United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Kufuatia upungufu wa Chakula ulipo nchini Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji imeitaka Serikali iwahimize Wananchi kuweka akiba ya chakula cha kutosha hasa kwenye maeneo yaliyopata mvua chini ya wastani.
Akiwasilisha taarifa Bungeni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe Dkt Christine Ishengoma alisema katika utekelezaji wa majukumu katika kipindi cha mwaka Januari 2016 hadi Janauari 2017 Kamati imebaini kuwa kuna upungufu wa chakula katika Halmashauri 55, nchini huku bei ya chakula nchini imeendelea kupanda kutokana na athari za ukame zilizopelekea uzalishaji kidogo.
Kutoka na hali Mhe Ishengoma aliliomba Bunge liitaka Serikali kuchukua hatua za kukabiliana na upungufu wa chakula nchini ikiwemo kuwahimiza Wananchi kuweka akiba ya chakula kwenye maeneo yaliyopata mvua chini ya wastani
Pia, Mhe Ishengoma alisema Kamati inalishauri Bunge liitake Serikali Sehemu ya akiba ya chakula kilichohifadhiwa na NRFA kitolewe na kuuzwa kwa bei elekezi iliyowekwa na Serikali katika Halimashauri 55 zilizobainika kuwa na upungufu mkubwa wa chakula.
“Mbali na hilo kamati pia inalishauri Bunge liitake Serikali ihakikishe kuwa, mbegu bora zinazostahimili ukame na zenye kukomaa kwa muda mfupi zinapatikana na kuwafikia wakulima mapema kabla ya mvua za msimu wa mwezi Machi,” alisema.
Kwa upande mwingine Mhe Ishengoma alisema Kamati imebaini kwamba, pamoja na sababu nyingine, changamoto za sekta ya kilimo kwa kiasi kikubwa zinachangiwa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo kukosa mtaji wa kutosha kuwezesha benki hiyo kuketeleza majukumu yake.
Kutoka na hilo Mhe Ishengoma alisema Kamati inashauri Serikali kuiwezesha Benki ya Maendeleo ya Kilimo ili iweze kuisaidia sekta ya Kilimo kukabiliana na changamoto mbalimbali.
Katika hatua nyingine Mhe Ishengoma alisema Kamati imebaini kuwa Migororo baina ya Wakulima na Wafugaji huchangiwa kwa kiasi kikubwa na kutotekelezwa ipasavyo mpango wa matumizi bora ya ardhi na hivyo kusababisha muingiliano wa shughuli za kilimo na ufugaji.
“Pia, Kamati imebaini kuwa pamoja na hatua zinazoendelea kuchukuliwa, migogoro baina ya wakulima na wafugaji imeendelea kuongezeka na kusababisha uvunjifu wa amani, vifo na uharibifu wa mazingira,” alisema Mhe Ishengoma.
Kutokana na hali hiyo Mhe Ishengoma alisema Kamati inalishauri Bunge liitake Serikali kushirikisha ipasavyo makundi yote yanayohusika na migogoro ya ardhi.