimbali za kimataifa. Swali langu la msingi lilisema; ni lini utaratibu wa kuwaenzi wanariadha hawa utafanyiwa kazi sasa? Muda mfupi uliopita tulizungumza habari hapa na Waziri wa TAMISEMI alijibu suala la Wakuu wa Mikoa na Wilaya wanaofanya vizuri kuwa recognized na kupewa vyeti, habari gani kwa ajili ya wanariadha hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, amejibu hapa Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba picha zao zitawekwa kwenye jumba la makumbusho, je, hiyo inatosha? Wapo wanariadha wengi ambao hali zao za kimaisha ni duni, naomba kujua wanafanyiwa lini mchakato wa kutambuliwa juhudi zao. Ahsante.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini pia niipongeze Serikali kwa kutuletea fedha hizo shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya unaoendelea hivi sasa, lakini pamoja na majibu haya mazuri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwanza kabisa kuna msongamano mkubwa bado katika Kituo hiki cha Afya cha Dongobesh kwa sababu ya huduma ambayo si nzuri sana kwenye zahanati zetu. Je, ni nini kauli ya Serikali wakati tukisubiri kukamilika kwa ujenzi ambao ndio kwanza umeanza wa Hospitali ya Wilaya ambao utapunguza msongamano kwenye kituo hicho cha afya kupeleka huduma ya vifaa tiba pamoja na watumishi kwenye zahanati zinazozunguka Kituo hiki cha Afya cha Dongobesh?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Tarafa ya Yaeda Chini haina kituo cha afya. Je, ni lini Serikali itapeleka Kituo cha Afya katika tarafa ya Yaeda Chini ambayo mioundombinu yake migumu na huko ndiko wanakoishi wenzetu Wahadzabe? Ahsante sana.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri na jitihada za Serikali, bado maeneo mengi ya Mkoa wa Manyara yana tatizo kubwa la mtandao. Ukiacha upatikanaji wa sauti, lakini bado kuna shida kubwa katika upatikanaji wa internet, kwa hiyo shughuli nyingi za Serikali zikiwemo hospitali, shule na ofisi mbalimbali zinashindwa kufanyika ipasavyo kutokana na ukosefu huo wa mtandao. Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha data zinaweza kupatikana katika Mkoa wa Manyara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni stendi ya Mji wa Babati ilihamia nje kidogo ya mji na tuna tatizo kubwa sana la mtandao katika stendi hiyo. Ni mtandao wa tigo peke yake ndiyo unaopatikana na kama tunavyofahamu shughuli zilizoko stendi ni nyingi na abiria ni wengi wanaotumia mitandao mbalimbali.

Je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba mtandao unapatikana katika stendi ya Mji wa Babati na ni lini labda pia Waziri yuko tayari kuambatana na mimi kuona tatizo hili kubwa katika Mkoa mzima wa Manyara. (Makofi)
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake lakini nimfahamishe tu kwamba miaka mitatu iliyopita wananchi wa maeneo ya Mruki, Hangoni, Sinai pamoja na Kwere walizuiwa na Halmashauri kuendelea kuendeleza maeneo yao yaliyohisiwa kwamba ndiko barabara itakapopita wakiwa wamefanyiwa tathimini nakuhadiwa fidia. Je, kwa kauli ya Serikali sasa wananchi hawa wanaruhusiwa kuendelea na majukumu yao ya kuendeleza maeneo yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa kuwa majibu ya Serikali pia hayajatoa time frame yaaani lini sasa upembuzi huo wa kina utakamilika. Je, Serikali iko tayari kusema ni lini upembuzi utaanza na kukamilika? Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, Tarafa ya Bashnet iliyopo Babati Vijijini haina kituo cha afya hata kimoja na kilichopo kinatoa huduma sawasawa na zahanati. Je, ni lini Serikali itakumbuka Tarafa ya Bashnet? Ahsante.

Hon. Dr. Tulia Ackson

Speaker

Legislative Role

Profile

Ask the Speaker / Comments

Ms. Nenelwa J. Mwihambi

Clerk of the National Assembly

Legislative Role

Profile

Ask the Clerk / Comments

View All MP's