United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamemchagua Mhe.Dkt. Tulia Ackson kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwa Naibu Spika wa Bunge la 11 baada ya kumshinda mpinzani wake kutoka Chama cha Wananchi (CUF) Mhe. Magdalena Sakaya.
Hatua hiyo imefikiwa baada ya Mhe. Dkt. Ackson kushinda kwa kura 250 ambazo ni sawa na asilimia 71.2 za kura halali dhidi ya mpinzani wake Mhe. Sakaya aliyepata kura 101 ambazo ni sawa na asilimia 28.8 ya kura halali.
Uchaguzi huo umefanyika leo, Mjini Dodoma ambao ulitanguliwa na uthibitisho wa jina la Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa Kassim.
Akiomba kura kwa wabunge Mhe. Dkt. Ackson alisema kuwa atajitahidi kuwatumikia wabunge wote bila kujali tofauti za kisiasa ili kuwaletea wananchi maendeleo.
Aliongeza kuwa atajitadi kumshauri vizuri Spika juu ya Sheria na Kanuni kwa kutumia uzoefu alionao kama Mwanasheria aliyebobea ili kuhakikisha haki inatendeka kwa wote.
Akimpongeza Mhe. Dkt. Ackson Tulia kwa ushindi alioupata, Mhe. Sakaya alisema kuwa matarajio yake na watanzania ni kuona nchi inakuwa na Bunge imara litakalo fanya kazi zake kwa uimara bila ubaguzi ili kuiletea nchi maendeleo.
Akitoa neno la shukurani mara baadaya kuchaguliwa Mhe. Dkt. Ackson alimshukuru Mhe. Rais kwa uteuzi aliufanya wa kumteua kuwa Mbunge na hatimaye kugombea nafasi ya Naibu Spika wa Bunge la 11.
“Naahidi nitawatumikia kama mtumishi wenu, tutafanya kazi kiufanisi na pia nitatumia weledi wangu katika kazi zangu kama Naibu Spika, naomba msisite kuniletea hoja zenu pale mnapokuwa nazo” alisema Mhe. Dkt . Ackson
Kabla ya kuchaguliwa kuwa Naibu Spika, Mhe. Dkt. Ackson alikuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali .
Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi
Kilosa (CCM)