United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti imeitaka Serikali kuhakikisha tozo ya ushuru wa bidhaa ya asilimia 10 inayotozwa kwa watoa huduma wa simu katika kutuma na kupokea simu usimfikie mteja.
Akisoma maoni ya Kamati kuhusu Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2016, Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, Mhe. Hawa Ghasia amesema Kamati yake inaunga mkono tozo hiyo lakini Serikali ihakikishe anatozwa Mtoa huduma na siyo Mpokea Huduma.
Aidha Kamati imeitaka Serikali kuanzisha utaratibu mara moja utakaokuwa unaonyesha katika simu ya mteja kodi na ushuru mbalimbali anaotozwa mteja kabla na mara baada ya kufanya muamala wowote.
Kamati hiyo pia imeishauri Serikali kutoendelea kuongeza ushuru wa bidhaa kwa vinywaji baridi vinavyozalishwa ndani ili kuwezesha sekta hii kuendelea kukua na kuleta manufaa makubwa kwa Taifa hususan kuongeza ajira.
Akizungumzia Muswada huo wa Sheria ya Fedha amesema una lengo la kufanya mabadiliko mbalimbali ya sheria zinazohusu kodi, ada na tozo mbalimbali ili kupata fedha za kugharamia bajeti ya mwaka husika.
Amesema hata hivyo mabadiliko yamekuwa yakihusisha sheria mama na kupendekeza Serikali kuangalia uwezekano wa kufanya mabadiliko kwenye sheria mama moja kwa moja badala ya kutumia Sheria ya Fedha.