| E-mail this to a friend | Printable version |
|
|||||
| Session No | Seating No | Contribution Date | Contribution To | ||
|---|---|---|---|---|---|
| 4 | 17 | 1 July 2011 | Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka 2011/2012 - Ofisi ya Waziri Mkuu na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa | ||
Mheshimiwa Spika, ninaipongeza Hotuba aliyoiwasilisha Waziri Mkuu na kuiunga mkono. Hata hivyo, yapo baadhi ya mambo ambayo yanahitjika kusimamiwa kwa karibu ili utekelezaji uweze kuwa wa ufanisi mkubwa. Mambo hayo ni kama ifuatavyo:- Mheshimiwa Spika, Wenyeviti wa Vijiji/Mitaa ndiyo Viongozi Wakuu katika ngazi ya mwanzo ya Uongozi wa Serikali, lakini walio wengi hawayaelewi vizuri majukumu yao, kutokana na kuchaguliwa na kutopatiwa mafunzo. Hivyo; ni muhimu sana kada hii ya uongozi ipewe umuhimu mkubwa wa mafunzo kwa sababu kero nyingi zinatokana na Wananchi wanaowaongoza katika maeneo yao; na hivyo hushindwa kuyakabili kutokana na kutozijua taratibu au baadhi ya sheria ndogondogo wanazotakiwa kuzitumia. Sambamba na hilo, baadhi ya Wenyeviti wa Mitaa/Vijiji wamekuwa vyanzo vya kero kwa kutumia nafasi zao vibaya kama vile utoaji wa vibali na uuzaji wa maeneo ya vijiji bila ushirikishi, kinyume na sheria na taratibu. Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kilimo ndiyo uti wa mgongo, ninashauri Wenyeviti/Serikali za Vijiji; ili tuweze kufaulu suala zima la Kilimo Kwanza, uwepo utaratibu wa kila Kiongozi wa Kijiji kuwa na shamba la mfano wa Kilimo Bora. Hii itasaidia Viongozi hawa wanapohimiza suala la Kilimo Bora, waweze kuelezea mifano waliyoifanya wao kwanza na Wananchi wengine watafuata. Aidha, lipo tatizo la Maafisa Ugani kutowajibika ipasavyo katika maeneo waliyopangiwa kutokana na kutokuwa na vitendea kazi kama vile usafiri wa kumwezesha kuyazungukia maeneo aliyopangiwa, hivyo kumfanya akate tamaa na yeye kuungana kuwa mwanakijiji. Ninaishauri Serikali iangalie namna ya kuwawezesha Watendaji hawa ili waweze kusimamia shughuli za kilimo katika maeneo yao. Mheshimiwa Spika, lipo tatizo la Watendaji wa Halimashauri kukaa eneo moja kwa muda mrefu (miaka 10 - 20), bila uhamisho, jambo ambalo linasababisha kuzoeleka na Wananchi na kuwa chanzo cha kutumika vibaya na wale wasioitakia mema nchi yetu. Ninaishauri Serikali, Watumishi wawe wanahamishwa ili kuzinusuru Halmashauri. Kada zinazotakiwa kuhamishwa ni Wakurugenzi, Waweka Hazina, Maafisa Utumishi, Maafisa Mipango na Madaktari. Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja. |
|||||