|
|
| Home »Pm questions & answers |
|
| |
 |
E-mail this to a friend |
 |
Printable version |
|
 |
Hon Mohamed, Hamad Rashid[CUF] |
Mheshimiwa Spika ahsante sana, tarehe 9 Septemba, 2009, Tume ya Uchaguzi Taifa ilichoma moto shahada za Wapiga Kura pale Bohari Kuu Dar es Salaam.
Je, Waziri Mkuu angetueleza ni utaratibu gani Tume iliutumia ya kukusanya kadi hizo na kufikia idadi ya kuweza kuchomwa?
|
| Answer From Prime Minister |
Mheshimiwa Spika, nilitaka kusema akichelewa mtu kama Mheshimiwa Hamad Rashid Mohamed, usimruhusu mwache hivyo hivyo.
Itakuwa vigumu kujibu swali la Mheshimiwa Hamad Rashid Mohamed kwa sababu sina maelezo fasaha ambayo ningeweza nikayatoa na ni jambo kubwa kwa hivyo nafikiri ninachoweza kuahidi tu ni kwamba basi ebu niachie nilitazame niwasiliane na wenzangu tuone kilichotokea hasa ni nini na kama unavyosema sasa tunafanyaje, maana nikiamua tu kukupa blabla hapa nadhani haitasaidia sana.
|
 |
Hon Mohamed, Hamad Rashid[CUF] |
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa jambo lenyewe kama unavyosema Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kubwa na nakushukuru sana kwa hekima yako na busara yako uliyoitumia katika kulijibu hili swali la kwanza.
Je, huoni kwamba ni vyema kuwa jambo lenyewe ni kubwa tukaunda katume kidogo tukachunguza undani wa jambo lenyewe hasa kwa kutilia maanani kwamba Tume ya Uchaguzi ya Taifa imeshutumiwa sana kwa kutokuwa na uadilifu, ili kuisafisha hii Tume kwanini tusiunde katume kidogo kulichunguza jambo lenyewe ili tupate uhakika wake?
|
| Answer From Prime Minister |
| Mheshimiwa Spika, bado nitasimamia palepale kwamba naheshimu sana mawazo yake lakini mimi nafikiri busara nzuri ni kunipa nafasi nilifanyie kazi. |
 |
Hon Chegeni, Dr. Raphael Masunga[CCM] |
| Mheshimiwa Spika ahsante, Mheshimiwa Waziri Mkuu hivi karibuni kumetokea mtafaruku wa kimashindano ya kibiashara kati ya Tanzania Breweries na Serengeti Breweries, kitu ambacho kinapelekea baadhi ya maeneo kuleta uvunjifu wa amani. Mashindano haya ya kibiashara yanaweza kuwa na tija lakini kuwa na hasara kubwa sana kwa nchi na hasa kiuchumi. Je, Mheshimiwa Waziri Mkuu suala hili unalifahamu na kama unalifahamu ni nini mkakati wa Serikali wa kuzuia ushindani usiokuwa na tija kwa faida ya nchi? |
| Answer From Prime Minister |
Mheshimiwa Spika, naomba nijaribu tu kueleza kidogo juu ya jambo hili kwa sababu na lenyewe sina undani wake kwa sasa. Lakini anapozungumza kwamba inaweza kupelekea uvunjifu wa amani sasa unakuwa umeelekea katika jambo ambalo linataka nalo lifanyiwe kazi, ni kwa maana gani hasa tunalisema hivyo lakini mimi nadhani, kubwa kwanza ni kukubali tu kwamba tuko katika mfumo wa soko ambalo ni huru, makampuni mbalimbali ya binafsi yanaendesha shughuli zake kwa mujibu wa taratibu na Sheria zilizowekwa.
Ni kweli kumekuwa na hali ya mvutano na malumbano kati ya Serengeti Breweries pamoja na East Africa Breweries na Tanzania Breweries kwa ujumla; na nilipata mimi nafasi ya kukutana na Mzee Mark Bomani pamoja na mmoja wa wana hisa wakubwa sana katika ile kampuni na nikazungumza nao kwa kirefu sana na nilichowaasa mimi ni kwamba, kwangu mimi kwa kadri ninavyofahamu kama Mtanzania ni vyema bado Serengeti Breweries katika kulinda heshima na vilevile kutoa ile kiburi cha Mtanzania naye anapofanya vizuri kuendelea kuonekana kwamba anafanya vizuri badala ya kuingia katika mvuto wa kitu kinachofanya vizuri kwenda tena kukiuza kwa mtu mwingine ambaye mimi naamini mwisho wa yote itakuwa ni kuiua kabisa hiyo kampuni na tutajikuta hatuna faida tutakayoipata.
Mheshimiwa Spika, jambo hili alilielewa na mimi napenda niamini kwamba sidhani kama watakuwa wamebadilika sana kwa sababu tangu wakati ule sina taarifa za kutosha lakini naweza nikamwahidi Ndugu Chegeni kwamba kwa masilahi ya nchi yetu pengine ni jambo ambalo tunaweza tukajaribu kulifuatilia tena tuone limefikia wapi na tunaweza kushauri nini mbele ya safari.
|
|
Records 1 to 3 of 12 |
|
|
|
|
|