United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa imetoa pongezi kwa Serikali kwa kuanzisha Wakala wa Serikali wa Mtandao (E – Government) ambao unafanya kazi kwa ufanisi.
Pongezi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mheshimiwa Jasson Rweikiza mara baada ya Kamati hiyo kupokea taarifa kuhusiana na Wakala huo kutoka kwa Waziri Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora, Mheshimiwa Angella Kairuki.
Alisema Kamati hiyo inapongeza Wakala huo kwa kazi nzuri ya kuunganisha wizara na taaisi za Serikali kimtandao na kwamba utekelezaji huo una maana kubwa kwa Taifa na vilevile utasadia kubana matumizi ya Serikali.
“Kamati inaiona tukiendelea kufanya hivi tutafika mbali, tuimarishe Wakala wetu ili tufike mbali, pongezi kwa Serikali kwa kuona umuhimu wa jambo hili na hivyo kulitilia maanani,” alisema.
Kwa upande wake, Mheshimiwa Kairuki alisema lengo kubwa la kuanzishwa kwa mtandano huo ni kuratibu na kusimamia utekelezaji wa Serikali Mtandao kwa taasisi za Serikali ili kuhakikisha taasisi hizo zinatumia teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku.
Alisema pamoja na kwamba Wakala huo unatekeleza majukumu yake kwa ufanisi lakini bado unakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba wa rasilimaliwatu ambapo kwa sasa wapo wafanyakzi 94 wakati mahitaji ni wafanyakazi 372.